Seventh-day Adventist® Church

PASTOR LETTA'S OFFICIAL WEBSITE

Menu

JUMA LA FAMILIA 2018


WIKI YA 

NYUMBA YA KIKRISTO NA

 

NDOA

 

 Idara ya Uchungaji ya Kanisa la Waadventista wa Sabato

 

3 – 10 February 2018


Ujumbe kwa Wasomaji

 

Wapendwa katika Bwana

 

Pokeeni salaam nyingi kutoka katika idara ya Huduma za Familia ya Union zetu mbili za Tanzania (Northern Tanzania Union Conference na Southern Tanzania Union Mission). Masomo ya Nyumba ya Kikristo na Ndoa yana vipengele kumi. Tunapendekeza kwamba masomo mawili ya mwanzo yatumike katika Sabato ya kwanza, asubuhi na jioni. Na masomo mawili ya mwisho yatumike katika Sabato ya mwisho asubuni na jioni.

 

Masomo haya yameandaliwa na Idara ya Huduma za Familia ya Halmashauri Kuu ya Kanisa la Waadventista wa Sabato (GC) na kuletwa kwenu na Mchungaji Daniel Ndiegi ambaye ni Mkurugenzi wa idara ya Huduma za Familia, Northern Tanzania Union Conference kisha kuhaririwa na Mchungaji Hebert Nziku ambaye ni Mkurugenzi wa Huduma za Familia, Southern Tanzania Union Mission. Yametafsiriwa na Moseti Chacha wa kanisa la Waadventista wa Sabato Lemara – Arusha

 

Tunaomba washiriki wahamasishwe kuhudhuria vipindi vya masomo haya bila kuacha watoto, ili wote wafaidi mbaraka uliopo ndani ya masomo haya kwa pamoja. Kwa kadiri mtakavyokuwa mnapitia masomo haya, mtagundua kuwa muundo wa masomo unajumuisha watoto, yaani nusu yake inahusu watoto na nusu inahusu watu wazima.

 

Bwana awabariki.

Mjoli wenu

 

Mchungaji Daniel Ndiegi

Idara ya Huduma za Familia (NTUC)

Simu: +255 767 543 904/784 543 902

Baruapepe: dndiegi@yahoo.com


YALIYOMO:

Somo la 1: Kujenga Tabia Kwa Ajili ya Umilele.

Somo la 2: Mambo ya Kitoto ambayo Hayapaswi Kukatazwa.

Somo la 3: Familia Zinazolea Imani.

Somo la 4: Kuwasaidia Vijana Wetu Kukamata Injili.

Somo la 5: Nyumba ni kwa Ajili ya Kushirikiana.

Somo la 6: Jinsi ya Kumpenda Mwana wa Ngurumo.

Somo la 7: Nitawaokoa Watoto Wako. 

Somo la 8: Kama Mapacha Wangeweza Kuongea Nasi.

Somo la 9: Mwanga wa mungu Katika Macho ya Mtoto.

Somo la 10: Mfano wa Baba Mzuri Sana.


Somo la Kwanza

KUJENGA TABIA KWA AJILI YA UMILELE

Na Linda Koh

Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Familia Divisheni ya Asia Pasifiki na Idara ya Huduma za Familia NTUC & STUM

Mada kuu: Maandiko hufunua kazi muhimu ya wazazi kujenga tabia imara kwa watoto wao, tabia ambayo itasimama imara dhidi ya mivuto hasi ya ulimwengu.

Fungu kuu: Kumbukumbu la Torati 6:1, 2, 5-7; Mithali 22:6

Dondoo za uwasilishaji: kote katika orodha ifuatayo, nambari zilizo katika mabano yaani, (1), (2), (3) hutumika kuonyesha vitu kutoka kwenye kipengele kinachoitwa Mwangaza wa Hubiri ambacho kinaweza kutumika kama kilelezo. Nyongeza ya vielelezo vyako binafsi vitasaidia uwasilishaji.

Katika dunia ya mabadiliko, kupungua kwa tunu za kifamilia, kuzembea maadili, na ongezeko la idadi ya wazazi wasiokuwa na wenzi, kunasababisha hali ya kiroho ya watoto wetu iwe hatarini. Kwa hiyo ni muhimu wazazi kutenga muda na nguvu zao katika kujenga msingi wa tabia ya mtoto wao. Ni muhimu kwa sababu tabia ya kiroho ya mtoto itaundwa tu bila kujali hali ikoje. Huenda ikaundwa na wazazi Wakristo au itaundwa na ulimwengu. Ujenzi wa tabia haupaswi kufanywa kwa kubahatisha. Wanazuoni wa maadili kama Robert Peck, Robert Havighurst, na Lawrence Kohlberg (1) hutuambia kwamba utoto ndio kipindi cha muhimu cha kujengwa na kuundwa kwa tabia ya mtu. Hata hivyo, katika miaka saba ya kwanza msingi wa tabia ya mtoto huundwa. (Tazama ‘Kuzma’, 1989, uk. 3)

Tengeneza Mpango kwa ajili ya Ujenzi wa Tabia

Wasanii wenye vipaji na wajenzi hutenda kazi kwa kufuata mipango iliyo dhahiri. Mchongaji asiye na mchoro unaomwngoza hukatakata tu bila mpangilio. Mjenzi asiye na ramani hujenga nyumba iliyo dhaifu na isiyo na mvuto. Kwa namna hiyo hiyo, wazazi lazima wawe na mpango; mpango wa vile wanavyotaka tabia ya mtoto wao iwe. Unataka kujenga nini katika maisha yake? Tafakari maneno ya Yesu, “Maana ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia?” (Luka 14:28).

Wazazi Wakristo wanahitaji kuweka malengo mahususi kwa ajili ya malezi yao. Jenga taswira ya mtoto wako kama Mungu anavyomwona, katika upeo wa ukomavu wake. Je unamuona akitembea na Mungu, akishirikishana  muda na mali na wengine, akiwahudumia wale walio wahitaji, akijikana nafsi, au akimtumikia Mungu katika utume? Wazazi wakiwa na picha kama hizo akilini juu ya kile ambacho wangependa kitokee kwa watoto wao, wanaweza kubakia kwenye lengo na kutilia mkazo mawazo ya malezi ambayo yataongeza uwezekano wa watoto wao kukubali maadili yao na, kadiri wanavyokuwa watu wazima, wataunga mkono na kutamani malengo kama yale ya wazazi wao. (2)

Fundisha kwa kufuata Mwongozo

Wajibu wa wazazi umeelezewa wazi katika Torati 6:1, 2, 5-7. Mafungu haya huelezea wakati ambapo Mungu aliwaambia watu wake wawafundishe watoto wao uaminifu wa Mungu na kukuza kicho kwa Mungu katika nyumba zao. Maelekezo ya wazazi lazima yatolewe kwa uangalifu na kwa uaminifu. “Amri hizi ninazowapatia… wafundishe watoto wako.” Hii inahitaji kutayarisha fursa kadiri iwezekanavyo, na shughuli ambazo zinamvutia mtoto ili kumfundisha tunu muhimu na imani kama vile upendo, heshima, uaminifu, na ukarimu.

Wazazi pia wanahitaji kufundisha bila kukoma na kwa ustahimilivu. “Yanene uketipo nyumbani, utembeapo njiani, ulalapo na uinukapo.” Uundwaji wa mwenendo na mafunzo ya tabia haupatikani kwa jitihada zilizoitenga, bali ni kwa kurudiarudia kusikokoma. (3) Ikiwa kucheza pamoja katika bustani au kusoma kisa pamoja kutawapatia wazazi wakati wa “kuvutia” ili kuongoza na kumfundisha mtoto, basi fanya hivyo kwa namna yoyote ile. Hatupaswi kuacha fursa zipite eti kwa kuwa tulipofika mwisho wa siku tulikuwa tumechoka sana, au kwa sababu watoto wametingwa na michezo yao, au kwa sababu kila mtu anatazama Runinga.

Samweli alikuwa mmoja kati ya mifano bora ya uaminifu wa kiroho katika Agano la Kale. Alidumu kuwa mtiifu kwa Mungu maisha yake yote. Alikulia katika nyumba ya Eli wakati ambapo Eli alikuwa kuhani mkuu. Alimshuhudia Eli akiwapoteza wana wake kwa mambo ya dunia. Aliona kile Eli alichokosea na makosa aliyopaswa kuepuka. Kwa bahati mbaya, Samweli alishindwa kama Eli alivyoshindwa na aliwapoteza watoto wake kwa njia hiyo hiyo (angalia 1 Samweli 8:3). Kuwa kiongozi mkuu hakukuhakikishii kuwa mzazi bora. Mafunzo ya watoto huchukua muda. Eli na Samweli walikuwa na shughuli nyingi katika kumtumikia Mungu kuliko kuchukua muda wa kulea wana wao au kujenga nao mahusiano ya karibu na yenye mvuto. Walishindwa kutii amri ya kuwafundisha watoto wao “uketipo nyumbani na utembeapo njiani, ulalapo na uamkapo” (Torati 6:7)

Fundisha kwa Mifano

Kuna msemo wa zamani usemao, “Matendo hupaza sauti kuliko maneno.” Ili mafunzo yawe na matokeo bora, basi ni lazima yaanzie ndani ya wazazi. Wazazi wenyewe lazima wawe mifano ya tunu na imani wanazoshikilia kwa nguvu. Watoto wanakuwa na heshima kubwa kwa maagizo endapo wanashuhudia udhati katika vielelezo kutoka kwa mama na baba zao.

Katika Wafilipi 4:9, Paulo anaelezea dhana hii kwa uwazi zaidi, “Mambo mliyojifunza kwangu na kuyapokea, na kuyasikia na kuyaona kwangu, yatendeni hayo; na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.” Paulo alikuwa mfano mzuri kwa Wakristo wa Filipi kwa yeye mwenyewe kuwa sampuli ya ukweli ule ule aliouhubiri. Ndiyo maana kanisa la Filipi lilikuwa limesitawi na lenye furaha. Yote haya hutuelezea mambo mengi kuhusu wazazi. Kama unataka mtoto wako awe mkarimu, ni lazima kwanza uonyeshe ukarimu, kama unataka wampende Mungu na kuheshimu Sabato yake, lazima uwaonyeshe jinsi unavyompenda Bwana na kuitunza Siku Yake Takatifu.

Tambua Utu wa Mtoto

Katika Mithali 6:22 tunakutana na lile fungu maarufu ambalo Wakristo wengi wanaweza wakalikariri, “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha hata atakapokuwa mzee.” Kufundisha na kujenga tabia ya mtoto kunawahitaji wazazi kutambua umuhimu wa tofauti binafsi ndani ya watoto wao. Kuwafundisha watoto wako hakumaanishi kuwalea kama unavyowaona. Badala yake ni kuwalea kwa njia wanayopaswa kuenenda kwayo, ukidumisha karama kwa mtu mmoja mmoja au uthabiti wa maamuzi.

Katika kila mtoto ambaye Mungu anamweka katika mikono yetu, kuna uthabiti wa maamuzi, seti ya mwelekeo fulani uliojengeka au sifa bainishi zilizo binafsi. Ni muhimu katika kujenga tabia kugundua huo uthabiti wa maamuzi na kuelekeza mafunzo kadiri ipasavyo. Sio hekima kwa wazazi kuwafanya watoto wawe kama wao (wa wazazi). Wazazi wanahitaji kuwa na hekima na kuwa makini kufahamu jinsi Mungu alivyowaumba watoto wao, ili kwamba wakuze na kutoa kile kilicho bora kutoka kwao. Lakini wazazi wanawezaje kutambua vipaji ambayo watoto wanavyo?

Mithali 20:11-12 bado ni jibu bora zaidi, “Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; Kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili. Sikio lisikialo, na jicho lionalo, Bwana ndiye aliyeyafanya yote mawili.” Wazazi watagundua mwenendo wa mtoto wao watakapomchunguza kwa uangalifu kwa kutumia “masikio yanayosikia, na macho yanayoona.” Chunguza, sikiliza, na tenga muda wa kuwa na mtoto wako ili kugundua vile anavyopenda, mitazamo yake, uwezo na udhaifu wake. Msaidie mtoto kuwa kile Mungu alichomdhamiria kuwa.

Mfundishe Mtoto Wako Kufikiri

Pamoja na kwamba ni muhimu kufundisha kwa mfano na kwa mwongozo, pia ni muhimu zaidi kumfundisha mtoto wako kufikiria yeye mwenyewe. Katika ujenzi wa tabia, watoto wanapaswa kutiwa moyo kufikiri kuhusu maadili ya kijamii na ya kiroho kwa uwazi zaidi, ili kwamba aweze kufafanua tunu zake mwenyewe na kuona matokeo ya utendaji wa tunu hizo. Katika kitabu chake kinachoitwa, Help Your Child Learn Right From Wrong, (Msaidie Mtoto wako Ajifunze Jema na Baya), Sidney Simon anapendekeza kwamba wazazi watenge muda wa kuwasaidia watoto wao kujadili tunu, kuchagua imani na tabia zao, kuwapongeza, kuwajali, na kuenenda kwa usawa katika imani zao (angalia Hollander, 1980)

Katika nyumba nyingi za Kikristo mtoto huambiwa kile anachopaswa kufanya na kile asichopaswa kufanya, lakini hafundishwi kuelewa kwa nini. Ndani yake, mtoto huyo hukosa hisia za kusimama imara katika kile anachoamini kuwa cha kweli. Kwa hiyo ni muhimu kumtia moyo mtoto wako kufikiria kuhusu kwa nini tendo Fulani ni jema au ni baya. Namna moja ya kufanya hili ni kumwekea mtoto mitanziko mbalimbali na kumuuliza kile ambacho angefanya na kwa nini angekifanya. Kwa mfano, unaweza kuuliza, “Unaweza kufanya nini endapo familia yako haina chakula cha kutosha na majirani wanacho cha kutosha, lakini hawapo tayari kukupatia chochote?” msaidie mtoto wako kufikiria kuhusu suala hilo na kutetea matendo yake.

 

Nitawezaje Kumsaidia Mtoto wangu Kujitawala?

Wazazi, jaribuni kutowakinga watoto wenu kutoka kwenye matokeo ya maamuzi yao. Ikiwa wataamua kutenda kwa namna Fulani katika masuala Fulani kwa kufuata ushauri wako, waruhusu kufanya uchaguzi huo. Wanapofanya uchaguzi mbaya, wanaweza kulazimika kukabiliana na madhara yake. Lakini uzoefu huo unaweza kuwa ni fundisho la thamani. Endapo wazazi watamfanyia mtoto wao uamunzi kwa kila jambo, yeye hatahitaji kujenga hali ya kujitawala, au kufikiria jambo gani ni sahihi lipi sio sahihi. Watoto kama hawa wanapokabiliwa na hali nyingi zenye majaribu, hawatakuwa na uzoefu wa nyuma ambao ungekuwa umenoa utambuzi wao au kuwasaidia kuwa na ujasiri kwamba wanafanya uchaguzi bora. (4), (5)

Kujenga Hisia ya Uwajibikaji

Ni muhimu kwamba watoto wetu wajenge hisia ya kuwajibika kama itawabidi kutenda kwa maadili na kufikiri kwa kufuata maadili. Lakini ili kujenga uwajibikaji, watoto wanapaswa kuwa na majukumu. Hii inahusisha kutunza mali zao wenyewe, kufanya kazi zao za nyumbani, kutimiza ahadi zao, na kufanyia kazi pesa yao ya mfukoni wanapokuwa wamefikia umri wa kufanya hivyo.

Hata hivyo, tunapaswa pia kuwapatia fursa za kuwajali wengine, kuchangia maendeleo ya wanafamilia wengine na washiriki wa kanisani pamoja na jamii. Majukumu kama haya yanaweza kuwa ni kama yale ya kumsimamia mdogo wake, kumtunza mnyama wa nyumbani, kushirikiana katika kazi za nyumbani, kusaidia taasisi ya misaada (kama kushiriki mashindano ya kutembea kwa ajili ya kuchangisha kwa ajili ya walemavu), au kutenga pesa yake ya mfukoni kwa ajili ya shughuli yenye maana. Katika umri mdogo watoto wanaweza kufundishwa uwakili wa Mkristo, usimamizi wa hekima kwa kila alichopatiwa na Mungu, pamoja na kumrudishia zaka na kutoa sadaka kwa ajili ya kazi yake.

Mafunzo ya kuwajibika yanapaswa kuanza mapema. Hata watoto wa miaka miwili wanaweza kumsaidia mama kukunja vitambaa vya vyombo! Kadiri uelewa wa mtoto unavyokua, wazazi wanapaswa kutafuta kila nafasi ya kuelezea kwa nini tunawasaidia wengine. Hii huwasaidia watoto kukua kwa namna ya uwiano, wakiwajali wengine, badala ya kudai tu haki zao bila kuwa na hisia za wajibu wao.

Utumishi wa Upendo

Kuwafundisha watoto kuwa na tabia nzuri, kumpenda Mungu, kuwa wananchi wazalendo sasa na baadaye, na kujali maendeleo ya wengine kunahitaji maisha ya kujitoa kwa upande wa wazazi. Inahitaji upendo “usiotafuta ya kwake yenyewe” lakini huishi na kujitoa yenyewe. Inahitaji sana sio tu vitu vinavyoonekana ambavyo wazazi wanaweza kuwapatia watoto wao. Badala yake, inahitaji wazazi wanaofanya kazi kila mara kwa upendo na uvumilivu katika kuwafundisha watoto wao kwa matendo yao na kwa mitindo yao ya maisha maadili na tabia nzuri ambazo wanatamani kuwapatia watoto wao.

Mwangaza wa Hubiri

Moja (1): Hatua za maendeleo ya maadili ya watoto

Utafiti wa Lawrence Kohlberg juu ya maendeleo ya maadili kwa watoto unaonyesha kwamba kuna muundo wa maendeleo unaomvuta mtoto kufanya maamuzi mema au mabaya.

  • Hatua ya uchanga (miaka 0-2). Kabla ya miaka miwili mtoto ana uelewa mdogo juu ya mema na mabaya. Mwenyewe hufuata msisimko. Hata hivyo, wazazi na watu wazima humzoeza kuitikia neno “hapana” kama mwongozo wa vitu ambavyo ni vibaya.
  • Hatua ya chekechea (miaka 2-5). Katika hatua hii mtoto hufanya maamuzi kwa msingi wa kuona kama atapongezwa au kuadhibiwa kwa tabia fulani anayoionesha. Watoto hawa kwa ujumla hujijali wenyewe, wanafanya kile wanachotaka kufanya. Kama akikamatwa na kuadhibiwa kwa tabia mbaya, watajizuia kuifanya tena.
  • Hatua ya shule ya awali (miaka 6-12). Hii ni hatua ambayo mtoto huwa anafuata na kukubaliana na kanuni, hufuata kile kinachokubalika kuwa sahihi kwa sababu ndicho kitu kinachokubalika kikifanywa. Kohlberf anaita hatua hii kuwa ni hatua ya, “Kijana-mzuri, Binti-mzuri.” Watoto huenenda kulingana na sheria kwa sababu wazazi wao huwaonea fahari au wataona aibu endapo wenzao watawaona kuwa hawafanyi jambo hilo. Kwa hiyo hufanya kile kilicho sahihi ili kuwa “Wazuri.”
  • Hatua ya Shule ya msingi ya juu (miaka 12-14). Mtoto huenenda kwa kufuata kwa makini kanuni za maadili za mema na mabaya kwa kiasi cha kuwa mfuata sheria. Watoto hufuata kwa ushupavu sheria za mchezo na kuheshimu mamlaka. “Ni kinyume cha sheria!” Zaidi ya yote, hii inaweza kuwa hatua ya hatari zaidi ya kubainisha jambo lipi ni jema lipi ni baya, kwa sababu watoto hufuata mkumbo wa marafiki kuliko kufikiria mambo na kufikia uamuzi mzuri kuhusu kile anachopaswa kufanya.
  • Hatua ya shule ya sekondari (miaka 15-18). Hii ndiyo ngazi ya mwisho ambayo wale wanaopevuka hufanya maamuzi ya kimaadili kulingana na kanuni za maadili zilizo ndani yake kuamua endapo kitu Fulani ni chema au kibaya. Haujengeki katika kutii mamlaka kama kipofu. Vijana ambao wamejenga mtazamo sahihi wa maadili ndani yao hawataathiriwa na msukumo- rika au tamaa ya kujiridhisha nafsi.

Mbili (2): Kuandaa mpango wa Ujenzi wa tabia – kufuata mfano wa waliotangulia

Hapo zamani za kale katika nchi ya malezi ya watoto, kulikuwa na wajenzi wawili. Wote walikuwa wamepewa majukumu ya kujenga jengo. Wote walikuwa wamepewa ushauri kwamba waanze mapema. (“Mlee mtoto katika njia impasayo naye hataiacha hata atakapokuwa mzee” Mithali 22:6.) wote walipewa miongozo kutoka kwa Msanifu Mkuu. Wote walipewa namba ya simu ambayo Msanifu Mkuu anaweza kupatikana, wakapewa na maagizo wawe wanawasiliana naye. Na wote walikuwa na vitendea kazi vilivyohitajika kumaliza kazi hiyo.

Mjenzi wa kwanza alijua kwamba wajibu ni wa kwake, na alijua dhahiri ushauri, lakini alipoanza kusoma miongozo akasema, “Maelekezo haya ni ya jumla sana. Ni vigumu kuhusianisha miongozo hii ya zamani na hali ya sasa.” Na mipango iliyokuwa imeelezewa kwa undani zaidi ilionekana haiwezekani. “Haiwezekani nijenge kwa namna hii kwa sababu ya aina ya ulimwengu ninaoishi na kwa sababu ya majukumu mengi yanayonisonga. Hata hivyo, ninataka kujua kwa hakika ni kwa nguvu kiasi gani na ni mara ngapi ninapigilia msumari ili kuhakikisha unaingia vizuri, na mipango hii sio mahususi kabisa. Sina muda wa kuanza kumpigia Msanifu Mkuu kila wakati. Atanionaje nikimsumbua kwa vitu vidogo kama hivi?” kwa hiyo akafuata njia yake, na akajenga hapa kidogo na pale kidogo. Alijenga pale ratiba zake zilipomruhusu, tena alipojisikia. Jengo lake likakua, lakini likaanguka ilipokuja dhoruba.

Mjenzi wa pili aliuchukulia kwa makini wajibu wake wa kujenga. Ili kuelewa vyema ushauri wa Msanifu Mkuu, alisoma miongozo kuanzia mwanzo hadi mwisho, akichagua kanuni zile ambazo angetumia kutengeneza mipango yake ambayo ingetimiza mahitaji yake. Alijifunza miundo iliyotengenezwa na wajenzi wengine waliofanikiwa, badala ya kuifuata tu kama kipofu, alichunguza kanuni za usanifu ambazo angezifanyia kazi kwa hali yake ya kipekee. Kazi nzuri iliyoje! Ingelikuwa rahisi tu kufuata kama kipofu kile wengine walichofanya.

Lakini katika miongozo ya Msanifu Mkuu alikuta changamoto hii: “Tazama, Bwana, Mungu wako, ameiweka nchi mbele yako; haya panda, itamalaki, kama Bwana, Mungu wa baba zako, alivyokuambia; usiogope wala usifadhaike.” (Kumbukumbu la Torati 1:21). Na akajipa moyo, akachukua vifaa vyake, na kuanza kujenga. Aliendelea kuwasiliana mara kwa mara na Msanifu Mkuu. Hakuogopa kukiri kwamba alikuwa na upungufu wa maarifa na hivyo kuomba msaada. Alishukuru kwamba alipewa namba ya kupiga moja kwa moja!

Hakufanya kazi iliyo kamilifu, hasa katika siku za awali ambapo alikuwa bado mgeni kwenye kazi hiyo. Ilimchukua muda kujifunza. Aligonga misumari kadhaa iliyokua imepinda. Kuna wakati alikosea kujenga ukuta mara moja au mbili hivi. Lakini hili lilipotokea alisema, “Samahani” na akaanza tena. Badala ya kuficha makosa yake, aliyarekebisha mara tu alipoyagundua. Pamoja na kwamba ilimchukua muda zaidi kidogo, na uvumilivu lakini matokeo yalikuwa ya kuridhisha, kwa sababu jengo lilikua karibu na kuwa kamili.


Baada ya miaka kumi na nane ya kupanga, kugonga, kupaka rangi, jengo pamoja na kwamba halikuwa limekamilika kabisa, lilikuwa tayari kusimama lenyewe. Na lilisimama, na kuhimili upepo na dhoruba. Watu walipokuja kupata joto kwenye hilo jingo, walilipenda kuanzia ndani hadi nje. Na Msanifu Mkuu akasema, “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako.” (Mathayo 25::21). Na alifanya hivyo..

Tatu (3): Mzee mmoja alisema, “Nilipokuwa kijana mdogo mtu Fulani alinipatia tango likiwa ndani ya chupa. Shingo ya chupa ilikuwa ndogo sana, na tango lilikuwa kubwa sana. Nikajiuliza jinsi lile tango lilivyoingia ndani ya ile chupa. Siku moja nikiwa nje ya bustani, niliona chupa iliyokuwa imeingizwa tango dogo la kijani. Ndipo nilipoelewa. Tango lilikua na likawa kubwa likiwa ndani ya chupa.” Kujenga tabia nzuri au kukuza tabia mbaya ni kama tango ndani ya chupa. Endapo tabia zitarudiwa wakati watoto wakiwa wadogo, itakuwa vigumu kuvunja watoto watakapokuwa wamekua.

Nne (4): Kay Kuzma alielezea uzoefu huu. “Nilikuwa na nyumba ya kukuzia mimea mwaka fulani na nyanya nilizopanda zilikua utadhani magugu, lakini mimea yake ilikuwa myembamba kiasi kwamba ilibidi nizitegemeze. Baadaye niliona mmea mdogo ukikua nje ya nyumba hii ya mimea, labda kutoka kwenye mbegu iliyoanguka. Sikuweza kuamini tofauti kati ya mimea hii. Mmea wa nje ulikuwa mnene na wenye nguvu. Hii ikanishawishi umuhimu wa hali ya hewa ya upepo. Pale mambo yanapojitokeza kwa urahisi sana kwa mtoto, hakuna funzo la kukuza tabia kama vile ujasiri, uvumilivu, au uangalifu katika matumizi mbali mbali. Kama hapakuwa na maumivu, hakuna haja ya huruma.”

Tano (5): Kay Kuzma anaeleza wakati ambapo binti yake Karrie alipoamua kutokwenda na familia katika safari maalum. Tiketi za ndege zilinunuliwa kwa ajili ya wanafamilia kwa gharama maalum. Baadae Karrie alibadili mawazo na kuamua kwenda tena. lakini nauli ya ndege hata hivyo, ilikuwa imeongezeka. Ilimbidi Karrie kulipa tofauti ya $200 kutoka kwenye akiba yake mwenyewe. Lilikuwa ni somo lililokuwa ghali, lakini Karrie alikiri kwamba lilikuwa somo la thamani.


SOMO LA PILI:

MAMBO YA KITOTO AMBAYO HAYAPASWI KUKATAZWA

Na Karen & Ron Flowers

Wakurugenzi, Idara ya Huduma za Familia, Konferensi Kuu nIdara ya Huduma za Familia NTUC & STUM

Mada Kuu: Dhana kuu ya kuwa mtu mzima ni kuendeleza masomo ya maisha na mahusiano uliyojifunza katika utoto.

Fungu Kuu: 1 Wakorintho 13:11; Mathayo 18:15-17

Dondoo za Uwasilishaji: Pamoja na kwamba watu wazima watapokea mbaraka kutoka kwenye ujumbe huu, walengwa ni wale wanaopevuka, vijana wanaoelekea utu uzima. Pote katika mtiririko huu, namba zilizo katika mabano (1), (2), (3) zitamaanisha mifano kutoka kwenye kipengele kinachoitwa Mwangaza wa Hubiri. Nyongeza ya mifano yako binafsi itakuza uwasilishaji.

Hali ya kiroho ya watoto wetu ipo hatarini katika dunia hii ya mabadiliko, kufifia kwa maadili ya kifamilia, kuzembea maadili, na ongezeko la idadi ya wazazi wasiokuwa na wenzi. Kwa hiyo ni muhimu wazazi kutenga muda na nguvu zao katika kujenga msingi wa tabia ya mtoto wao. Ni muhimu kwa sababu tabia ya kiroho ya mtoto itaundwa tu bila kujali chochote. Huenda ikaundwa na wazazi wa Kikristo au itaundwa na ulimwengu. Matengenezo ya tabia hayapaswi kuchukuliwa kwa bahati nasibu tu. Mchungaji, mwanafalsafa na mwandishi wa vitabu Robert Fulghum anasema kwamba mambo ya muhimu aliyohitaji kujifunza katika maisha yake, alijifunza akiwa chekechea.

Haya ni baadhi ya mambo niliyojifunza: Shirikiana kila kitu. Usipige watu. Rudisha vitu pale ulipovikuta. Safisha uchafu wako mwenyewe. Usichukue vitu ambavyo siyo vyako. Omba samahani unapomuumiza mtu. Nawa mikono yako kabla hujala. Mwaga maji ukimaliza kujisaidia. Biskuti za moto na maziwa ya baridi ni vizuri kwa ajili yako. Ishi maisha yenye uwiano, jifunze kidogo na fikiria kidogo na chora, paka rangi na uimbe na kucheza muziki, na cheza michezo na kufanya kazi kila siku. Lala kila siku mchana. Unapokwenda matembezi, kuwa makini na magari, shikaneni mikono, na msiachane. Kuwa makini na usishangae shangae. Kumbuka mbegu ndogo kwenye kikombe: mizizi huenda chini na mmea huenda juu na hakuna anayejua hasa ni kwa namna gani au ni kwanini, lakini hata sisi tupo hivyo. Samaki, panya buku na panya weupe na hata mbegu ndogo vyote hufa. Hata sisi pia. (All I Really Need to Know I Learned in Kindergarten, 1988, uk. 4, 5)

 

Tunapokuwa watu wazima tutafanya vyema kukumbuka masomo rahisi ya mahusiano tuliyojifunza tukiwa watoto. Fulghum anaendelea kusema: Hebu fikiri, hata dunia ingekuwa bora kiasi gani, ingekuwa wote duniani tunapata biskuti na maziwa karibia saa tisa kamili kila mchana na kisha kulala na viblanketi vyetu kwa ajili ya usingizi kidogo. Au kama serikali zote zingekuwa na sera ya kurudisha vitu pale vilipokuwa na kusafisha uchafu wake wenyewe. (uk 5, 6).

Yesu alisema jambo linalofanana na hilo kuhusu kuwa kama watoto: “Bali Yesu akawaita waje kwake, akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu, wala msiwazuie, kwa kuwa watu kama hao ufalme wa Mungu ni wao. Amin, nawaambia, Mtu ye yote asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hauingii kamwe.” (Luka 18:16, 17). Hakuna mashaka katika hatua hii ya maisha yenu mnavutiwa zaidi na tamko la mtume Paulo katika 1 Wakorintho 13:11, “Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto.” Mafungu haya mawili yanawezaje yote kuwa kweli? Kwa upande mwingine, kuwa kama mtoto kumependekezwa na Kristo mwenyewe. Lakini hapa, Paulo anasema mambo ya kitoto yanapaswa kuwekwa kando. Kuna tofauti katika mafundisho ya Yesu na mafundisho ya Paulo? Au sehemu zote hizi zinawasilisha ukweli?

Mafumbo ya Maandiko

Maandiko wakati mwingine huwasilisha kweli ambazo ni kinzani, kama vile: watawaacha baba na mama, na bado waheshimu baba na mama; yoyote atakaye kuokoa uhai wake ataupoteza, lakini yoyote atakayeupoteza uhai wake kwa ajili yangu ataupata; wa kwanza atakuwa wa mwisho na wa mwisho wa kwanza; mkubwa atakuwa mtumwa. Matamko kuhusu kuwa kama mtoto yaliyotolewa na Yesu pamoja na Paulo hutoa fumbo lingine. Mara nyingi katika kujifunza mafumbo kama hayo tunagundua ukweli uliojificha.

Kukua

Wale wanaojifunza kuhusu ukuaji na maendeleo ya mtoto wameweka chati ya makuzi ya mtoto kuanzia tumboni hadi utu uzima. (1) Upo katika upande wa mwisho wa mabadiliko kati ya utoto na majukumu ya maisha ya utu uzima. Sehemu kubwa ya kazi binafsi unazojihusisha nazo, zinahusika kukufanya ujitenge na wazazi wako, uwe mtu wa pekee, ukitengeneza mitazamo yako binafsi juu ya vitu, na mfumo wako wa maadili. (2)

Ulizoea kufikiri kama mtoto, kutafakari kama mtoto. Ulikua katika kipindi ambacho mawazo yako hayakukuruhusu kutambua kwamba ile glasi nyembamba ndefu haikuwa na ujazo wa maji mengi zaidi kuliko ile fupi nene. Uelewa wako wa ulimwengu uliokuzunguka na mitanziko yake ulikuwa ni wa namna iliyo rahisi. Kila kitu kilikuwa cheusi ama cheupe, hapakuwa na vivuli vya kahawia. Katika muktadha wa kiroho pia, imani yako ilikuwa rahisi. (3)

Lakini sasa unaacha mambo ya kitoto. Utu uzima unaonekana kuvutia, wa kusisimua, na sasa unatamani kuweka utoto nyuma yako na kuendelea na maisha yako. Upo katika hatua ya kufanya baadhi ya maamuzi ya muhimu zaidi ambayo utafanya katika maisha yako, maamuzi kuhusu aina ya ajira utakayojihusisha nayo, maamuzi kuhusu mwenzi wa maisha, maamuzi ambayo yataamua mawimbi ya bahari ya maisha yako.

Unatathmini dini ya wazazi wako katika madaraja mapya. Maswali yako yamebadilika kutoka katika maswali ya utoto kwamba “Mungu anaishi wapi na anafananaje?” hadi kwenye “Ninafahamuje kwamba Mungu kwa hakika yupo na je ninamhitaji kweli katika maisha yangu?” Maswali ya akili ya mtu anayesogelea utu uzima. Kama haya ndiyo maswali yaliyopo akilini mwako leo, upo pale unapopaswa kuwa hasa kama Mkristo anayesogelea ukomavu. Ndio maswali ambayo sisi watu wazima tunapaswa kutafakari na kufanya maamuzi kwa ajili yetu sisi wenyewe, na tunataka kuwa pamoja nawe pale unapofanya tathmini yako ili kukupatia msaada wowote ambao ushuhuda wetu unaweza kukupatia. Hata hivyo, hatuwezi kujifunza au kufikiri kwa ajili yako. Hii ni sehemu ya mchakato wa kukua.

Vitu ambavyo havipaswi kuachwa

Katika ushupavu wa miaka ya 1800, kadiri uamsho ulivyosambaa katika Marekani, kundi moja lilitafsiri maneno ya Yesu katika Mathayo 18:3 kwa uhalisia. Walitembea wanne wanne, wakiwaigiza watoto na kubwabwaja kwao. Lakini Yesu hazungumzii matendo ya kitoto. Yesu na Paulo wote wako sahihi. Utoto huupatia nafasi utu uzima katika maendeleo ya kimwili, kiakili, na kihisia. Uelewa wa kawaida pia hukua. Kiroho tunakuwa watu wazima, lakini hali yetu ya kiroho inakuwa na vimelea rahisi kama vya mtoto. Unaachana na uchanga kwa ajili ya ukomavu, lakini sehemu ya ukomavu huo ni kuendeleza dhana ya kuwa rahisi bila waa, dhana inayodhihirishwa katika utoto. Kwa hiyo, unapojaribiwa kutupa vitu kama vile vigari vya kuchezea ambavyo havisisimui tena, zingatia kutunza tabia chache za kitoto kwa ajili ya baadae.

 

  1. Watoto hupenda zawadi na huzipokea kwa furaha. Hawachunguzi zawadi na kujiuliza imetoka duka gani. Hawaulizi, “Ameipata hii kwa bei punguzo, au amelipia gharama kamili?” Na hawasumbuliwi na wazo kwamba sasa ni lazima na mimi nimnunulie. Nitapaswa kutoa kitu kinacholingana na kile nilichopewa kwa thamani.

 

Ufalme wa mbinguni ni wa watu kama hawa kwa sababu wanaupokea kama zawadi, kwa sababu Mtoaji anawapenda na anawapatia bure. Unapoingia katika changamoto za maisha ya utu uzima, inawezekana ukajaribiwa kufirikia kwamba hili ni rahisi sana, na kwamba kuna kitu ambacho unapaswa kufanya ili uokolewe. Lakini kumbuka kwamba, swali la mafarisayo siku zote lilikuwa swali lisilokuwa sahihi. Siku zote waliuliza, “Nifanye nini …?” hata hivyo Yesu, alishughulikia swali tofauti, swali la msingi la uwepo wa wanadamu. Mimi ni nani? Jibu la Mungu kwa swali hilo ni kwamba alikuweka ndani ya Kristo na kuwatamka kuwa wana na binti zake. (4) Mlisulubiwa na Kristo (Gal. 2:20), mlikufa pamoja naye (Rum. 6:5-8), mlifufuliwa pamoja naye na sasa mnaketi naye katika mahali pa mbinguni (Efe.2:5, 6). Kwa mtazamo unaofaa wa uhalisia wa kiroho sasa anawataka kuenenda kama watoto wa nuru (Efe. 5:8), kuenenda kama wanaomstahili Bwana, mkizaa matunda katika maisha yenu (Kol. 1:10), kuwa wa kawaida katika maisha ya kila siku kwa uhalisia wa kile alichowaitia kuwa katika Kristo.

 

  1. Watoto hutenda kwa hiari, wakitenda mara moja kwa kile wanachoelewa. Hisia zao hazijasongwa na mawazo ya umakini na ukosoaji. Hawana mifumo ya kujitetea dhidi ya aibu au kuficha aibu zao. (5)

 

Ni mabadiliko gani ambayo yangeweza kuletwa na kizazi chako katika makanisa yetu endapo ungedumu kuwa muwazi katika hali yako ya unyonge! Kama ungetualika wote, ukionesha mfano wewe mwenyewe kwa kuvua sura ya nje na kushirikishana kwa uwazi na wengine wote ile furaha uliyo nayo, na mashaka yetu wote. Kingeweza kuwa kizazi ambacho kitaongoza kanisa katika hisia mpya za jumuia. Tunahitaji usaidie kutufanya kuingia “kila mmoja kwa mwingine” katika ngazi zote ambazo zilikuwa katika uelewa wa kanisa la awali. Ni rahisi kwa watu wazima kuonyeshana vidole, kuoneana wivu, hata kudanganyana na kusengenyana. Usipoteze uwezo wako wa kuleta muafaka, kuungama dhambi zenu wenyewe kwa wenyewe, kuhudumiana, kuchukuliana mizigo, au kujengana. Tunawahitaji mbaki kuwa tayari kuwa na hiari ya kuitikia kweli yoyote ile. Katika makanisa yetu mengi tunahitaji kuwa na hiari zaidi, kumsifu Mungu zaidi, na kudhihirisha kufurahishwa kwa Bwana.

 

  1. Watoto hawaachi kuuliza maswali. Watu wazima mara nyingi huchoshwa na maswali ya watoto: “Baba, nini kinafanya anga liwe bluu/samawi?” “Je minyoo wanalala usiku?” “Nini kinachofanya kucha za miguu kuwa ngumu kuliko za vidole?” “Tutafika saa ngapi?” (6)

 

Kizazi hiki kimejawa na maswali. Maswali ambayo yanaweza kuwakosesha raha watu wazima, kuwaogopesha, wakati mwingine kuwakasirisha kwa sababu wanaweza kuhisi unatishia nguzo za imani yao. Mara nyingi hawaridhiki na majibu mafupi, ya kawaida. Mnatia changamoto fikra zetu. Mnatusonga kwa maeneo na mawazo yasiyo mazuri kuhusu masuala ambayo tusingependa kuzishughulikia. Hata hivyo, hii inaweza kuwa karama bora zaidi ambayo ujana wenu ungeleta kanisani. Mnaweza kuwa kizazi kinacholifanya kanisa hili kuwa harakati inayokataa kukukubaliana tu na orodha ya misingi ya imani ambayo tumekuwa tukikariri. Tafiti zinaonyesha kwamba orodha kama hizo hupoteza baadhi ya maana zake kadiri vizazi vinavyopita. Hukosa maana kubwa katika maisha yenu na zitakuwa na maana ndogo zaidi kwa watoto wenu kiasi kwamba hazitakuwa zimetoka moja kwa moja kwenye neno la Mungu. Kwa hiyo, endeleeni kuuliza maswali. Mungu anaweza kuwasiliana na akili zinazouliza maswali.

 

  1. Watoto ni wenye kuamini, na ni tegemezi. Katika umri mdogo, mtoto huutazama ulimwengu kwa jicho la kushangaa na lenye mategemeo makubwa, na anaishi kwa furaha ya kuamini. Watoto ambao imani yao haijavunjwa kwa kutelekezwa, kunyanyaswa au kufanyiwa ukatili huendelea kuwa na ujasiri wa imani katika maisha yao. Watoto hawasumbuliwi na dhana kuwa wao ni tegemezi. Majanga yanapokuja, hawajifanyi kuwa wanajitosheleza. Wanawageukia wale wanaowaamini kwa imani rahisi tu kwamba kutakuwa na mwitikio.

 

Wengi wetu kama watu wazima tumekuwa wachovu, wenye mashaka, wenye kubeza. Kama mafarisayo, tumegeukia kujitumainia nafsi zetu kama kitu pekee tunachoweza kutegemea katika ulimwengu wetu. Hata hivyo, Yule mwenye kiburi na mwenye kujitumainia nafsi hawezi kuingia katika Ufalme wa Mbinguni. Ndio maana kisa cha Yesu na watoto, ambacho kinakubaliwa ulimwenguni kote kuwa kisa kinachofurahisha zaidi katika Agano Jipya, ndio pia kwa maana yake halisi ni moja ya changamoto zinazosumbua zaidi. Ulikuwa ni mwaliko kwa watoto. Pia lilikuwa ni kemeo kwa wale wenye kiburi na kujiona wenye haki.

 

Ni muhimu kadiri mnapopita katika kipindi hiki cha maisha yenu kwamba mjitenge kutoka kwetu sisi kama wazazi wenu na kuwa watu binafsi mnaojitegemea. Jambo hili ni muhimu zaidi kwa ajili ya ustawi wetu wote. Lakini jitahidi usipoteze uwezo wako wa kuomba msaada na kukubali matendo ya ukarimu unapokuwa katika nyakati za shida. Katika maisha utapitia vipindi ambavyo utawahudumia wengine na vipindi ambavyo utahitaji mtu akuhudumie. Kumbuka, hakuna kosa katika kuhitaji msaada wa mwingine, ndio maana Mungu alitufanya kuwa familia. Kujifunza ni kwa jinsi gani na lini kuwategemea wengine kunafanya uelewa wetu wa kumtegemea Mungu kuwa rahisi zaidi. Unaweza kutusaidia wote kupita hali yetu ya kutegemea nafsi zety wenyewe na kuwa na imani kama ya mtoto, na kuelekea kutegemea neema ya Mungu kikamilifu.

 

  1. Watoto wanapenda kucheza. Mara nyingi kwetu sisi watu wazima, maisha huwa ni biashara nzito isiyokuwa hata na muda wa kucheza. Wengi wetu tulikuwa na dhana kwamba kucheza hakuna thamani, kitu ambacho hauna muda wa kufanya. Lakini tunapenda kufikiri kwamba Kristo alikuwa mchezaji, mwenye hiari, kwamba Yeye na wanafunzi Wake walizama majini walipokuwa wakitembea pembezoni mwa bahari ya Galilaya au mto Yordani.

 

Muda si mrefu maisha yetu yanagubikwa na mizigo ya maisha ya utu uzima. Haiwezekani kutafakari sasa mikunjo na mahangaiko ambayo maisha yanatuletea. Baadhi yanatokana na sisi wenyewe, mengine yanakuja kwa namna ambayo sisi wenyewe hatuwezi kufanya chochote kuyazuia. Katika yote hayo, tenga muda wa kuomba na kucheza. Tunahitaji kizazi chenu kisitufanye kuchukulia maisha kwa uzito kiasi kwamba tusahau kucheza, kufurahi na kusherehekea vitu vizuri, hata tunaposaidia kubeba mizigo ya wengine pamoja. Yesu alionyesha tamaa yake kwa watu wake aliposema, “Nalikuja ili muwe na uzima, tena muwe nao tele” (Yohana 10:10). Maisha Aliyoishi kwa ujazo kamili ni urithi kwa watoto Wake.

 

Hitimisho

 

Mawazo ya Fulghum yanatupatia changamoto. Dunia ingekuwa bora kiasi gani endapo tungeutazama kwa urahisi, unyenyekevu, imani na utegemezi kama mtoto, kama wote tungepata biskuti na maziwa alasiri na kisha kulala na kwenye viblanketi vyetu kwa ajili ya usingizi? Kama serikali zote zingekuwa na sera ya msingi ya kurudisha vitu kila mara pale vilipokuwa na kusafisha uchafu wao wenyewe. Vipi kama wote tungekumbuka, bila kujali umri wetu – “tunapokwenda nje duniani, ni vyema kushikana mikono na kubakia katika umoja?”

 

Kwa namna moja unaacha utoto nyuma, kwa namna nyingine unakuwa na fursa ya kufuatana na baadhi ya utoto katika utu uzima. Mtu na asiudharau utoto au ujana wako, ni ufunguo wa kuishi maisha yenye mafanikio kama Mkristo. “Tusipokuwa kama watoto wadogo, hatuwezi kuingia katika Ufalme wa Mbinguni.” Kufanana kwako na mtoto ndio kunakoweza kuwa sifa yako bora zaidi na zawadi yako bora zaidi kwetu sote.

 

Mwangaza wa Hubiri

 

Moja (1): Makuzi ya hatua kwa hatua yanaweza kuwa kwa namna Fulani tofauti kutoka kwa mtoto mmoja hadi mtoto mwingine, kulingana na mazingira ya mtoto, hata hivyo, tabia mbali mbali za maendeleo huonekana kufanana kwa watoto. Huku akikiri kwamba kukua ni kamili, Berger (1994), kwa mfano, anaorodhesha maendeleo ya afya ya kijamii, kujitambua, na akili ya kijamii kupitia vipindi vya kabla ya kuzaliwa, miaka miwili ya kwanza, miaka ya kucheza, miaka ya shule, ile ya kupevuka, ya utu uzima wa awali, utu uzima wa kati, na ya utu uzima wa mwisho.

 

Mbili (2): Robert Havinghurst ameorodhesha majukumu kumi yanayohusu ukuaji na kupevuka kwa vijana:

  1. Kuanzisha uhusiano uliokoma na jinsia zote mbili.
  1. Kuanzisha wajibu mkomavu katika masuala ya jinsia.
  1. Kuukubali mwili wake binafsi.
  1. Kukubali uhuru wa kihisia kutoka kwa wazazi.
  1. Kutengeneza mpango kwa ajili ya uhuru wa kiuchumi.
  1. Kuchunguza na kujiandaa kwa ajili ya kazi au utaalamu Fulani.
  1. Kujifunza mtiririko wa maisha yake binafsi au ya kifamilia.
  1. Kutengeneza stadi za kijamii ili kutambua tabia zinazofaa katika hali mbali mbali.
  1. Kutengeneza tabia inayofaa na stadi za kijamii ili kuchukua nafasi yake kama mwanajamii mtu mzima.
  1. Kuanzisha kanuni zinazoweza kufanyiwa kazi za maadili binafsi. (Cutler and Peace, 1990, uk. 28, 29)

 

Tatu (3): katika makala yake nyingine Robert Fulghum anaongelea kuhusu kusikia sala ya Bwana akiwa kama mtoto na kudhani ilisema, “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako liwe Howard.” (Our Father who art in heaven, Howard be thy name) kwa vile Howard lilikuwa jina la upande wa mama yake, alijihisi kuwa ameunganika kwa karibu zaidi, kwamba ni sehemu ya familia, na kwa hiyo akategemea kabisa kwamba maombi yake yatajibiwa.

 

Nne (4): Na neno lililotamkwa kwa Yesu pale Yordani, “Huyu ni Mwana Wangu ninayependezwa naye,” hukumbatia wanadamu. Mungu alizungumza na Yesu kama mwakilishi wetu. Pamoja na dhambi zetu zote, na madhaifu yetu, hatujatengwa wala hatujakosa thamani. “Ametuumba na kutupokea katika upendo.” … Sauti ilizungumza na Yesu inazungumza na kila nafsi inayoamini, huyu ni mwana Wangu, Ninayependezwa naye. (The Desire of Ages/Tumaini la vizazi vyote, uk 113).

 

Tano (5): Mimi (Ron) niliwahi kumuuliza mtoto, “Una miaka mingapi?” alinipatia jibu la mara moja. Akiinua vidole vine alijibu, “Nina minne,” na kwa pumzi hiyo hiyo akauliza, “wewe una miaka mingapi?” sikuwa na vidole vya kutosha kuinua. Nilipojibu, “mimi nina hamsini,” Yule mtoto alionekana kuchanganyikiwa hivi.

 

Sita (6): kwa kipindi cha mwaka hivi au zaidi, wasichana wadogo wawili waliishi na mama yao jirani na sisi. Kwa sababu mimi (Ron) nina tabia ya kuweka mara kwa mara mlangoni vitu vya zamani nyumbani kwangu ambavyo havihitajiki pamoja na bango lililoandikwa “Bure” kwa faida ya wapita njia, wasichana hawa wawili walianza kuniita “Mzee Bure.” Nilipokuwa nikifanya kazi katika bustani yangu ya majani au ya maua, waliniangalia kwa kutaka kufahamu na kusema, “Unafanya nini Mzee Bure?” nakumbuka niliwahi kujaribu kuwaelezea mbolea. Waliniuliza, “nini hiyo” “ni chakula kwa ajili ya majani,” nikajibu. “Lakini sasa majani yanakulaje?” nikasema, “majani hula na vidole vyake vya miguu,” wakiwa wameonekana kuridhika waliondoka lakini waliondoka na kile kilichoonekana kuwa ripoti ya kufurahisha sana kwa mama yao.

 

 


Somo la Tatu

 

FAMILIA ZINAZOLEA IMANI

 

Na

 

Karen & Ron Flowers

 

Wakurugenzi, Idara ya Huduma za Familia, Konferensi kuu

 

Na

 

Idara ya Huduma za Familia NTUC & STUM

 

Mada Kuu: Maandiko hufunua umuhimu mkubwa wa familia katika kupitisha maadili ya kiroho kutoka kizazi kimoja kwenda kingine.

Fungu Kuu: Kumbukumbu la Torati 6:4-25; Mathayo 22:37-38

Dondoo za Uwasilishaji: Katika orodha ifuatayo, namba zilizo katika mabano (1), (2),

(3) zitamaanisha vitu kutoka kwenye kipengele cha mwisho kabisa kinachoitwa Mwangaza wa Somo ambacho kitatumika kwa ajili ya mifano. Unaweza kuongeza mifano yako mwenyewe ili kukuza uwasilishaji.

 

Kadiri Musa alivyokaribia mwisho wa maisha yake, alitamani kuhamisha urithi wa imani kwa Mungu ambayo ilikuwa yake kwa wale waliomfuata. Akiwa amevuviwa na Mungu, kiongozi huyu ambaye alikuwa amezeeka alitafuta kama vile wanariadha wa Olimpiki “kupitisha mwenge” kwa kizazi kipya kwa jumbe zilizoandikwa katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati.

 

Dk. John Youngberg, Profesa wa Elimu ya Kidini katika Chuo cha Andrews anaandika kwamba, “Kitabu cha Kumbukumbu la Torati … ni tamko gumu sana juu ya elimu ya kidini ambayo inaweza kupatikana katika Maandiko. Kitabu hiki kinaeleza maana ya tatizo la waalimu wa dini, maudhui yake, na dhana kadhaa ambazo zinachangia au hata kuamua mabadiliko yenye mafanikio ya urithi kutoka kizazi kimoja kwenda kingine … tatizo la Kumbukumbu la Torati ni kwa jinsi gani ‘mwanzilishi’ anayekaribia kufa anaweza kuhamisha urithi wa imani yake kwenda kwa kizazi kipya ambacho hakikushuhudia miujiza ya kutoka Misri au ukuu wa Sinai.”

 

Kile Musa alichopitia kinafanana na kile kinachowakabili wazazi wanapotafakari hitaji la kuwasadikisha watoto wao na kuwapatia urithi wa kidini. Dk. Youngberg anasema, “Maadili mengi hayaendelei kuwepo kwa sababu tu ni mema au kwa sababu ni ya kweli. Yanaendelea kuwepo kwa sababu tu yametengenezwa madhabahu katika mioyo ya vijana. Maadili yetu ya kidini tunayothamini sana siku zote yapo kizazi kimoja tu nyuma ya kupotea!” Katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati 6:4-25 kuna mashauri kutoka kwa Mungu ambayo yatatusaidia leo tunapotafakari kuhusu kulea imani katika familia zetu.

 

Kumwabudu Mungu Sana

 

Torati 6:4, 5. “Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.” Sehemu ya Kumbu kumbu la Torati 6:4-9 imekuja kufahamika kama Shema katika imani ya Kiyahudi, kutoka kwenye neno la Kiebrania la “sikia” katika fungu la 4. Shema ndio msingi na kanuni ya Msingi ya imani ya Uyahudi na inatumika katika kufungua kila huduma ya Kiyahudi. Neno lake la ufunguzi ni Andiko la kwanza ambalo kila mtoto wa Kiyahudi hulikariri. “Bwana ni Mungu wetu, Bwana ni mmoja.” Katikati ya dini zenye miungu mingi, fungu hili hutamka kwamba Mungu wetu ni mmoja. Pia hutamka kwamba ahadi yetu kwa Mungu lazima iwe kipaumbele. Ni kama vile Musa angekuwa anasema, “Weka vipaumbele vyako vizuri. Kitu kimoja ndicho cha msingi – uhusiano wako wa upendo na Mungu. Hivyo vitu vingine vinashika nafasi ya pili.”

 

Yesu pia alisema, “Utafuteni kwanza Ufalme wa Mungu na haki Yake, na hayo mengine yote mtazidishishiwa.” Mathayo 6:33. Mahali pengine tena alipigia mstari maelekezo ya Kumbukumbu la Torati 6:5, akitamka kuwa amri ya kwanza iliyo kuu, “Nawe utampenda Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa nafsi yako yote, na kwa akili yako yote. Hii ndio amri ya kwanza iliyo kuu” Math 22:37, 38.

 

Pokea Neno la Mungu Ndani yako

Torati 6:6. “Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako;” Mungu ana shauku kwamba kila mmoja wetu ahisi upendo Wake kwa namna ya binafsi na kuliweka neno la Mungu moyoni mwake. Moyo humaanisha mawazo, hisia, kiini cha mtu kulingana na maandiko ya Kiebrania yanavyohusika. Pamoja na kwamba dini ya Yehova huathiri tabia na matendo ya nje ya mtu, hujihusisha kwanza na hali ya moyo, roho ya ndani ya muumini.

 

Kiwango cha juu cha motisha katika maisha, katika mahusiano na huduma hutokea pale Neno la Mungu linapokuwa limekubaliwa, linapokuwa limethaminiwa na kuwekwa ndani ya moyo. (1) Moyo hutumika sana kwenye maneno ya wote Musa na Yesu (tz. Math 22:37, 38). Matendo ya nje, kama vile kuongea, kufundisha na tabia zingine, sio mbadala wa uzoefu wa ndani. Upendo wa Mungu kuongoza moyo ni muhimu kabla haujaanza kufundishwa kwa wengine. (2)

 

Fundisha Neno la Mungu Kwa bidii

Torati 6:7 “Nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii….”

 

Agano la kudumu. Agano la Mungu kwa watu Wake linakusudiwa kuwa la kudumu (Mwanzo 9:12; Kutoka 31:16). Halikukusudiwa kwa ajili ya kizazi kimoja tu. Kuelewa tu agano la Mungu kwa watu Wake hakulifanyi lihamishike tu lenyewe kutoka kizazi kimoja kwenda kingine. Kila mmoja katika kizazi kinachofuata lazima afundishwe maana ya agano hilo na kualikwa kuingia yeye mwenyewe katika uhusiano wa agano hilo na Mungu.

 

Umuhimu wa maelekezo ya nyumbani. Kumbukumbu la Torati huambatanisha umuhimu wa kufundisha ndani ya familia (Torati. 4:9; 6:20-25; 11:19). Nyumba inapaswa kuwa kiini cha kutunza na kueneza kweli. Musa alielewa kwamba ukuu wa taifa ulitegemea mafundisho ya Neno la Mungu nyumbani. (3)

 

Jinsi ya kufundisha kwa bidii. “Kufundisha kwa bidii” kumeelezewa katika mafungu yanayofuata:

 

Kufundisha bila kukoma. Torati 6:7. “Nawe … utayazunguzia uketipo ndani ya nyumba yako, utembeapo njiani, ulalapo na uamkapo.” Maelekezo kutoka wa wazazi yanapaswa kuwa maisha ya kila siku yenye mafundisho yaliyochanganywa na nyakati mafundisho ya mara kwa mara. “Uketipo,” “utembeapo,” “ulalapo,” na “uamkapo” huelezea shughuli za kawaida za maisha. “Mwanadamu wa kileo anaweza kujaza mizunguko ya maisha yake kwa tamaduni za ibada wakati wa chakula, kusoma Biblia mara kwa mara, maombi ya familia, na maombi binafsi.” – The Interpreter’s Bible, uk. 375.

 

  • Fundisha kivitendo. Torati 6:8, 9. “Yafunge yawe dalili juu ya mkono wako, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yako.Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako.” Maelekezo yalipaswa kufanywa kuwa halisi na ya kivitendo katika kazi, kujifunza, maburudisho, katika kuishi kifamilia na katika nyanja zote za maisha.. (4), (5)

 

Fungu hili hatimaye lilipoteza maana yake pale marabi walipolitafsiri kwa jinsi lilivyo, wakifunga vikaratasi vidogo kutoka kwenye vitabu vya Musa mikononi mwao na kwenye vipaji vya nyuso zao na kwenye miimo ya milango ya nyumba zao. (6) Ushauri huu lakini, ulifungwa katika lugha ya mfano ili kuwasilisha kanuni za msingi. Kweli za Neno la Mungu zinapaswa kuongoza matendo yetu, zikiwakilishwa na mikono, na fikra zetu, zikiwakilishwa na kipaji cha uso. Kuweka Neno la Mungu kwenye miimo ya milango yetu humaanisha kwamba kweli ya Mungu inapaswa kuwa alama yetu ya kututambulisha, kama damu kwenye miimo ya milango ya Waisraeli kule Misri ilivyokuwa alama ya utambulisho ili kwamba familia iliyopo humo ndani iweze kuokolewa (Tazama Kutoka 12:7, 13). (7)

 

  • Fundisha kwa hekima. Torati. 6:20 “Na zamani zijazo atakapokuuliza mwanao … ndipo umwambie mwanao….” Hapa Mungu anawasilisha dhana mbili zenye nguvu katika mafundisho ya maadili yenye matokeo. Mzazi mwenye hekima hutambua thamani ya maswali ya watoto na kisa cha binafsi.

 

Ni asili ya watoto kuwa na maswali. Hebu na tuunge mkono hii roho ya kuuliza maswali na kwa namna hiyo kuwasaidia kutengeneza imani yao wenyewe. Maswali yao yanaweza yakawa magumu, lakini usiogope kujaribu kuyajibu. Kuogopa maswali na kukatisha tamaa kuuliza kunaweza kukadumaza ukuaji wa imani ya mtoto. Ni lazima tujibu maswali kadiri yanavyojitokeza, tukitoa majibu yanayohitajika na yanayofaa kwa ajili ya maendeleo ya hali ya mtoto. Kila mara tunapojibu kwa ukweli, kwa uaminifu na kwa uwazi, tunasaidia kujenga imani na kuandaa njia ili kwamba vijana watiwe moyo kuuliza maswali yenye maana zaidi. (8)

 

Katika kujibu maswali ya watoto, Mungu anawaagiza wazazi kujibu kwa visa vya jinsi alivyokuwa hai katika maisha yao wenyewe. Visa hufundisha na kuvutia kuiga pamoja na kuburudisha. Kujiweka wazi kwa watoto kuhusiana na safari ya kiroho kumekuwa na mvuto mkuu kwenye akili na mioyo ya watoto. (9)

 

Ishi Neno la Mungu kwa Uaminifu

Torati 6:12, 14, 18. “Ndipo ujitunze, usije ukamsahau …. Msifuate miungu mingine …

Nawe fanya yaliyo sawa, na mema, machoni pa Bwana.”

 

Uaminifu. Neno la Mungu linatambua kwamba wale ambao ni wenye shida, hawahitaji msukumo mkubwa ili kumgeukia Mungu na kumtumikia. Lakini kinachohitajika ni watu ambao katikati ya wingi na malimbuko mengi wataendelea kuwa waaminifu kwake, wale ambao hawatavutwa na miungu mingine, wala kuiendea miungu ya watu wanaowazunguka.


Kuwa mfano usiobadilika. Watoto huiga maadili yaliyo sehemu ya maisha ya wale wanaowaona. Kubadilika badilika huleta kuchanganyikiwa na mashaka. (10)

 

Ujasiri wa kutokuwa mkamilifu. Maisha ya Mkristo mwaminifu ambaye ni mzazi hayamaanishi kutokuwa na doa kabisa. Mungu anaatuhitaji kuwa wazazi wakamilifu, lakini katika hali yetu ya kuvunjika, pamoja na kwamba hatujakamilika, tuwaongoze watoto wetu kwa Mwokozi mkamilifu ambaye tumempata na kuiongoza miguu yao katika njia ya kumpata wao wenyewe.

 

Hitimisho

Kusudi letu kuu ni kuandaa njia kwa ajili ya watoto wetu ili waweke agano na Mungu wao kama sisi tulivyoweka agano letu naye. Hatuwezi kulazimisha, lakini tunaweza kwa upendo na uvumilivu kuwaelekeza. Tunaweza tukaishi kwa uaminifu mbele yao na kuwaalika kama Musa alivyofanya aliposema, “basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako;” Torati. 30:19. Hebu sisi na watoto wetu baada yetu na tujibu kama Yoshua, “Ila mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Bwana” Yosh. 24:15.

 

Mwangaza wa Hubiri

 

Moja (1): Michakato inayoathiri badiliko la mtazamo. Herbet Kelman aliwahi kuelezea michakato mitatu ambayo inaathiri badiliko la mtazamo: kuafikiana, utambulisho, na kutia moyoni (Kelman, 1958). Kuafikiana hutokea pale mtu anapokuwa anaongozwa na mwingine. Mtoto anaafikiana na kanuni za mzazi kwa sababu mzazi analazimisha tabia kwa adhabu, au kumnyima vipaumbele. Katika mchakato wa utambulisho, shauku ya uhusiano na mtu mwingine au kikundi hupelekea kuchukua maadili yake. Kupenda kuwa na mtu au kuwa sehemu ya kikundi hupelekea kukubali maadili yao kama ya kwake. Kwenye kutia moyoni, maadili yanayoendana na tabia huchukuliwa kuwa na maana kwa ajili yake mwenyewe. Kutia moyoni maadili ya Mungu ndio kusudi lililodhihirishwa katika Kumbukumbu la torati 6:6.

 

Mbili (2): Upendo ndani ya moyo huleta badiliko katika maisha. Aleida Huissen mwenye miaka sabini na nane wa Rotterdam huko Netherlands alikuwa akivuta sigara kwa miaka hamsini. Kwa sehemu kubwa ya muda huo amekuwa akijaribu bila mafanikio kuacha tabia hiyo. Kisha kitu fulani kikatokea na akafanikiwa kuiacha. Siri ilikua ni nini? Alikutana na Leo Jansen mwenye miaka sabini na tisa. Wawili hawa walipendana na Leo akatangaza ndoa. “Nitapenda uwe nami kwa muda mrefu,” alisema. “ni lazima uache kuvuta sigara kabla haijakuua.” Aleida akasema, “Nia haijawahi kutosha kunifanya niache tabia hii. Upendo ulinifanya niache.” – imetolewa kwa John C Maxwell, The Communicator’s Commentary , uk. 127.


Tatu (3): Umuhimu wa nyumbani kama kiini cha kufundishia maadili. Ustawi wa jamii, mafanikio ya kanisa, mafanikio ya taifa yanategemea mivuto ya nyumbani. – Ellen G. White, The Ministry of Healing, uk. 349.Urejeshwaji na kuinua ubinadamu kiroho huanzia nyumbani. Kazi ya wazazi hutangulia zingine zote. Jamii imeundwa na familia, nayo inatokana na vichwa vya familia ambavyo kwa pamoja vinaiunda. – Ellen G. White,  The Ministry of Healing, uk. 349.

 

Nne (4): Mkate usio na chumvi. Allen na Mark walipenda kujiunga na mama alipokuwa akitengeneza mkate. Siku moja chumvi ilisahaulika na mkate ukakosa ladha. Mama akatumia nafasi hii kuzungumza na watoto hawa kuhusu kile Yesu alichosema kuhusu Wakristo kuwa chumvi ya dunia, ili kuufanya ulimwengu kuwa mahali bora zaidi kwa upendo wao. “Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? …” (Mat 5:13)

 

Mkate ulitengenezwa vizuri ukawa na sura nzuri, lakini haukuwa na ladha, kama vile kuna kitu Fulani cha muhimu kinakosekana. Mama akasema, “Watu wengi unapowatazama wanaonekana kuendelea na maisha yao sawa sawa tu bila Yesu, lakini bila Yesu kuna kitu Fulani cha muhimu siku zote kitakuwa kinapungua katika maisha ya wanadamu.” Walijaribu kuupaka mkate siagi na kisha kunyunyiza chumvi, lakini hiyo haikufanya kazi vyema pia. Mama akaongezea, “Wakristo ambao hawafanyi urafiki na majirani zao na kujichanganya na wale wanaowazunguka ambao hawamfahamu Yesu hawaleti ladha pia katika ulimwengu. Yesu anatuhitaji tujichanganye na kushirikisha wengine upendo Wake katika mizunguko yote tunayoishi.”

 

Tano (5): Somo kutoka kwenye magugu. Miaka michache iliyopita mimi na kijana wangu tulikuwa tukifanya kazi kwenye bustani. Dickie akauliza akiwa amechanganyikiwa, “Baba, Mungu aliumba magugu?” nilianza kutoa jibu la haraka ili niendelee na kazi yangu, lakini nikagundua hii ilikua ni fursa ya kufundisha somo la kiroho.

 

Nikaweka chini kijembe changu cha kung’olea magugu na nikasema, “Dickie, unafahamu kuhusu Adamu na Hawa. Walikuwa ndio watu wa kwanza kuishi katika dunia. Mungu aliwaweka kwenye bustani nzuri isiyokuwa na magugu yoyote. Basi siku moja shetani akaja, akiwa anafanana na nyoka. Akamwambia Adamu na Hawa kutomtii Mungu; akawaambia kwamba wale baadhi ya matunda ambayo Mungu alikuwa amewakataza wasile. Na unajua nini kilitokea? Walikula. Kisha dunia ikaanza kupata matatizo. Baada ya Adamu na Hawa kutomtii Mungu, magugu yakaanza kuota na ikawabidi waondoke kwenda kufanya kazi na kuiacha bustani yao nzuri.”

Akiwa na uso mzito Dickie akajibu, “Hiyo si inasikitisha sana!”

Ninahusisha tukio hili ili kuonyesha umuhimu wa kanuni ya biblia:

Masomo yanayojitokeza katika uzoefu halisi wa maisha mara nyingi huwa na matokeo zaidi kuliko kujifunza kwa namna iliyo rasmi.

 

Maelekezo haya kutoka kwenye maisha halisi ndio kinachozungumziwa katika Kumbukumbu la Torati 6. Waisraeli walipaswa kuunganisha mafunzo ya mtoto katika kitani ya maisha yao ya kila siku. Katika utamaduni wetu tuna tabia kubwa ya kutenganisha vilivyo vitakatifu na vya kawaida. Tunahakikisha kwamba watoto wetu wanapata elimu (shuleni), mafunzo (nyumbani), na maelekezo ya kiroho (kanisani, katika ibada ya familia, na kwa nyakati Fulani shuleni).

 

Lakini kugawa gawa huku kunasababisha matatizo. Moja ya sababu inayofanya watoto na vijana wengi kutoka kwenye nyumba za Kikristo kuona maana ndogo sana katika uzoefu wao wa Kikristo ni kwa sababu imani yao ya Kikristo haikuwahi kuingizwa katika maisha yao ya kila siku. Wazazi wao walishindwa kupitia uzoetu au kudhihirisha furaha yao katika ubunifu mkuu wa Mungu katika uumbaji. Walishindwa kuona na kuelezea biashara zao na masuala ya familia kwa mtazamo wa Mungu-watoto Wake wakimiliki milki katika ulimwengu kwa ajili ya utukufu wa Muumba wao. Kama matokeo yake, watoto wao walishindwa kuona kwamba Mungu huvutiwa sana na kuhusika katika kila eneo la maisha. – Bruve Narramore, Parenting with Love and Limits, uk. 61.

 

Sita (6): Wayahudi waliweka sheria kwenye “mikono,” “vipaji vya nyuso” na kwenye “miimo ya milango”. Wakitafsiri jinsi yalivyo maneno ya fungu la 8, utamaduni wa Wanaume wa Kiyahudi wa zamani ilikuwa kunakili sehemu nne kutoka kwenye sheria (Kutoka 12:1-10; 13:11-16; Torati 6:4-9; 11:13-21) na kuweka mafungu haya katika vishikizo vya ngozi na kuvifunga kwenye mikono yao ya kushoto na katika vipaji vya nyuso zao wakati wa maombi ya asubuhi. Pia waliweka Torati 6:4-5 na 11:13-20 kwenye kiboksi cha chuma au kioo na kufunga kwenye upande wa kuume wa miimo ya milango ya kila nyumba. – John C. Maxwell, The Communicator’s Commentary, uk. 128.

 

Saba (7): Kweli ya Mungu hutambulisha nyumba zetu. Katika barabara ya Foxly, karibu na chuo cha Newbold, nyumba za hapo, kama zilivyo nyumba nyingi kote Uingereza, hutambulishwa kwa majina badala ya namba za mtaa. Bwana na Bibi Mchungaji Ernest Marter, mchungaji mstaafu wa kanisa la Waadventista Wasabato na mke wake, walijenga nyumba yao katika mtaa huu. Waliyaita makazi haya “Shukrani” na kuweka bango la kuvutia lenye jina hilo pembezoni mwa njia ya kuingilia. Inafananaje na ishara zilizopo katika kitabu cha Kumbukumbu la torati! Kama vile Waisraeli walivyoonywa kuandika maneno ya Bwana “kwenye miimo ya milango yao na kwenye malango yao,” ndivyo nyumba ya Shukrani ilivyowatangazia wote walioingia na kupita kwa shukrani na upendo kwa Yesu anayetawala mioyo ya wale wanaoishi ndani yake.

 

Nane (8): “Sijui” haijibu swali. Siku moja mvulana mdogo alikuwa akitembea na baba yake. Walipolipita gari lililokuwa na sura isiyo ya kawaida, Yule mvulana akauliza, “Baba, ile ni nini?”

“Sijui,” baba akasema..

Kisha wakafika kwenye ghala la kizamani, “Kuna nini pale Baba?” mvulana huyu akauliza.

“Sijui,” baba akajibu.

Kisha wakaona mtu akiwa na chombo cha kuchimbia chini akichimba njiani.

Mvulana akauliza, “Yule mtu anafanya nini baba?”

“Sijui,” lilikuwa jibu la baba tena.

Baada ya kutembea kidogo wakiwa kimya, mvulana huyu akamgeukia baba yake na kusema, “Baba, haupendi nikikuuliza maswali mengi?”

Baba akajibu, “Hapana, kwani utajifunzaje sasa jambo lolote?” –John C. Maxwell, The Communicator’s Commentary, uk. 134.

 

Tisa (9): Nguvu ya visa. Sababu nyingine kila mtu anapenda visa ni kwamba kuelezea jambo ndio njia rahisi zaidi ya kufikiria. Haichukui jitihada kubwa sana kiakili kufuatilia kisa, na bado katika kupitia kisa mtu anaweza akajifunza kwa kiwango kikubwa kweli kwa namna imara zaidi … Watoto hawawezi kufikiri sana kama watu wazima wanavyopaswa kufikiri, wala hawawezi kushika mawazo magumu kama watu wazima wanavyotegemewa kushika; kwa hiyo visa ndio njia ya asili ya kuwafundisha kweli. Kisa sahihi, kikiingizwa katika uelewa wao, ni kifurushi kidogo cha kweli kwa namna ambayo akili yao inaweza kumeza. – Arthur Spalding na Eric B. Hare, Christian Storytelling. Uk. 14.


Kumi (10): Watoto hujifunza kile wanachokiishi

Kama mtoto ataishi na ukosoaji, Atajifunza kuhukumu.

Kama mtoto ataishi na ukatili, Atajifunza kupigana.

Kama mtoto ataishi na udhalilishaji, Atajifunza kuwa na aibu.

Kama mtoto ataishi na aibu, Atajifunza kuwa na hatia.

Kama mtoto ataishi na uvumilivu, Atajifunza kuwa mvumilivu.

Kama mtoto ataishi na kutiwa moyo, Atajifunza kuwa na ujasiri.

Kama mtoto ataishi na sifa, Atajifunza kushukuru.

Kama mtoto ataishi na usawa, Atajifunza haki.

Kama mtoto ataishi na usalama, Atajifunza kuwa na imani.

Kama mtoto ataishi na ukubali, Atajifunza kujipenda.

Kama mtoto ataishi na ukubali na urafiki, Atajifunza kutafuta upendo duniani. -Dorothy Law Nolte

 


Somo la Nne

 

KUWASAIDIA VIJANA WETU KUKAMATA INJILI

 

Na

 

Elaine & Willie Oliver

 

Idara ya Huduma za Familia, Divisheni ya Amerika Kaskazini

 

Na

 

Idara ya Huduma za Familia NTUC & STUM

 

Mada Kuu: kwa vile mara nyingi maadili hushikwa badala ya kufundishwa, sisi kama wazazi na walezi tuna fursa ya pekee kuwasaidia watoto na vijana kuishika injili kwa kutoa mandhari ya upendo, uwazi na neema na kuwaruhusu vijana wetu kushuhudia tabia yetu sisi wenyewe, pamoja na makosa yetu na maombi yetu ya msamaha.

 

Fungu Kuu: Kumbukumbu la Torati 6:6-9

 

Dondoo za Uwasilishaji: katika orodha hii, namba kwenye mabano (1), (2), (3) hutumika kuashiria vitu kutoka kwenye kipengele cha Mwangaza wa Hubiri ambavyo vinawez kutumika kwa ajili ya mifano. Nyongeza ya mifano yako binafsi itakuza uwasilishaji.

 

Katika Kumbukumbu la Torati 6:6-9, Mungu anatoa mwongozo kwa wazazi ili kuwasaidia kuvutia imani kwa watoto wao na shauku ya kumjua na kumtumikia. Mamlaka yake kwa mama na baba inajumuisha: kuwa na sheria zake mioyoni mwao, kushirikishana na watoto wao hizo amri zake, na kuwa mfano wa amri zake katika maisha yao nyakati zote.

 

Kuwa na Amri za Mungu Moyoni mwako

 

Wazazi hawawezi kuhamishia kwa watoto wao kile ambacho wao wenyewe hawana. Imani na ahadi kwa Mungu lazima vifanye makao ndani ya mioyo yao kwanza. haiwezekani amri zake ziwe ndani yetu kwa jinsi alivyokusudia Mungu bila kuzitafakari kwa muktadha wa habari njema ya injili. Kuikubali injili ya Yesu ni kigezo cha kwanza cha kuwa na amri za Mungu katika moyo wa mtu.

 

Kukubali neema ya Mungu kwa imani. “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu;” (Waefeso 2:8). Neema na imani vinaonyeshwa hapa kuwa vitu viwili vya muhimu


katika kiini cha injili ya Yesu Kristo. Neema ni upendeleo usiostahili, wema usiostahili. Wokovu unakuwa wetu pale tunapokubali neema ya Mungu kwa imani. Imani ni kupumzika katika Mungu, kuweka imani yote ya mtu kwake. Maisha ya mzazi ambaye kila mara humtegemea Mungu kwa ajili ya kila kitu anachofanya humdhihirishia mtoto maana ya imani (Wagalatia 3:26; Yohana 3:16; Marko 16:15, 16; Waebrania 11:6; Yohana 1:16).

 

Kukubali nguvu ya Mungu katika maisha yako. “Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye…” (Warumi 1:16). Pale mtu anapokubali wokovu ambao Mungu ameupatia ulimwengu katika Kristo – ambayo ni zawadi yake ya neema - anapata uzoefu wa nguvu kuu ya Mungu ya kuokoa katika Kristo. Akili zetu na mioyo yetu inabadilishwa kadiri anapoandika sheria zake ndani yetu. Amri zake huishi ndani ya mioyo kupitia kwa nguvu iliyopokelewa wakati wokovu ulipokubaliwa. Kweli hizi ni kwa ajili yetu kama wazazi ili tuzipitie na kisha tushirikishe na uzao wetu (Yohana 1:12; 2 Wakorinto 12:9; Tito 2:11, 12; Waebrania 8:10; 13:9; Warumi 5:20, 21; 12:2).

 

Kushiriki amri za Mungu na watoto wako

Kama Mungu alivyowaagiza wazazi Waisraeli kuweka mvuto ndani ya watoto wao kuhusu njia za Bwana, ndivyo anavyotuagiza leo. Kushirikishana huku ni kitu anachofahamu kwamba kinawezekana kwa namna maalum kwa wazazi na kinapaswa kupatiwa kipaumbele cha juu.

 

Wajibu wa wazazi katika kujichanganya kwa watoto. Wazazi hutawala maisha ya kijamii ya watoto. Familia ndio uwanja mkuu wa kujumuika. Ili kuwa na uhakika, kuna mawakala wengine (wachungaji, marafiki, waalimu, vyombo vya habari) na sehemu zingine ambazo mjumuiko hutokea (makanisa, viwanja vya michezo, shule, sehemu za burudani), lakini wazazi katika familia bado ndio waalimu wa kwanza na wa muhimu wa maadili katika maisha ya watoto wao. (1) Maandiko yanaelezea aina hii ya kuhusika kwa wazazi (Waefeso 6:4) na E. G. White anaunga mkono (2)

 

Kile tafiti zinachotuambia kuhusu kuhamisha maadili kutoka kwa mzazi kwenda kwa watoto. Valuegenesis, ambao ni mradi mkubwa wa utafiti ulioendeshwa na Kanisa la Waadventista wa Sabato miaka kadhaa iliyopita, hudhihirisha wazi kwamba familia ndipo mahali pa kwanza ambapo imani na maadili ya watoto hupaliliwa. Katika utafiti huu, vitu vitano vya muhimu kuhusu familia ambavyo hugusa makuzi ya imani kwa watoto na vijana vinaoneshwa kuwa ni:

  • Mama. Mama huwa huru mara kwa mara kuwashirikisha watoto imani yake.
  • Baba. Baba huwa huru mara kwa mara kuwashirikisha watoto imani yake.
  • Msaada. Wazazi huwasiliana na watoto mara kwa mara kwa namna iliyo chanya yenye kutoa msaada.
  • Mamlaka. Wazazi wana viwango vya juu, wanaweka vikomo vya muda, na kuvisimamia kwa upendo.
  • Umoja wa kiroho. Familia mara kwa mara huhusika katika ibada ya pamoja yenye maana na ya kuvutia na kujihusisha katika miradi ya huduma ya kuwafaidia wengine. (3)

 

Ili kuleta injili kwa vijana nyumbani, basi, wazazi wanahitaji kuwa na imani iliyo hai ambayo wataiwasilisha kwa watoto wao katika mikutano ya kila siku huku wakiwa wanaendesha magari barabarani, wakiwa wanafanya kazi bustanini, wakiwa ndani ya treni, wakiwa wanasoma pamoja, wakiwa wanacheza pamoja na wakifanya ibada pamoja. Watoto na vijana lazima wahisi kuwa wako huru kwenda katika daraja lenye kingo, vijana wataelewa mipaka ambayo imewekwa kwa upole na imara kama ulinzi na mawasiliano ya upendo na kujali kwa wazazi wao.

 

Mabadiliko ya ukuaji wa kiroho kwa vijana. Kulingana na Valuegenesis, kuna vitu vya msingi vine vinavyohitajika kwa vijana ili kukua katika utu uzima wa kiroho:

  • Mtazamo wa neema kuhusu wokovu. Wazazi wanahitaji kushiriki na vijana wao dhana ya kibiblia ya wokovu kama zawadi ya Mungu mwenye upendo kwa viumbe wasiostahili. Sio tabia njema inayotuokoa. Hakuna jambo lolote tunaloweza kufanya ili kustahili wokovu. Kile tunachoweza kufanya ni kukubali zawadi inayokuja na nguvu ya ushindi. Zawadi hii huja na shauku kubwa ya kuwasiliana na Mtoaji, uhusiano wa binafsi na Yesu. Ni uhusiano huo ndio huleta uelewa na kuongoza tabia zetu, sio tabia zetu zinazotufanya tupendelewe na Mungu (Waefeso 2:8; Yohana 1:12; Yohana 3:16).
  • Furaha katika kumwabudu Mungu kupitia nyanja zote za maisha. Vijana wanahitaji kuelewa kwamba hakuna kugawanyika sehemu mbili katika maisha ya Mkristo. Katika kila shughuli mtu anatakiwa kurudisha utukufu kwa Mungu. Iwe ni darasani, au katika uwanja wa michezo, iwe ni nyumbani au kanisani, iwe ni kazini au katika maburudisho, vijana wanapaswa kutiwa moyo kutengeneza ufahamu wa uwepo wa Mungu katika maisha yao na kutafuta furaha katika uelewa wa uwepo wake (1 Wakorinto 10:31).
  • Hali ya hewa ya ukubali, uwazi na ustawi. Injili ya Yesu Kristo huvuta zaidi maisha ya vijana pale wanapokuwa katika mazingira ya kutiwa moyo na kuungwa mkono kadiri wanavyokua kuelekea utu uzima wa kiroho. (4) Badala ya kuwakatisha tamaa au kuwakosoa vijana wao, wazazi watafanya vyema kuwa na uvumilivu na ukarimu na kudhihirisha upendo ili kutengeneza mandhari chanya ambayo itawezesha kukua kiroho ndipo vijana watakapoweza kupokea Injili. (5)
  • Fursa za kuwahudumia wengine katika utume. Hakuna kinachojenga misuli, iwe ni ile ya kimwili ya au kiroho kama mazoezi. Imani ambayo ni ya kinadharia tu muda si mrefu itakuwa imani dhaifu isiyojitosheleza. Kuwapatia vijana fursa ya kuwahudumia wengine kutasaidia kujenga hisia za thamani- “Ninaweza nikaleta tofauti katika maisha ya wenginee.” Hisia hizi hutafsiriwa katika mfumo wa maisha, ambao ni wa kutoa huduma kwa Mungu na kwa jirani. Huduma ni daraja la kutoka kwenye imani ya kinadharia kwenda kwenye imani iliyo hai.

 

Kuwa Mfano wa Amri za Mungu Katika Maisha Yako

 

Kuna msemo maarufu unaosema: “Fanya kama ninavyosema, lakini usifanye kama ninavyofanya.” Tangazo la televisheni kuhusu matumizi ya madawa huonyesha baba na mwanaye wakiwa katika chumba cha kijana. Baba anamshika kijana wake akivuta bangi na anagomba kwa hasira, “Umejifunza wapi kufanya hivyo?” kijana anajibu kwa hasira, “Kwa kukutazama wewe.” Baba anaghafilika kwa sababu hajihusishi na madawa ya kulevya. Lakini kijana amekuwa akimuona na madawa mengine ambayo pia yana madhara.

 

Kwa vile maadili yanashikwa badala ya kufundishwa, hakuna shaka kuhusu sababu kubwa ya watoto wetu hufanana nasi. Kama wazazi hukaripiana na hawana uvumilivu, watoto mara nyingi hukaripiana na pia hawana uvumilivu. Tumekuwa tukishangazwa kwa jinsi watoto wetu wanavyotenda kama sisi - jambo ambalo kila mara hatujawa tayari kulikubali. Kwa kweli, ni rahisi kuelekeza tabia hasi ya watoto wetu kuwa inatoka upande wa familia ya mwenzi wetu. Tunaita hali hii kukataa na kujitetea. Mara nyingi, kinyume chake huwa kwa kweli tunaelekeza mambo yale yaliyo chanya na mazuri yanayojitokeza kwa watoto wetu kwamba yanatoka kwa malezi mazuri ya familia yetu. (6)

 

Kuna shaka kidogo kuhusu kwa nini Mungu alimvuvia nabii kuandika katika Kumbukumbu la torati kuhusu jinsi tunavyopaswa kushiriki injili na watoto wetu. “…yatie muhuri kwa watoto wenu. Uyanene uketipo nyumbani na utembeapo njiani, ulalapo na uamkapo. Yafunge kama ishara katika mikono yako na yafunge katika kipaji cha uso wako.” Ili kuwa na uhakika, wengi wetu tuna shauku juu ya watoto wetu wanaokua katika nyumba zetu lakini hawamkubali Yesu Kristo na kubatizwa. Uamuzi kama huu haujitokezi tu kutoa katika utupu. “Kwa kutazama tunabadilishwa.” Ni zaidi tu ya kumwambia mtoto wako kwamba anapaswa kubatizwa. Jinsi tunavyoishi kila siku, tunashuhudia kwao kwa namna iliyo chanya au hasi. Maombi yetu ya dhati kanisani yanaweza yasiwe na matokeo endapo kuna ukali, kukosa uvumilivu na kukosa upendo nyumbani.

 

Kuwasilisha injili kwa watoto wetu tunaweza tukaiita kuwa ni biashara ya “masaa 24 – siku 7 za juma”- juhudi tunazofanya siku nzima, kila siku, bila kujali tunafanya nini; kuhusiana nyumbani au nje ya nyumbani, asubuhi na mapema au usiku wa manane, kwa taratibu za kila siku za maisha yetu nyumbani na vipaumbele tunavyopatia mambo ya kiroho, kwa ukarimu wetu, kujali kwetu, upendo wetu, tunamshuhudia Yesu na neema Yake iokoayo. Hata tunapofanya makosa (na ni kweli tutafanya), kujifunza jinsi ya kuombana msamaha sisi kwa sisi na watoto wetu kutashirikisha uhalisia wa msamaha wa Mungu na utayari wake wa kutupatia fursa mpya na uwezo wa kuishi maisha ya ushindi kwa ajili yake.

 

Hitimisho

Mwandishi wa Kumbukumbu la torati anaweka wazi maelekezo kutoka kwa Mungu. Lazima tuwe na uzoefu binafsi na uhusiano na Bwana wetu kwa kukubali neema yake na kutiwa nguvu kuishi kwa ajili yake. Lazima tuwe na maamuzi kuhusu kushirikisha watoto wetu maadili yetu ya kiroho katika mandhari ya ukubali, uwazi, na upendo. Na pia tunapaswa kuwa macho kuhusiana na dhana kwamba tunawashuhudia watoto wetu hata pale ambapo hatutambui kwamba tunafanya hivyo. Kwa hiyo mara nyingi kile tunachofanya ni muhimu zaidi ya kile tunachosema.

 

Kwa uwezo wetu sisi wenyewe biashara hii haiwezekani, lakini “kwa Mungu kila jambo linawezekana.” Kama hatujawa na mafanikio katika biashara hii ya kuwasilisha habari njema ya injili kwa watoto wetu kuliko tulivyotegemea, tunaweza kwa ujasiri kuwainua kwenye maombi mbele ya Baba yetu wa mbinguni mwenye neema anayetufahamu sisi na wao. Tunapomgeukia, tunaweza tukapokea msamaha kwa ajili ya mapungufu yetu. Tunaweza kupata uelewa wa ndani zaidi katika habari njema ya injili, tukagundua njia zenye matokeo bora zaidi katika kutumia mvuto wetu, na kupokea uwezo wa kuendelea katika mahusiano na watoto wetu na kwa matumaini kujenga upya mahusiano yaliyoharibika. Kilicho bora zaidi ya yote ni kwamba tunaweza tukapata uhakika mpya kuwa, kwa kutenda kwa Mungu kupitia Kristo Ameshughulikia wokovu wetu na wokovu wa watoto wetu. Tunaweza tukamwamini katika hilo. Tukiwa na tumaini jipya tunaweza tukaendelea kufanya kazi nzuri ya kufundisha, kupitia katika kuishi hilo na neno, mwaliko wa kukubali zawadi yake ya neema.


Mwangaza wa Hubiri

 

Moja (1): watoto kuishi pamoja imekuwa ikielezewa labda kuwa kazi moja ya kiulimwengu ya familia. Kwa maelfu ya miaka familia imekuwa ikihodhi maisha ya kijamii ya mtoto. Kabla ya uchumi wa viwanda, watoto wadogo walitumia muda wao mwingi wakiwa na wazazi wao, ndugu zao, babu na bibi, mashangazi, wajomba, na binamu zao. Baada ya uchumi wa viwanda kuja, malezi ya watoto yamekuwa ni kazi ya msingi ya familia ndogo ya baba, mama na ndugu waliozaliwa pamoja. Miongo kadhaa iliyopita, muda ule uliokuwa wa familia umepatia nafasi muda wa kuwa na marafiki katika vituo vya kulelea watoto, na walezi, na mashuleni. Lakini pamoja na mabadiliko haya, wazazi na familia wamebaki kuwa mawakala wa msingi na eneo kitovu penye nafasi ya kujumuika. (Gelles, 1995, uk.290)

 

Mbili (2): Baba na mama wanapaswa kuwa waalimu wa kwanza kwa watoto wao … mafunzo ya watoto huchukua sehemu ya muhimu katika mpango wa Mungu wa kudhihirisha nguvu ya Ukristo. Wazazi wana wajibu mkuu wa kuwafundisha watoto wao kwamba wanapoenda ulimwenguni, wanapaswa kutenda mema kwa wale watakaohusiana nao na sio mabaya. (Child Guidance, uk. 21)

 

Tatu (3): tunafahamu kwamba familia ndiyo maabara muhimu ambapo imani na maadili ya watoto wetu hujengwa. Vifuatavyo ni vitu vitano ambavyo vimekuwa muhimu kulingana na utafiti kuhusu imani, maadili na maagano:

 

Mama. Mama anapokuwa mshika dini sana, ni rahisi kwake kuzungumzia imani yake, na kuwashirikisha watoto wake mara kwa mara, na kuwa na majadiliano kuhusu imani na vijana, vijana wanakuwa na nafasi nzuri zaidi ya kukua kiimani na kutengeneza agano kwa mtazamo wa kidini.

 

Baba. Baba anapokuwa mshika dini sana, ni rahisi kwake kuzungumzia imani yake mwenyewe, na kuwashirikisha watoto wake imani yake, na kuwa na majadiliano ya mara kwa mara nao, wanakuwa na nafasi nzuri ya kudhihirisha imani inayokua na hisia za uaminifu kwa dhehebu lao.

 

Msaada. Mawasiliano ya mzazi na mtoto yanapokuwa ya mara kwa mara na yaliyo chanya, pale maisha ya familia yanapokuwa ya upendo, kujali, na kusaidiana, na pale wazazi wanapowasaidia watoto wao kazi za shuleni mara kwa mara, vijana wanakuwa na nafasi nzuri ya kuwa na imani inayokua, inayojitosheleza na hisia za uaminifu kwa dhehebu lao.

 

Mamlaka. Wazazi wanaposhikilia viwango imara, na kuvisimamia kwa usawa, kwa uimara, na kwa upendo, kuadhibu tabia mbaya, na kuweka vikomo katika jinsi mtoto anavyotumia muda, vijana wanakua katika imani na kudhihirisha agano na uaminifu kwa kanisa lao. Pamoja na kwamba dhana ya mamlaka ina mguso mdogo ukilinganisha na makundi hayo matano, mamlaka inaonekana kuwa chanya kwa mazingira ya nyumbani pamoja na kwamba sio kwa ajili ya shule za dini na mikusanyiko yake. Pale nidhamu inapotolewa na wale watu tunaofahamu kwamba wanatupenda, hupokelewa kwa utayari.

 

Umoja wa kiroho. Pale familia inapojihusisha katika ibada ya pamoja, na kwamba ibada inakuwa ya kuvutia na yenye maana, pale familia inapojihusisha katika miradi ya kusaidia watu wengine, watoto na vijana wanakuwa na nafasi nzuri ya kudhihirisha imani iliyokua, inayojitosheleza na uaminifu kwa dhehebu lao (Tyner, 1996, uk.5)

 

Nne (4): Usiwatendee watoto wako kwa ukali tu, ukisahau utoto wako na kusahau kwamba wao ni watoto tu. Usitegemee watakuwa wakamilifu au kujaribu kuwafanya kuwa wanaume au wanawake katika matendo yao mara moja (The Adventist Home, uk.196)

 

Tano (5): Moyo wa mtoto ni mlaini na huvutwa kirahisi; na pale sisi tulio watu wazima tunapokuwa “kama watoto wadogo” tunapojifunza urahisi na upole na ulaini wa upendo wa Mwokozi, hatutaona kuwa ni vigumu kugusa mioyo ya wale walio wadogo na kuwafundisha upendo wa huduma ya uponyaji (The Adventist Home, uk. 195)

 

Sita (6): Jessica na Julian, ni watoto wetu walizaliwa katika mji wa New York ambapo waliishi kwa kipindi kirefu. Kama umeishi na kuendesha gari katika mji wa New York, au kama umewahi kutembelea Manhattan na umekuwa na bahati (!!) ya kuendesha katika msongamano ule wa magari unaweza ukaelewa kile ninachozungumza; utajenga ukosefu wa uvumilivu katika msongamano huo. Unaanza kuongea na madereva wengine chini chini. Wakati mwingine sio chini chini, bali unapaza sauti kabisa, “Twendeni basi!” au “endesha basi!” hii ni misemo ya kawaida inayotumika pale taa ya barabarani inapokaribia kuwa kijani na gari la mbele yako halijaanza kusogea.

 

Tulikuwa hatujaona ni kiasi gani tumeshakuwa sehemu ya utamaduni huo wa kuendesha hadi siku moja, tulipokuwa tukijaribu kupita katika barabara nyakati ambazo watu wanawahi kazini katika mji na tukajikuta hatufanyi maendeleo yoyote, tulisikia Jessica aliyekuwa na miaka mitatu akisema kutoka nyuma kwenye kiti chake, “Vipi huko, Twende zetu!” tulishtuka! Na tukaangaliana kwa lile jicho la kukubali kwamba, “tunakuwa mfano hata pale ambapo hatutambui.”

 

Katika tukio lingine, baada ya miezi 18 ya kuwa na ibada ya familia baada ya Jessica kuzaliwa, tulikuwa tukifanya utani kuhusu maisha yake ya mbeleni na kujiuliza wenyewe endapo siku moja angeamua kuwa Mkristo wa kanisa la Waadventista wa Sabato. Tulipokuwa tukipiga magoti kufunga kipindi cha ibada, binti yetu alianza kuomba. Maneno yake hayakuweza kueleweka vizuri, lakini mioyo yetu ilienda mbio kwa furaha na tulikuwa tumejawa na hisia tulipotambua kwamba mfano wetu chanya ulikuwa umeanza kuonyesha matokeo.

 

 


Somo la Tano

 

NYUMBA NI KWA AJILI YA KUSHIRIKIANA

 

Na

 

Karen & Ron Flowers

 

Wakurugenzi, Idara ya Huduma za Familia, Konferensi Kuu

 

Na

 

Idara ya Huduma za Familia, NTUC & STUM

 

Mada kuu: Nyumba ya kweli ya Kikristo ina imani na uzoefu wa kushirikisha wengine ambao unaweza ukawasaidia na kuwabariki.

 

Fungu Kuu: Isaya 39:4

 

Dondoo za Uwasilishaji: Katika orodha ifuatayo, namba zilizo katika mabano (1), (2),

(3) zitamaanisha vitu kutoka kwenye kipengele kinachoitwa Mwangaza wa Somo ambacho kitatumika kwa ajili ya mifano. Nyongeza ya mifano yako mwenyewe itakuza uwasilishaji. Katika kitabu cha Isaya 39 kuna kisa cha ugeni wa wajumbe kutoka Babeli kwenda Yerusalemu. Akiwa na furaha ya kuwaburudisha, Mfalme Hezekia aliwapitisha katika mji wake mkuu. Hazina yake, ghala zake za dhahabu na fedha, majumba yake ya makumbusho na ghala za kutunzia kumbukumbu za thamani, nyaraka na maeneo vilipotunzwa vitu walivyobuni. Waliona ghala lake lote la silaha. Kumbukumbu zinaonyesha kwamba kwa ujumla aliwaonyesha vile vitu vilivyodhihirisha mamlaka yake kama mfalme. Hakuna mahali palipotajwa kuwa aliwaonyesha hekalu au kuwaelezea huduma zake. Baada ya kuondoka kwao, nabii Isaya alimjia mfalme akiwa na swali la kuweza kushtua kutoka usingizini, “Wameona nini nyumbani mwako?” (Isaya 39:4).

 

Hezekia hakupoteza nafasi ya kuonyesha mitego ya mamlaka yake. Wageni wake walitazama na kisha kurudi nyumbani, lakini bila kugundua hazina yake ya kiroho. Mtunzi wa Zaburi anasema kwamba ufunuo wa Mungu kwa wanadamu ni Neno Lake kutamaniwa kuliko dhahabu (zab. 19:10), lakini Hezekia hakuweka msistizo kwa vitu ambavyo vingefungua macho na mioyo ya mabalozi wale waliokuwa na maswali juu ya Mungu wa kweli. Isaya anaelezea huu kuwa ufunuo wa muhimu zaidi pale alipomuuliza mfalme, “wameona nini katika nyumba yako?”


Mawakili wa Nyumba ya Bwana

Wakristo wanatambua kwamba kila walicho nacho ni cha Mungu. Ametuweka kuwa mawakili na wasimamizi Wake juu ya kile alichotukabidhi. Kama vile muda wetu, talanta zetu, hazina na hekalu la mwili, nyumba zetu ni za Bwana lakini ametukabidhi. Sisi ni mawakili wa nyumba zetu ambazo kwa uhalisia, ni nyumba za Bwana. Mungu anataka nyumba zetu ziwe vituo vya ushuhudiaji. Tunahitaji kujiuliza swali leo, “Wameona nini nyumbani mwako?”

 

Kiongozi mmoja wa uwakili aliyefahamika sana alizoea kuzungumza kuhusu “kusikiliza sauti ya Mungu katika mapato yetu,” maana yake ni kusikiliza uongozi wa kutoka kwa Mungu kuhusu jinsi tunavyopaswa kutumia kile kilicho chake. Kwa namna iyo hiyo tunaweza tukaweka nyumba zetu mbele yake, na kwa maombi kusikiliza uongozi Wake katika kila kilichopo hapo, rasilimali za upendo na kujali, pamoja na vitu vya kimwili, vinaweza kutumika katika utume kwa ajili ya Mungu. (1), (2)

 

Tunapaswa Kushirikishana Nini?

Kabla wale wajumbe kutoka Babeli hawajaja, Hezekia alikuwa amepitia muujiza wa kuponywa kutoka kwenye ugonjwa mbaya sana. Badiliko hili katika afya yake liliambatana na ushahidi usio wa kibinadamu wa mibaraka ya Mungu katika tukio lisilo la kawaida ambapo, jua lilirudi nyuma madaraja kumi. (Angalia Isaya 38:4-8.) Mfalme alipewa nafasi ya ajabu ya kushirikisha kweli ya thamani kuhusu Yehova ambayo yeye na taifa lake walikabidhiwa.

 

Taarifa kuhusu Mponyaji. Somo tunalopata kutoka kwenye maisha ya Hezekia ni kwamba Wakristo wameitwa, sio kuonyesha mibaraka ya mafanikio ya vitu na mambo mbalimbali, pamoja na kwamba tunaweza kutambua mibaraka hii kuwa imetoka kwa Mungu. Kwa mara ya kwanza tunapaswa kushirikisha, na kuruhusu miingiliano yetu na wengine kutoa ufahamu kwamba tuna mahitaji yanayofanana na wanadamu wote. Tulikuwa tunaumwa, ndio, tukiwa tunakaribia kufa. Lakini kuna Mmoja ambaye ametuponya na anaendelea kutuponya. Tulikuwa tumepotea kiroho, lakini kuna Mmoja ambaye aliangalia hali yetu, akatuhurumia, na kutuokoa.

 

Kutumia nyumba zetu kwa ajili ya utume kunaweza kukatofautiana kuanziakwa kitu rahisi kama vile kumkaribisha maji ya kunywa mtoto wa jirani anayecheza na watoto wetu, kuwaalika washiriki wa kanisani au wageni kwa ajili ya chakula cha pamoja, hadi kufikia ukarimu wa kumpatia chumba mhanga wa unyanyasaji au mraibu asiye na makazi wakati ambapo anapitia mchakato wa urejeshwaji. Inaweza kumaanisha kuendesha darasa la kujifunza Biblia na majirani hapo nyumbani kwetu, au kutoa muda kwa ajili ya ushauri na maombi ya faragha na mtu Fulani. Wana furaha wale wanaopata nafasi ya kufungua Neno la Mungu na mtu mwingine na kushiriki kwa undani imani yao. Pamoja na kwamba kushirikisha kwetu kunaweza kusiwe kwa namna ya kuiweka wazi na kwa undani imani yetu, kushirikiana nyumba zetu lazima kujengwe kwenye jiwe la msingi la mafundisho ya Biblia kuhusu injili. Wakati ambapo injili inaweza ikaendeshwa na makusudi mbalimbali, mwishowe kutoa tu kwa injili peke yake hufanya huduma kuwa furaha kuu.

 

Injili. Msingi wa kile Wakristo wanachopaswa kushirikiana na wenye dhambi ni habari njema ya neema ya Mungu iliyodhihirishwa katika maisha, kifo, na ufufuo wa Yesu. Mbali na kila kitu tunachoweza kufanya, Mungu alitupenda bila masharti na akatenda kwa niaba yetu. Kristo alijitambulisha Mwenyewe pamoja nasi (Mathayo 1:23). Mungu anatazama jamii yote ya wanadamu kama imekuwa “katika Kristo,” ikishiriki katika historia yake, maisha yake, kifo chake na ufufuo Wake (1 Wakorinto 1:30; Ebr. 2:9; Warumi 5:14-19). Kwa sababu ya Yesu, Mungu anawahesabia haki wasio wacha Mungu (Warumi 4:5) na hazikumbuki tena dhambi zetu kuwa ni kitu. (2 Wakorinto 5:19) Tulikuwa tumekufa katika dhambi zetu, lakini kwake yeye, Mungu anatuchukulia kama tumefufuliwa kiroho, tumeinuliwa na kuketi katika mahali pa mbinguni (Waefeso 2:1). Wito wa Mungu ni kwa wenye dhambi kumwamini Yesu, kukubali kafara yake kwa ajili yetu, na kutembea kulingana na wito ambao tumeitiwa. (Waefeso 4:1), kumruhusu Mungu atende kazi ndani yetu kunia na kutenda yaliyo mapenzi Yake (Wafilipi 2:13)

 

Tunda la injili. Uhakika wa injili unapatikana katika kuwa “ndani ya Kristo,” uhalisia wa Kiroho uliokamilishwa na Mungu ambao muumini anaukamata kwa imani. Pamoja na hili, Mungu anataka kutenda kazi katika maisha ya muumini ambaye Agano Jipya linamzungumzia kama “Kristo ndani yako” (Wakolosai 1:27), Roho kukaa ndani yake (Warumi 8:9), au Kristo kukaa ndani ya moyo kwa imani (Waefeso 3:17). Matokeo ya mtindo wa maisha ya Mkristo sio injili moja kwa moja, lakini ni tunda la injili. Kuja mara ya pili kwa Yesu sio injili moja kwa moja lakini ni tumaini la injili.

 

Ukarimu halisi wa Kikristo, upendo, kujali na kutiana joto unaodhihirishwa katika nyumba ya Kikristo, hutoka kwenye miyo ya watu ambao wameguswa na wameponywa na injili. Kutoka kwenye nyumba zetu kutakuwa na mashahidi wa mtindo wa maisha na kutakuwa na kushirikishana na wengi kweli zote za Biblia ambazo ni muhimu. Lakini tofauti lazima iwekwe wazi kati ya kile hasa kinalichopo kwenye habari njema, na ni ushauri upi ambao ni mwema au ni taarifa ipi iliyo njema.


Tushirikiane na Nani Rasilimali za Nyumbani Kwetu?

 

Eneo la karibu la utume. “Kama watendakazi wa Mungu, kazi yetu ni kuanza na wale walio karibu. Ni kuanzia nyumbani kwetu wenyewe. Hakuna eneo la utume lililo muhimu kuliko hili.” – Child Guidance, uk. 476, “Kazi yetu kwa ajili ya Kristo ni kuanza na familia nyumbani … kwa wengi eneo hili la nyumbani limekuwa likitelekezwa kwa aibu, na ni wakati ambao rasilimali za kimbingu na uponyaji wake uwasilishwe, ili kwamba hali hii ya uovu iweze kurekebishwa.” – Testimonies for the Church, toleo la 6, uk. 429, 430. “Unaweza kuwa mwinjilisti nyumbani, na mchungaji wa neema kwa watoto wako.” – Child Guidance, uk. 479.

 

Faida ya kwanza ya kuzifanyia kazi rasilimali za nyumba zetu za Kikristo ni kwa ajili ya wokovu wa familia zetu wenyewe. Mungu alikusudia familia ziwe ni sehemu ya asili au ya kawaida ya kufuata maelekezo ya Yesu, Enendeni mkawafanye kuwa wanafunzi (Mathayo 28:19). Katika mzunguko wa familia inayojali mahitaji ya ndani ya mmojawapo wa familia kujihisi kuwa sehemu yake, kwa upendo, kwa ukaribu na mawasiliano ya kijamii vyote kushughulikiwa. Kwa vile ni katika familia ndipo mtu huanza kujifunza kuhusu mahusiano, familia ya Kikristo huwa na uwezo wa ajabu wa kufundisha kuhusu Mungu wa upendo na kuwashirikisha kwa upendo wengine (Yohana 13:35). Kwa neema ya Mungu familia inaweza kuwa wakala mwenye nguvu kwa ajili ya kunidhamisha washiriki wake kwa ajili ya Kristo. (3) katika haraka yetu ya kuwashughulikia wengine, hatupaswi kuzembea washiriki wa nyumba zetu wenyewe.(4)

 

Kufika nje ya nyumba zetu. “Utume wa nyumbani hupanuka na kwenda zaidi ya washiriki wake tu. Nyumba ya Kikristo inapaswa kuwa somo, ikitoa mfano wa ubora wa kanuni za kweli za maisha. Mfano kama huo utakuwa nguvu ya wema kwa ulimwengu. Mvuto wa nyumba ya kweli kwa mioyo na maisha ya mwanadamu una nguvu kuliko hubiri lolote ambalo linaweza kuhubiriwa.”-The Ministry of Healing, uk, 352.

 

Watu walio katikaa nyumba zinazotuzunguka wanahitaji kile ambacho sisi kama Wakristo Waadventista kwa upendeleo tumejaliwa kuwa nacho katika familia zetu. Dunia ina njaa ya upendo. Njaa ya mifano ya jinsi upendo wa kweli unavyoweza kuzaliwa katika moyo na kujaza maisha ya familia, nyumba zinateseka. Wengine talaka, wengine wanatengana, wengine wanashikilia kwa nguvu kadiri wanavyoweza, mara nyingi wakipambana ndani ya mapaa yao au wakivumilia maumivu na kukata tamaa. Wale kati yetu ambao tunaona njia ya kuishi kwa mafanikio maisha ya Kikristo nyumbani tuna kitu cha kuwashirikisha wengine ili waone na kufahamu.


Vituo vya ushuhudiaji vilivyo hai. Dhana muhimu ya kufanya familia zetu kuwa vituo vya kimishonari ni kuruhusu wengine watazame mahusiano yetu katika ndoa na maisha ya familia, kushiriki kwa namna Fulani katika uzoefu wa maisha yetu. Wengi hawana mifano ya kufuata ya familia bora. Wanahitaji tu kuona jinsi nyumba zetu na mahusiano yetu yanavyofanya kazi na jinsi Roho wa Yesu anavyoleta tofauti.

 

Kwa ajili ya wote, wazee na vijana, walio kwenye ndoa na wasio kwenye ndoa, kuna wingi wa mahitaji ya kibinadamu katika mitaa yetu ambayo inaweza kufaidika na upendo ambao Kristo analeta katika nyumba zetu na ujumbe maalum aliotukabidhi tushirikishe wengine. Utume unapaswa kuwa mtindo wetu wa maisha. Ni lazima tutafute njia za kujenga madaraja ya mahusiano kwa wengine. (5)

 

“Nenda kwa jirani zako mmoja baada ya mwingine, na nenda karibu nao hadi mioyo yao itiwe joto kwa mvuto na upendo wako usio na ubinafsi. Waonee huruma, omba nao, tafuta fursa ya kuwatendea wema, na kadiri uwezavyo, kusanya wachache pamoja na fungua Neno la Mungu katika mawazo yao yaliyotiwa giza.” – Welfare Ministry, uk 64.

 

Vifungo vya urafiki huanzia kwenye matendo ya ukarimu na kujali ambayo tunaonyesha, kuanzia kwenye zawadi tunazotoa, vyakula tunayoshirikisha wengine, muda tunaotumia na wengine katika mazungumzo katika daraja linaloshughulikia hisia zetu na zao za ndani. Nyumba yetu hutupatia nafasi zisizohesabika za kutengeneza mahusiano kama hayo na kushiriki na wengine Ukristo wetu wa Kiadventista. Ni lazima tuvunje vikwazo vinavyotutenga na familia zinazotuzunguka.(6)

 

Hitimisho

“Eneo letu la mvuto linaweza kuonekana kuwa dogo, uwezo wetu kuwa mdogo, fursa zetu kuwa chache, mafanikio yetu kidogo; lakini uwezekano wa ajabu ni wetu kupitia matumizi ya fursa za nyumba zetu kwa uaminifu. Endapo tutafungua mioyo yetu na nyumba zetu kwa ajili ya kanuni za kimbingu kwa ajili ya maisha tutakuwa mifereji ya kupitishia nguvu ya uhai. Mifereji ya uponyaji, inayoleta uhai na uzuri na kuzaa matunda itaririka kutoka katika nyumba zetu ambapo sasa kuna ukame na uhaba.” – The Ministry of Healing, uk 355.

 

Mwangaza wa Hubiri

 

Moja (1): Tofauti kati ya kuburudisha na ukarimu. “Kuburudisha husema, ‘ninataka kukuvutia kwa nyumba yangu nzuri, urembo nilioweka kwa ustadi, mapishi yangu ya umahiri.’ Ukarimu, kwa upande mwingine, hutafuta kuhudumu, husema, ‘Hii nyumba sio yangu. Kweli ni zawadi kutoka kwa Bwana wangu, mimi ni mtumishi Wake na ninaitumia kama Apendavyo.’ Ukarimu haujaribu kuvutia, ila kuhudumia.” -Karen Burton Mains, Fungua Moyo, Fungua Nyumba, uk 25.

 

Mbili (2): Nyumbani: Nyenzo kwa ajili ya utume. Kila mmoja wetu anaweza kushiriki kwa namna Fulani katika uinjilisti kupitia ukarimu, kwa matumizi ya nyumba kama nyenzo kwa ajili ya utume. Wazo kuu kuhusu nyumba ni kwamba ni ya kiulimwengu kwa kila Mkristo. Wote tunaishi mahali fulani, katika chumba au bweni au nyumba ya kupanga au jumba la fahari. Katika dunia hii isiyo na ukarimu nyumba ya Mkristo ni muujiza unaopaswa kushirikishwa. –Ibid, uk. 137.

 

Tatu (3): Eneo la karibu la utume. Utafiti wa hivi karibuni wa Dk. Janet Kangas kwa zaidi ya vijana 1500 Waadventista wa Sabato katika Marekani ya Kaskazini unaonyesha kwamba “nyumbani ndipo mahali penye mvuto wa muhimu wa kidini.” –Janet Leigh Kangas, A study of the Religious Attitudes and Behaviours of Seventh-day Adventist Adolescents in North America Related to their Family, Educational and Church Backgrouds, (Utafiti wa mitazamo na tabia za kidini za vijana Wasabato wanaopevuka katika Marekani ya Kaskazini kwa historia zao za kifamilia, kielimu na kanisani.) Utafiti wa Udaktari ambao haukuchapishwa, Chuo cha Andrews, 1988, Sehemu ya utangulizi.

 

Nne (4): Mama, kwanini wewe sio mwema hivi kwetu? “Ukarimu, kama ilivyo msaada huanzia nyumbani, “ Mains, uk. 77. “Waume, wenzi, watoto, au kwa namna isiyo ya kawaida, marafiki zao, mara nyingi hupokea sehemu ndogo ya usikivu wetu. Dhana hii ililetwa kwa nguvu nyumbani kwangu na binti yangu, ambaye alisema kwa akili sana mbele ya sebule iliyojaa wageni, ‘Mama, mbona hauwi mwema namna hii kwetu wakati watu hawapo hapa?’ “ –Ibid.

 

Tano (5): Lazima tujihusishe na maisha ya watu wengine. “Ninaamini kwamba kanisa, linapofanya kazi vyema, linaweza likaleta uponyaji kwa wale wanaolijia. Ndani ya kanisa kuna muundo muhimu, mpangokazi wa kifalsafa, na mamlaka ya kushughulika na watu na matatizo yao. Nguvu ipo katika utu wa Roho Mtakatifu. Lakini washiriki wa kanisa wanapaswa kuwa tayari kuacha kujitenga kwao na kufuatia starehe ya mali ili kuweza kujihusisha na maisha ya wengine. Hii ndio njia pekee ya kutoka kwenye upweke na kuingia katika jamii. “ –Brenda Hunter, Beyond Divorce, uk. 56.

 

Sita (6): Kushuhudia kupitia katika ukarimu. Mchungaji Samuel Monnier, Kiongozi mstaafu wa shughuli za kilei katika Konferensi Kuu aliyefahamika kwa semina zake za Maranatha na Wainjilisti Walei, anaeleza uzoefu ufuatao wa maisha ya familia na ukarimu:


“Nyumbani kwetu baada ya ibada ya familia Jumapili asubuhi tunakuwa na baraza la familia na kwa wakati ule mara nyingi tulichagua mtu wa kumualika nyumbani kwetu kwa ajili ya chakula. Mimi na mke wangu Yvonne tulipigia kura chaguzi za watoto wetu. Kisha tuliomba kwamba mtu huyo angekubali mwaliko wetu. Anapokubali, tuliomba kila siku kwamba kila mmoja wa familia yetu angekuwa na mtazamo chanya na kwamba mgeni wetu angeguswa na Roho Mtakatifu. Kabla tu ya kufika kwake tuliomba tena kwa ajili yake.

 

Tukiwa mezani nilitangaza kwamba tulikuwa Wakristo na tulifurahia kuomba mbaraka wa Mungu. Yvonne alichagua mmoja kati ya watoto kwa ajili ya kuomba. Maombi kama haya kutoka kwa watoto yaligusa mioyo ya wageni. Kwa makusudi kabisa hatukuzungumza kuhusu Mungu, kanisa au dini katika meza yetu ya mazungumzo, pamoja na kwamba nilieleza kwamba tulikuwa tumefanya maamuzi binafsi ya kutokutumia pombe wala nyama. Kabla wageni wetu hawajaondoka nyumbani kawaida niliwashirikisha ushuhuda wangu kwa dakika kama mbili jinsi nilivyokuwa Mkristo na maana ya imani katika maisha yangu. Niliwashirikisha ahadi ya Biblia na kutoa ombi. Katika ombi hilo nilikumbuka vitu tulivyozungumza, nikimueleza Baba yetu wa mbinguni kujali kwetu na shauku yetu kwa ajili ya mambo mbalimbali ambayo yalikuwa yametamkwa na mgeni wetu na sisi.

 

Mara nyingi wageni wetu walifanya hivyo kwa kutualika na sisi katika nyumba zao. Tulijibu kwamba tutajitahidi kujenga uhusiano, tukibaki wazi katika mada zinazohusiana na kanisa au Mungu. Nilikuwa na Biblia ndogo pamoja nami kila mara na kabla ya kuondoka katika nyumba zao, niliwauliza, “Ninaweza nikasoma ahadi ya Biblia; ninaweza kuomba?” kwa njia hii rahisi ya kiutendaji familia yetu ilishuhudia. Pale watu walipokuwa tayari kwa ajili ya kujifunza zaidi, tulitafuta njia za kuwahusisha katika matukio kanisani, katika kongamano, filamu, na baadae katika mikutano ya uinjilisti. Katika matukio yote haya tulikuwa pamoja nao. Kwa namna hii tulitengeneza marafiki wengi na kuona wengi wakianza kuelekea katika barabara ya ushirika wa kanisa.”

 
Somo la Sita

 

JINSI YA KUMPENDA MWANA WA NGURUMO

 

Na

 

Karen & Ron Flowers

 

Wakurugenzi, Idara ya Huduma za Familia, Konferensi Kuu

 

Na

 

Idara ya Huduma za Familia, NTUC & STUM

 

Mada Kuu: Kwa msaada wa Mungu tunaweza kuendelea kupendana sisi kwa sisi katika familia zetu hata tunapopitia vipindi vigumu pamoja katika maisha yetu.

 

Fungu Kuu: 1 Yohana 4:7-11

 

Dondoo za Uwasilishaji: Katika orodha ifuatayo, namba zilizo katika mabano (1),

 

(2), (3) zitamaanisha vitu kutoka kwenye kipengele kinachoitwa Mwangaza wa Somo ambacho kitatumika kwa ajili ya mifano. Nyongeza ya mifano yako mwenyewe itakuza uwasilishaji.

 

Vizazi kadhaa vilivyopita, ilikuwa ni kawaida kwa wauzaji wa Biblia kwenda nyumba kwa nyumba Marekani kote pamoja na Kanada wakiuza Biblia kubwa za familia. Tunakumbuka kuwaona katika nyumba za babu na bibi zetu wakiwa na vitabu vikubwa vizito vyenye majalada ya ngozi na maandishi makubwa yenye herufi zilizoandikwa kisanii. Kulikua na kurasa za kuandikia tarehe za kuzaliwa, vifo, harusi na matukio mengine ya kifamilia. Nyingi kati ya hizo zilikuwa na sehemu za kuandika majina ya ukoo, “mti wa familia” yako. Ziligeuka na kuwa mahali pa kutunzia picha na kadi na barua kutoka kwa wanafamilia.

 

Mara nyingi, katikati ya Biblia hizi kubwa kulikuwa na machapisho ya picha nzuri. Picha moja ambayo ilijumuishwa sana ilikuwa ni picha ya Yesu na wanafunzi wake, wakiwa wameketi katika meza wakisherehekea Pasaka ya Mwisho. Ilikuwa inafurahisha kuona kwamba Yesu na kundi lote walikuwa wameketi upande mmoja wa meza. Kiukweli, familia katika Nchi Takatifu wakati wa Yesu hawakutumia hata meza za namna ile. Achana na hilo, ilikuwa ni sura ya Yesu na suya za mitume ndizo zilizoteka usikivu. Karibu na Yesu alikuwapo yule mtume mdogo kuliko wote, akiwa kama mvulana tu, akiwa na uso wa kitoto wenye aibu. Alikuwa ni Yohana, mwana wa Zebedayo. Picha ilionyesha akimwegemea Yesu, shavu lake kifuani mwa Yesu.

 


1.   Mwana wa Ngurumo

 

Kwa picha hii inayoitwa, “Pasaka ya Mwisho” msanii huyu Leonardo Da Vinci ameifanya dhana kwamba mtume Yohana alikuwa mtu wa aina ya upole, anayependwa kuwa maarufu. Lakini picha inayoonyeshwa kwenye Injili ni tofauti kabisa. Yohana alikuwa mkali, asiye na adabu, kijana mwenye damu inayochemka. Roho yake isiyofundishika ikiambatana hasira kali vilimpatia jina “Mwana wa Ngurumo” au “Mtu wa ngurumo” (Marko 3:17). Mwenye hasira kali na za karibu, kwa asili hakuwa mnyenyekevu na mwenye kujisalimisha. Alitamani mamlaka na madaraka, na alifanya mbinu ya kuwa mkuu kwa mitume kwa ujanja. Katika tukio mojawapo, yeye na kaka yake walijaribu kumshawishi Yesu ili awapatie nafasi za juu katika Ufalme Wake kwa kumtumia mama yao kupeleka ombi lao (Mathayo 20:21). Hii iliwakasirisha sana wanafunzi wengine na walibwabwaja wenyewe kwa wenyewe hadi Yesu alipoingilia kati.

 

Yohana alikuwa na roho ya kukosoa. Alikua na chuki za kidini na kikabila pia ambazo hazikuwa na sababu, na alilionea wivu kundi lake mwenyewe. Hakutaka kuona mtu mwingine akigusa kile alichochukulia kuwa ni uwanja binafsi wa Yesu na wanafunzi (Luka 9:49). Alikuwa ni Yohana aliyepata hasira, kuudhika na kuwa tayari kupigana Wasamaria walipokosa ukarimu kwa Bwana wake. Kwa kulipiza kisasi, alitaka waharibiwe kwa moto (Luka 9:54, 55). E. G. White katika Desire of Ages, uk. 295, alimtambulisha kama mwenye kuudhika haraka, mkosoaji, mwenye majivuno, mwenye roho ya vurugu, mgomvi na mwenye gubu.

 

2.   Upendo unaotazama ndani

 

Mara kadhaa, Yohana hujiita “mwanafunzi aliyependwa na Yesu” (Yohana 13:23; 19:26; 21:7, 20). Kwa nje mafungu haya yanaonyesha kwamba Yohana alikuwa “anapendeka” na Yesu alimpenda ghafla tu. Picha ya Da Vinci imesaidia kukuza dhana kwamba Yesu alimpenda kwa sababu alikuwa mpole na mkarimu, na mwema. Lakini, Yesu alimpenda Yohana pamoja na kwamba kinyume chake, vigezo hivi ndivyo vilivyotawala maisha yake.

 

Kinyume cha neno “kupenda” au “kuvutiwa na” kwa kiyunani Philos, yaani neno ambalo linatumika kuelezea upendo wa Yesu kwa Lazaro (Yohana 11:36), Yohana yeye alitumia neno la tofauti kuelezea mtazamo wa Yesu kwake. Ni neno linalotumika kote katika Agano Jipya kwa ajili ya Upendo wa Mungu unaookoa (agape). Injili ya Yohana huonyesha upendo huu ukitenda kazi mara kadhaa; Paulo anatoa makala ya Kikristo kuhusu vigezo vya upendo huu (1 Wakorinto 13). (1) Yesu anawaamuru wafuasi Wake kupenda kwa namna hii (Yohana 15:12), lakini huu ni upendo wa msingi, usiofahamika katika moyo wa mwanadamu (Yohana 5:42) isipokuwa tu Roho wa Mungu ameumimina ndani yetu (Rumi 5:5).

 

Injili ya Yohana iliandikwa baadaye sana katika maisha yake. Ilikuwa ni wakati wa kutafakari ujana wake na mwendelezo wa upendo wa Mungu kwake hata katikati ya kutokupendeka kwake. Muundo wa neno “kupendwa” katika mafungu haya katika lugha halisi ulikuwa na maana ya “kuendelea kupenda.” Maajabu ya maajabu,, Yesu aliendelea kumpenda pamoja na tabia alizokua nazo.

 

Mtazamo wa Bwana. Mafungu mawili hutupatia mtazamo wa upendo wa Yesu kwa mwafunzi huyu kijana na aliye mgumu. “… Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7). “Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima…” (Mathayo 12:20).

 

Kutazama kwenye moyo. Fungu la kwanza huonyesha jinsi Mungu anavyojali maisha na hali ya ndani ya mtu. Ni kama vile Yesu alimtazama Yohana kwa kutumia miwani maalum. (2) Yohana na wale walio kama yeye, kwa mwonekano wa nje huwasilisha tabia na mitazamo ambayo ni migumu kuishi nayo, na hata ya kuudhi. Vitu hivi vinavyomfanya mtu huyu, iwe ni mtoto, kijana au mtu mzima kuwa mgumu kupendeka kweli hutupatia taarifa muhimu kuhusu jinsi mtu huyo anavyojihisi kwa ndani. Yesu alielezea muunganiko wa karibu kati ya hali ya nje na ya ndani ya mtu mahali pengine aliposema, “kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.” (Mathayo 12:34).

 

Mianzi iliyopondeka. Maelezo ya Injili yanayofafanua “mwanzi uliopondeka” au utambi ufukao moshi” yanarandana kabisa na Yohana. Maelezo haya yanatoka kwa Mathayo, anayemtambulisha Yesu kama yeye aliyetimiza unabii wa Masihi wa Agano la Kale unaopatikana katika Isaya 42:1-4. Yesu ni mpole, mwenye huruma, mvumilivu, mwenye kustahimili. Hauvunji mwanzi uliokunjwa na upepo; badala yake anaunyoosha, anaufunga, ili kwamba uweze kustahimili upepo tena. Utambi unaofuka moshi, ukikaribia kuzimika, hauzimi bali anaufufua, na kuupuliza utoe nuru kubwa. Yesu alifahamu kwamba watu wote wanateseka na urithi wa dhambi unaowaacha wakiwa wamevunjika ndani. Aliwatazama watu kama Yohana kama hasa waliojeruhiwa ndani.

 

Hatuwezi kufahamu kilichosababisha kupondeka (kwa mwanzi) au kuelewa kikamilifu. Tunafahamu kwamba majanga ya maisha kwa watu wengi huacha alama zisizofutika. Wengi hutumia maisha yao kupona na kujaribu kuchukuliana na hali. Tunafahamu kwamba Mungu alikusudia wakina baba na wakina mama wawapatie watoto wao malezi ya kimwili, kihisia, kiakili na kiroho. Wanahitaji kuguswa, kushikwa, kukumbatiwa, kubembelezwa kwa sauti yenye kujali ya uelewa, waoneshwe matendo ya upendo, kulindwa, usalama, na hisia ya kuwa sehemu ya kitu. Katika maana halisi, aina hii ya kujali kunapokosekana au kuwa kidogo katika maisha ya utoto, watu hukabiliana na maisha ya kuchukuliana na mapungu Fulani. Pale ukali uliopitiliza, hasira, kukosekana kwa ukarimu, matendo ya unyanyasaji, au majanga mengine ya kimwili, kiakili au kihisia yanapokuwa yameongezewa katika ukosefu wa malezi ya msingi, madhara zaidi hutokea. Hali zote hizi mwishowe hupata nafasi ya kujidhihirisha katika utu na tabia ya mtu huyu. Wazazi na watu wengine wanaowalea watoto wanapaswa kuwa macho kwa mahitaji yanayoongezeka ya vijana nyakati zote za majanga katika maisha yao. (3)

 

Kwa bahati mbaya, tabia ya mwanadamu kuwa vile ilivyo, watu ambao ni wagumu kupendwa mara nyingi huwafanya wengine kutoa vigezo visivyopendeka pia. Ni kawaida kuitikia kwa ukimya, kugombeza, kubishana, kutishia, kuwapuuza, au kwa namna fulani kuwaadhibu. Lakini sio Yesu. Wakati sisi tunatazama tu mwonekano wa nje, Yeye anatazama kile kinachohitajika ndani.

 

Jinsi Yesu Alivyompenda Mwanafunzi Mgumu

 

Yesu alijipanga kumpatia Yohana kile moyo wake ulichotamani zaidi, yaani upendo uokoao. Ni upendo tu ndio wenye huruma kwa uvunjifu ambao watu hujihisi kwa ndani, upendo unaokubali, upendo unaotolewa kama zawadi. Upendo wa aina hii hujidhihirisha kwa njia fulani mahususi:

 

Upendo wa agape huamini. Yesu alimvuta Yohana karibu Yake, akimleta katika mzunguko wa ndani wa wanafunzi aliowaamini zaidi. Angalia kumbukumbu zinazo jirudia rudia zinaonyesha Yohana akiwa katika kikundi kidogo cha wateule akiwa na Petro na Yakobo (Mathayo 17:1; Marko 5:37; 14:33; Luka 8:51). Bwana wetu mwenyewe alishirikiana na Yohana, akimpatia dhana na mafunuo maalum, kama yale kwenye Mlima wa Kubadilika (Mathayo 17:2). Kuamini kuna nafasi kubwa ya kuvuta kuamiwa.

 

Upendo wa agape ni dhaifu. Yesu alifungua hisia zake za ndani kwa Yohana na wanafunzi wengine. Wengine walipokuwa wakimtenga, aliuliza, “Ninyi nanyi mwataka kuondoka?” (Yohana 6:67) pale Gethsemane, Mwokozi alijifanya kuwa dhaifu mbele ya Yohana na wengine, akitafuta msaada na kuungwa mkono kutoka kwao (Mathayo 26:37, 38). Tupo tayari kukabiliana na vikwazo vyetu sisi wenyewe mbele ya macho ya mtu aliye mwaminifu kwa uwazi na aliye dhaifu kama sisi.

 

Upendo wa agape hujenga vifungo vya urafiki wa karibu. Yesu alitafuta urafiki na Yohana pamoja na wanafunzi wengine, badala ya kuchukua nafasi ya bwana na watumishi wake (Yohana 15:13, 15). Aliwachukulia kama familia (Mathayo 12:49)). Aliwasiliana nao kwa uhuru. “Kila nilichojifunza kutoka kwa Baba yangu nimewafunulia” (Yohana 15:15). Alitenga muda wa kuwa nao faragha (Marko 3:7; 6:31; Yohana 6:3; 11:54). Sehemu inaaandika upendo wa familia na ukaribu ambao Yesu baadye alikuwa nao na Yohana (angalia Yohana 20:2, ambapo neno “upendo” humaanisha “Yule ambaye Yesu alimpenda”). (4, 5)

 

Upendo wa agape hutoa wajibu. Alipokuwa Ametundikwa msalabani, Yesu alimpatia Yohana wajibu mkuubwa – kumtunza mama yake mwenyewe (Yohana 19:26, 27). Huu haukuwa wajibu wa kwanza Yesu aliompatia Yohana (angalia Marko 6:7; Luka 8:51), lakini ulikuwa wajibu uliokuwa wazi na muhimu zaidi na ulioonyesha kina cha imani na ukaribu Aliokuwa nao na Yohana.

 

Upendo wa agape husahihisha kwa upole na uimara. Upendo wa Yesu kwa Yohana ulimfanya amkemee na kumrekebisha pale njia yake ilipopinda kutoka kwenye maadili na hukumu za Yesu (Mathayo 20:22-24; Luka 9:52-56). Baada ya kumkemea, Yesu alitumia fursa hii kuweka sawa kanuni za maisha katika familia Yake. (6, 7)

 

Upendo wa agape hutoa kafara. Pale msalabani, akiwa na mama yake Kristo, Yohana alimtazama Aliyekua anasulubiwa na kuona udhihirisho mkuu wa upendo, Yesu, ambaye alikuwa ni mwili halisi wa upendo, akifa pale. Anakumbuka, “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13). Mtu mwenye upendo wa vizazi vyote alikuwa amekuwa mbadala wake, Mwana kondoo wa Mungu aichukuae dhambi ya ulimwengu, upatanisho kwa ajili ya dhambi zake. Akiwa na macho ya kuona kweli ambayo ni Roho tu ndiye anawezesha kuona, anatambua pale msalabani, hasira yake ya karibu inakufa, roho yake ya kisasi inaondolewa, kuudhika kwake kunafikia kikomo cha milele. Asili yake ya kinyama inasulubiwa pale. Yohana anasulubiwa na Kristo (linganisha Wagalatia 2:20). Mwana wa Mungu amefanywa kuwa dhambi kwa ajili ya Yohana (2 Wakorinto 5:21) aliyefanywa kuwa Mwana wa Ngurumo, asiyevutia asiyependeka—kwamba kwake Yeye, Yohana na sisi sote, tumefanywa kuwa wenye haki, tumefanywa kuwa wa kuvutia na kupendeka. Mwana wa Ngurumo akiwa karibu na msalaba, anatambua kwamba sasa yeye ni mwana wa Mungu, na anaanguka katika magoti yake kwa ibada mbele ya msalaba. Na baadae aliandika, “Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo.” (1 Yohana 3:1). Kutoka kwenye msalaba ule panatiririka upendo uokoao unaobadili maisha ambao hutimiza mahitaji ya ndani ya nafsi yake.

 

Kristo alidhihirisha upendo wake kwa Yohana kwa njia nyingi. Njia hizi ziligusa na kubadili moyo wake. “Kina na hamasa ya upendo wa Yohana kwa Bwana wake havikuwa sababu ya upendo wa Kristo kwake, bali ni matokeo ya upendo huo. Yohana alikuwa na shauku ya kuwa kama Yesu, chini ya mvuto ubadilishao wa upendo wa Kristo alikuja kuwa mpole na mnyenyekevu. Nafsi ilifichwa ndani ya Yesu” (The Acts of Apostles, uk 544).

 

Hitimisho

Changamoto tunazokutana nazo tunapolea watoto wetu zinaweza kuwa kubwa sana. Kutakuwa na nyakati ambazo tutashangazwa, tutakatishwa tamaa, tutakasirishwa, labda kushtushwa, kwa mwenendo wao au wetu sisi tunapokuwa na mwingiliano nao katika majanga mbalimbali katika safari nzima. Lakini kuna nguvu ya kubadili mioyo na maisha. (8) nukuu hizi mbili zinaweza zikatugusa:

 

“Unaweza kuwa mwinjilisti nyumbani, mchungaji wa neema kwa watoto wako” (Child Guidancce, uk. 479). Katika changamoto yoyote, janga lolote, tunaitwa kuhudumu kwa neema kwa watoto wetu kwa wakati huo. Nukuu ya pili inazungumza matokeo ya kudhihirisha upendo wa Kristo uokoao kwa vijana wadogo:

 

“Kadiri wanavyokosa mvuto wa kupendeka, ndivyo inavyohitaji kuumia zaidi katika kudhihirisha upendo wako kwao. Pale mtoto anapojenga imani kwamba unataka kumfurahisha, ndipo upendo unapovunja kila kikwazo. Hii ni kanuni ya Mwokozi ya kushughulika na mwanadamu; ni kanuni inayopaswa kuletwa ndani ya kanisa” (The Adventist Home, uk. 198).

 

Hebu upendo wa Yesu na utubadilishe, utulainishe, na kutufanya kuwa wapole na wenye kujali. Hebu na nguvu yake ifanye upya mahusiano yetu ya nyumbani na ya familia, hasa mahusiano yetu na watoto wetu, ili kwamba iwe kwetu kama alivyosema, “Wote … watajua ya kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkipendana ninyi kwa ninyi” (Yohana 13:35).

 

Mwangaza wa Hubiri

 

Moja (1): Agano Jipya hutumia neno la Kiyunani agape kuelezea upendo wa Mungu.

 

Upendo wa Mungu wa agape hutofautiana na upendo wa kibinadamu kwa njia tatu:

 

  1. Upendo wa kibinadamu una masharti; upendo wa Mungu hauna masharti. Unamiminika kutoka kwake bila kujali wema wetu au thamani yetu (angalia Matendo 15:11; Waefeso 1:7; 2:8, 9; Tito 1:14).

  1. Upendo wa kibinadamu hubadilika; upendo wa Mungu haubadiliki. Upendo wake haushindwi (angalia Yeremia 31:3; Warumi 8:35-39; 1 Wakorintho 13:8).

 

  1. Upendo wa kibinadamu ni wa kibinafsi; upendo wa Mungu ni wa kujikana nafsi (angalia Wafilipi 2:6-8).

 

Udhihirisho mkuu wa upendo wa Mungu usio na masharti, usiobadilika, wa kujikana nafsi ulionyeshwa pale Yesu alipokufa kifo cha pili pale msalabani kwa ajili ya wanadamu wote (angalia Warumi 5:8; Waebrania 2:9) (Sequeira, 1993, uk. 27).

 

Mbili (2): Siku moja familia fulani ilitembelea maonyesho ya sayansi ambapo kila mgeni aliombwa kutazama picha kubwa iliyolingana na ukuta wa shamba lenye miti ya matunda iliyoanza kutoa maua. Kisha kila mgeni alipewa miwani ya kutazamia pande tatu (3D glasses). Chumba kilijawa na mishangao ya “Oh, Inapendeza namna gani!” “Tofauti ilioje!” “najihisi kama nipo katikati ya miti!” ilionekana kama matawi yalikuwa yametokeza kutoka kwenye picha na kufika kwenye vichwa vya wageni. Wengine walidhani hata wanaweza kunyoosha mikono na kushika maua yake. Miwani hii ya kutazama pande tatu (3D) iliwapatia kimsingi namna ya tofauti ya kutazama na kuhisi picha ile.

 

Tatu (3): Tafiti za hivi karibuni zinaonyesha kwamba kupoteza ndugu mliozaliwa pamoja kwa kifo ni moja kati ya majanga makubwa yanayoweza kusababisha kudhihirika kwa baadhi ya matatizo ya kitabia, kwa mfano kugombana, kutaka usikivu, kukosa adabu nyumbani, ukaidi, ukali, kujitambua, na kukosa msimamo. Watoto wa chekecheka, miaka 4 na 5, na watoto wa shule, miaka 6 hadi 11, walionyesha matukio mengi ya tabia za ukorofi kufuatia tukio kama hilo. Familia zilizofiwa … zinapaswa kuwa macho kwa ongezeko la mahitaji ya usikivu kwa watoto baada ya ndugu kufariki, na wanapaswa kuandaa wanafamilia wengine na marafiki kuwasaidia kutimiza mahitaji yaliyoongezeka ya watoto hao” (Growing Child Research Review, 1995, uk 4).

 

Nne (4): “Kadiri mzazi anaavyomtazama mwanaye machoni kama njia ya kuonyesha upendo wake, ndivyo mtoto anavyostawi kwa upendo na hisia zake hujaa zaidi… mara nyingi tunawapenda watu ambao wanaweza kututazama machoni. Kutazama machoni kunafurahisha, hakika, hasa pale kunaposindikizwa na maneno mazuri na tabasamu” (Campbell, 1988, Uk, 39, 40).

 

Tano (5): “Mawasiliano ya mwili yanayofaa na ya mara kwa mara na kijana wako ni njia ya muhimu ya kumpatia hisia ya kujua kwamba kweli unamjali. Hii ni muhimu hasa pale kijana wako anapokuwa sio muongeaji sana, mpole, mwenye hasira, au mwenye kujizuia. Katika nyakati hizi, kukutanisha macho kunaweza kukawa kugumu au hakuwezekani kabisa. Lakini mawasiliano ya kimwili yanaweza kutumika kwa ufasaha. Mara chache vijana huwa na mwitikio hasi pale anapoguswa kidogo begani, mgongoni au mkononi. Kwa mfano kijana wako amekaa kwenye kiti akitazama televisheni, kitu rahisi ni kumgusa begani unapompita …

 

“Hata pale kijana wako anapokua hatambui mawasiliano yako ya kimwili, kule kumgusa kunapeleka ujumbe wa upendo. Matokeo yake ni kumfanya ajihisi, ‘mama yangu na baba yangu wananipenda na kunijali, hata katika nyakati ambazo kuhusiana nao kumekuwa kugumu kwangu’” (Campbell, 1981, uk. 48,49)

 

Sita (6): “Sio upendo bali ni hisia zinazolaghai makosa, zinatafuta kwa kulaghai au kuhonga ili kupata makubaliano salama, na hatimaye kukubali mbadala mahali pa kitu kinachohitajika” (Education, uk. 290)

 

Saba (7): “Watoto hawapaswi kuachwa kwenda mbali na njia salama iliyoelezwa katika neno la Mungu, kuelekea katika njia zinazoongoza kwenye hatari, ambazo zipo wazi kila upande. Kwa upole, lakini kwa uimara, na ustahimilivu, na jitihada za maombi, shauku zao mbaya zinapaswa kuzuiwa, na matamanio yao kukataliwa” (The Ministry of Healing, uk 391)

 

Nane (8): Mwalimu alikuwa mkarimu na mwenye upendo kwa Yohana, kijana wa kiafrika aliyekuwa na matatizo na uhitaji mkubwa wa ukarimu na upendo. Siku moja alimletea zawadi ya urafiki, ganda la samaki lililokuwa zuri ajabu. “Umepata wapi ganda hili zuri la samaki?” mwalimu aliuliza alipokuwa akiichunguza zawadi hii.

 

Yohana alimwambia kwamba kuna mahali pamoja tu ambapo ndipo magamda hayo yanaweza kupatikana. Alipopataja mahali hapo, fukwe fulani kilomita kadhaa kwa umbali, mwalimu alibaki mdomo wazi. “Ni zuri sana, lakini usingeenda mbali namna hiyo kunitafutia zawadi.” Macho yake yakiwa yanang’aa, huyu mvulana wa kiafrika aliuliza, “Kutembea ni sehemu ya zawadi pia.” (Imechukuliwa kutoka Mala Power Follow the Year.)

 


Somo la Saba

 

NITAWAOKOA WATOTO WAKO

 

Na

 

Karen Flowers

 

Mkurugenzi, Idara ya Huduma za Familia, Konferensi Kuu

 

Na Idara ya Huduma za Familia, NTUC & STUM

 

Dondoo zifuatazo zinatoka katika kitabu cha ushairi kinachoitwa, “Although the Day Is Not Mine to Give, I’ll Show You the Morning Sun” (Pamoja na kwamba siku sio yangu, nitakuonyesha jua la asubuhi), kimeandikwa na kufafanuliwa na David Melton. Maoni yametolewa na Karen Flowers.

 

Mwanangu, Mwanangu, Siku zako za utoto zinapita haraka.

Kadiri majira ya mwaka yanapopita, ninaajiuliza kwa nini yanapita haraka hivyo  Ninajikuta, nikijiambia,“Kama ningeweza kuishi tena, Kwa namna fulani ningezikamata nyakati;”

Bila kujali, Ninawaruhusu wengine wapite wakati nikilitafakari hili.

Mambo mengi yanapora usikivu wetu: mashine ya kufulia lazima ilishwe, gari linahitaji matengenezo tena.

Ninatumai kwamba Katika miaka hii,

Nimeshughulikia zaidi ya magoti yaliyochubuka

Na vidole vilivyo na mikato.

Ninatumai kwamba mahali fulani, Katika kila siku,

Kwamba sijapuuzia mahitaji ya moyo wako,

Na ukuaji wako wa kiroho.

Ninatumai kwamba mahali fulani baada ya muda,

Kulikuwa na muda wa thamani fulani.

Na kama ingekuwepo ya kutosha …

Na kama ingekuwepo ya kutosha …

Na kama ingekuwepo ya kutosha …

Sijui sasa ningerejeshaje kwako.

 

 

 

 


Kuwa wa wazazi kwa wengi wetu kulionekana kuwa ni rahisi katika miaka ya awali. Katika mahangaiko ya kila siku, pale mambo yalipotulia katika ratiba tuliyozoea, tulijaribiwa hata kufikiri kwamba tunaweza tukajitahidi wenyewe. Kulikuwa na vitabu ambavyo tulisoma, stadi tulizojifunza, mafanikio yaliyoficha mapungufu. Lakini katika mshtuko wa nyakati ambapo homa ilipanda au mtoto alipogonga mguu chini na kwa jeuri kupiga kelele “Hapana!” hapo tulijua ni kiasi gani tulimhitaji Mungu. Kwanini tunasikia sauti ya Mungu pale tu kunapokuwa shida?

 

“Kumbuka,” maneno Yake hutukumbusha kwa upole, “Mimi ni mzabibu. Tawi haliwezi kuzaa matunda lenyewe; lazima likae ndani ya mzabibu. Ninyi pia hamwezi kuzaa matunda, msipokaa ndani yangu. Mbali ya mimi hamuwezi kufanya neno lolote.”

 

Maneno haya yanaweza kuvuta taswira ya Mungu akimkaripia mzazi kwa ajili ya maombi ambayo hayakuombwa, ibada zilizoacha kufanywa, misaada iliyopuuzwa. Lakini hebu faraja ya maneno yake ikufunike. “Tupo pamoja katika hili, Mimi na wewe,” ninasikia Mungu akisema. “Katika nyakati njema, tutajivunia wote na kutiwa moyo. Na nyakati zitakapokuwa ngumu, nitakupatia uwezo wa kuendelea kupenda. Shida yako siku zote itakuwa ni fursa kwangu.”

 

Uelewa wa Mungu kwa changamoto za malezi sio uelewa uliopatikana kwenye vitabu, au ufahamu tu wa kila kitu wa Mungu mwenye hekima juu ya yote. Amekuwepo hapa pamoja nasi. Ufahamu Wake ni kutokana na kushiriki uzoefu mbalimbali. Kumbuka anasema, “Naye Neno akafanyika kuwa mwili akaketi kati yenu.”

 

Mwaliko wake ni “Njoo kwangu unapokuwa umechoka nami nitakupumzisha. Kuwa na uhakika kwamba hauhitaji kuwa na wasiwasi kuhusu kile utakachokula au utakacho kunywa au utakachovaa. Maana wanadamu hutafuta vitu hivi. Lakini kumbuka, mimi ni mkate wa uzima. Yeye ajaye kwangu hataona njaa. Na yeye aniaminiye hataona kiu. Utafuteni kwanza Ufalme wa Mbinguni na haki yangu, na hayo yote mtazidishiwa, kwenu ninyi na watoto wenu.”

 

Jana, Uliniuliza maswali mazuri sana:

Kwa nini majani ni ya kijani?

Yule mtu aliingiaje kwenye TV?

Na …Mungu anafananaje?

Leo, Unauliza maswali ya akili inayochunguza:

kuna umbali gani kuelekea kwenye jua?

Kwa nini radi hutoa mwanga?

Na …Mungu anaishi wapi?


Kesho, Ninafahamu kutakuwa na maswali zaidi.

Baadhi, sina hamu ya kuyasikia.

 

Baadhi nitashindwa kuyajibu: Kwa nini anga limechafuka kahawia?

Kw anini mito inakuwa myeusi? Kwa nini bado kuna vita?

Na …Kuna Mungu kweli?

 

Kwanza kuna hamu ya kusikia maswali, mianzo ya mabadilishano ya lugha na uelewa kati ya mzazi na mtoto. Kisha kuna kukereka kwa maswali yasiyoisha kuazia jua linapochomoza hadi wakati wa kuingia kitandani na hata baada ya hapo. Kisha zinakuja changamoto za maswali ya akili zinazochunguza. Akili zinazochunguza yasiyochunguzika. Akili zinazochanganua kanuni zetu. Akili zinazobishana haraka kabla hatujafikiria vyema. Tunapata wapi majibu? Tutawezaje kushindana nao? Na bado tutawezaje kuwaachia wengine kuyajibu maswali yao hayo?

 

“Unajua kwamba,” Mungu amejibu, “kwamba Mimi ndio Njia, Kweli, na Uzima? Hakuna mtoto anayekuja kwa Baba ila kwa kupitia kwangu. Mnaniita Mwalimu na Bwana, na mnafanya vyema, maana ndivyo Nilivyo. Usijiulize utasemaje au utasema nini. Mantiki ya kibinadamu haitatosha. Omba, na utapatiwa maneno. Tafuta majibu, nami nitakuongoza katika kweli yote. Bisha, na milango ya hekima itafunguliwa kwako.”

 

Ninapojaza Siku zako za utoto Kwa zawadi za nyimbo za Krismasi na visa vya kufikirika, Lazima pia Nikuandae kwa uhalisia.

Lazima nikupatie vyote- Namna ulimwengu unavyopaswa kuwa Na jinsi ulivyo hasa.

Kukupatia vyote Kunaweza kukuchanganya, Lakini kupuuza vyote

Kutakudanganya kuhusu uhalisia wa maisha …

Nitakuongoza Kwa kipindi hiki kifupi,

Bila kufahamu endapo utakuwa au hutakuwa mmoja,

Katika kutengeneza mistari sawa ya wanadamu;

Au utakuwa mmoja,Na peke yako; Mtu mmoja

Wa kutengeneza njia mpya Kwa ajili ya wengine kufuata …

Katika miaka inayokuja, Nitaona ndani yako,

Taswira yangu mwenyewe. Ni wazo la kufurahisha

Ninapoelewa, Na ninapokuwa na mamlaka Dhidi ya mitazamo yangu.

Ni wazo lenye nguvu Na kuogofya Pale nitakapokuwa sipo …

Unapojiandaa Kutengeneza njia mpya Za kwako mwenyewe, Tunapokuja katika njia Ambayo wewe mwenyewe unaiona,

Au unapokuja kwenye kilima Ambacho wewe mwenyewe unaweza kukipanda, Ninaahidi kutokukuzuia.Badala yake, Nitakutia moyo kuendelea.

Hapatakuwa Na kwaheri Kati yetu, Hakuna kuagana.

Maana unapoondoka, Sehemu ya uwepo wangu Itaenda nawe, Na sitakuwa tena Mzima na kamili Hadi utakaporejea.

 

Kuwatazama watoto wetu wakikua huleta baadhi ya uzoefu fulani katika maisha, uzoefu wenye furaha na kuogofya zaidi. Lakini kama vile majani yanapoanguka kutoka kwenye mti wakati wa Hari, watoto wetu watavutwa katika miduara mipana zaidi ya kuchunguza na kuvutwa. Wakati ambapo mvuto wa mtu binafsi na matukio ya ajabu yanapokuwa na nguvu mtoto hujiweka huru kutoka kwenye nguvu zinazomfunga kwetu na anaruka kwenda kwenye mzunguko wake mwenyewe, hii huwakilisha moja ya mabadiliko makubwa kwa mzazi na mtoto. Mara nyingi huja ikiwa imefungamanishwa na hisia nyingi. Ni wakati ambapo wazazi wanapotathmini. Ulimwengu ambao tunapaswa kuwaachia watoto wetu una shida kuliko ule uliotegemeza mwanzo wetu kama watu wazima. Tumesema vya kutosha? Tumefanya vya kutosha kuwaandaa? Vipi kuhusu uzoefu pamoja kama familia? Ni kweli pamekuwa na nyakati nzuri, lakini vipi kuhusu uvunjifu wetu wenyewe na makovu yaliyobaki kwa watoto wetu?

 

“Kumbuka,” huja sauti ya faraja ya Mungu. “Mimi ni Mchungaji Mwema. Nimetoa uhai Wangu kwa ajili ya kondoo Wangu. Hakuna njia ambayo mwanao atapitia ambayo siifahamu. Utakaposhindwa kuwa pale ili kumvuta, nitaifanya njia ya kwenda mbinguni iwe ya kuvutia kama majani mabichi na maji matulivu. Utakapokuwa haupo kumwongoza, nitakuwa naye, hata katika mabonde ya uvuli wa mauti. Anapokwenda kinyume, kwa upole gongo langu na fimbo yangu vitamrudisha. Na kila zawadi bora unayotamani kwa ajili yake, nitambariki hadi kikombe chake kitafurika, hadi siku nitakayowaleta wote kuishi nami milele.

 

“Mimi ni Mwanakondoo wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu. Na kama Nikiinuliwa, nitawaleta kwangu. Mimi ni Alfa na Omega, Mwanzo na Mwisho. Kabla ya kuwepo kwa Abrahamu mimi nalikuwepo, Mimi Niko. Nitakuwa nanyi, hata mwisho wa dahari, na nitawaokoa watoto wako.

 


Somo la Nane

 

KAMA MAPACHA WANGEWEZA KUONGEA NASI

 

Na

 

Karen & Ron Flowers

 

Wakurugenzi, Idara ya Huduma za Familia, Konferensi Kuu

 

Na

 

Idara ya Huduma za Familia, NTUC & STUM

 

Mada Kuu: Uzoefu wa kifamilia wa Yakobo na Esau pamoja na wazazi wao, Isaka na Rebeka, hutupatia utambuzi kwa ajili ya wazazi wa kileo.

 

Fungu kuu: Mwanzo 25:27-34; 27:1-46; 28:1-9

 

Dondoo za Uwasilishaji: dondoo zilizowasilishwa katika kipengele hiki havihusishi mtiririko wa somo ulioandaliwa. Misaada ifuatayo imepangwa kutoa mpangokazi, nyenzo za kusaidia, na mifano kwa ajili ya kuandaa somo au masomo yanayohusiana na mada iliyotajwa. Unaweza ukataka kurekebisha mawazo haya kulingana na mtindo wako, ukitoa mambo kutoka katika kujifunza kwako mwenyewe na uzoefu wako ili kutimiza mahitaji mahususi ya kusanyiko lako. Pote katika maandishi yafuatayo, namba zilizo katika mabano (1), (2), (3) zitaonyesha mifano, nukuu na nyenzo zingine zinazopatikana katika kipengele cha Mwangaza wa Hubiri ambacho kitakuwa msaada katika maandalizi na uwasilishaji wa somo lako.

 

Majadiliano na watoto mara nyingi huwa na matokeo ya kushangaza, ya kufurahisha, wakati mwingine hata ya kushtua. Ni wawazi bila aibu. Ingekuwaje kama mada ya majadiliano ni malezi yetu kwao? Ingekuwaje endapo wana na binti zetu wangepewa sauti na lugha ya kueleza hisia na uzoefu wao katika nyumba zetu na sisi tukiwa kama wazazi wao? Unadhani tungesikia wakisema nini?

 

Leo tunataka kutembelea nyumba ya kale ya Isaka na Rebeka na kugundua kile ambacho mapacha hawa wa Agano la Kale, Yakobo na Esau, wanatushirikisha kutoka kwenye uzoefu wao wa kukua katika ile nyumba. Ili kuwa na uhakika, Yakobo na Esau hawakuwa watoto wadogo tena au hata vijana wadogo wakati wa lile tukio maarufu la haki ya mzaliwa wa kwanza na habari za supu ya dengu (Mwanzo 25:29-34) na ulaghai (Mwanzo 27). Walikuwa kwa wakati huu takribani miaka 75. Esau alikuwa ameoa, ana wake wawili nje ya imani ya kifamilia. Yakobo alikuwa mhuni. Hata hivyo, majibu  ambayo mapacha hawa walionyesha na mawasiliano ya wazazi kila mmoja na mwenziwe pamoja na mapacha hawa, yanafunua aina za tabia ambazo zilikuwa na mizizi katika miongo kadhaa iliyokuwa imepita.

 

Muonekano wa Familia 

Esau na Yakobo walikuwa ndio watoto pekee wa Isaka na Rebeka. Isaka mwenyewe alikuwa mtoto wa muujiza, kutimizwa kwa ahadi ya Mungu kwa Ibrahimu na Sara kwamba wangepata mtoto, hata katika miaka yao ya uzee (Mwanzo 17:17-19). Kwa hiyo swala kwamba alidekezwa tangu akiwa mdogo halikuwa na mashaka. Akiwa kijana, ni wazi kwamba aliwaamini na kuwa karibu sana na wazazi wake. Katika safari ya kwenda kutoa kafara mlima Moria, alikubali bila maswali jibu la baba yake mzee kuhusu Mungu kujipatia mwanakondoo kwa ajili yao. Baadae, bila ubishi alikubali, bila kukataa, kile kilichokuwa kwake uhalisia wa kushtua na kuogofya, kwamba alikuwa ndiye mhanga wa kafara. Alimruhusu baba yake kumweka kwenye madhabahu ya kafara (Mwanzo 22:7-9). Uzoefu wa kuwa karibu kabisa na kifo lazima ulikuwa wa kushtua na wakati huo huo wa kuijenga imani yake. Kwa namna fulani imani ya baba kwamba Mungu anaweza kama itahitajika, kumfufua kutoka kwa wafu (Waebrania 11:19) ilikuwa ndiyo imani ya mwana pia. Tunaweza tukadhani kwamba kile kinachofahamika kuhusu safari ya Moria kilipitishwa na Isaka kwa uzao wake na hatimaye kuandikwa na Musa pale alipokuwa akiandika kitabu cha Mwanzo. Baadae katika maisha, Isaka alikubali maamuzi ya baba yake na kusubiri kwa uvumilivu matukio kujifunua kadiri Ibrahimu alivyochukua jukumu la kumtafutia mke kupitia kwa ugeni wa mjumbe aliyeitwa Eliezeri, mtumwa wa baba yake, huko Mesopotamia ambapo ndugu wa familia yao waliishi (Mwanzo 24:2-4, 62, 63). (1)

 

Rebeka alikuwa ni binamu wa mbali wa Isaka. Alikuwa binti wa Betueli, ndiye aliyekuwa binamu wa kwanza kwa Isaka. Kulingana na kilichoandikwa kuhusiana na majibu yake kwa Eliezeri alipokuja nyumbani kwao huko Harani, alikuwa jasiri, mwenye kujitambua, anayechangamana na watu na aliyependa matukio mapya. Ni dhahiri alikuwa makini kiroho na mwenye imani. Je alisikia sauti ya Mungu katika sauti ya Eliezeri? Inaonekana aliisikia. Kuhusiana na mwenzi wake mtarajiwa, kwa kweli alifahamu tu kwamba, alikuwa ni sehemu ya familia yao kubwa na kwa sehemu ndogo, kile alichosema Eliezeri. Alikuwa na uwezo wa kufanya maamuzi yake mwenyewe, hata maamuzi ya mbali sana, kama alivyofanya alipojibu kwa utayari ombi la mjumbe huyu kwamba aende naye kama mke kwa ajili ya Isaka (Mwanzo 24:58). Kwa jinsi inavyofahamika, hakuwahi kurudi kwao au kuwatembelea ndugu zake tena. Maandiko yanaandika kuhusu harusi yao kwamba “Isaka akamwingiza Rebeka katika hema ya mama yake, Sara, akamtwaa Rebeka, akawa mkewe, akampenda; Isaka akafarijika kwa ajili ya kufa kwa mamake.” (Mwa. 24:67).


Inawezekana Rebeka alijaza pengo katika maisha ya Isaka lililoachwa na kifo cha Sara mama yake ambaye alimlilia miaka mitatu. Biblia haizungumzi zaidi kuhusu wanandoa hawa zaidi ya, “alimpenda …” kumbukumbu hii ya upendo wa wanandoa hawa ni ya pekee katika kumbukumbu za Biblia, sio kwamba wanandoa wengine hawakupendana, lakini hii imeelezwa waziwazi kwa suala la Isaka na Rebeka.

 

Kwa kipindi Fulani wanandoa hawa walipitia changamoto ya kukosa uzao. Lakini kama ilivyo kwa wanandoa wengi wa namna hii, waliomba kwa dhati kwa ajili ya watoto. Wakati mwingine, majibu ya maombi yetu tunayotamani hayaji. Lakini katika suala la Rebeka, alipata ujauzito (Mwanzo 25:21). Haukuwa ujauzito uliouwa rahisi. Alipata karaha nyingi kiasi kwamba aliiombea hali yake. Asili ya karaha hii ilikuja kufahamika kwamba alibeba mapacha! Mapambano yao ya kugombania maeneo wakiwa tumboni ilikuwa ni ishara ya mapambano yao ya baadaye kama mataifa mawili. Kisha Mungu akasema kitu ambacho hakupaswa kusahau kamwe: “Mkubwa atamtumikia mdogo” (Mwa. 25:23). Katika kujifungua, Esau alizaliwa kwanza; Yakobo baadae.

 

Jenga Uhusiano na Watoto Wako Wote

Kama Esau na Yakobo wangeweza kuzungumza nasi, wangeweza kutia mwanga matatizo yaliyokuwa ndani ya familia yao ambayo yalisababisha hatimaye Isaka kumpenda Esau na Rebeka kumpenda Yakobo (Mwanzo 25:28). Upendeleo unaweza kuanza pale mzazi anapoona katika mtoto mmoja furaha ya namna Fulani. Utaona kwamba nyie wawili “mnaelewana,” mnaongea pamoja kirahisi; mnaunganika kwa utayari zaidi. Wakati mwingine wale tunaowapendelea hufanana sana nasi. Cha kufurahisha ni kwamba Esau na Isaka walikuwa tofauti katika tabia na silika kama ilivyokuwa kwa Yakobo na Rebeka. Kila mzazi alivutwa kwa Yule aliyekuwa kinyume chake. Esau, asiyejali, anayependa mambo mapya, alipendwa na Isaka aliyekuwa mpole, anayependa kutafakari; Yakobo, kijana mkimya, aliyependa kukaa ndani, alithaminiwa kwa ukaribu wa uhusiano wa mama yake ambaye alimpenda.

 

Upendeleo unaoonyeshwa na wazazi huwafanya watoto kuwa katika upinzani usio wa muhimu kila mmoja dhidi ya mwenzake. Kuwa makini na mahitaji yao yanayotofautiana, lakini watendee kwa usawa kama walio sawa. Chukua hatua za muhimu za kutengeneza mahusiano na kila mtoto, hata pawe na changamoto kiasi gani kuhusiana na tabia yao mahususi au silika yao.

 

Kuwa Mtu wa Mabadiliko katika Familia Yako

Familia zote zina uwezo na familia zote zina changamoto. Nyuzi za mambo yote mawili zinaweza kuonekana wazi zikiwa zimefumwa katika vazi la historia ya kila familia. Baadhi ya familia huhamisha urithi wa uwezo. Wakati mwingine mapungufu ya kitabia hutiririka vizazi hata vizazi, kama vile unyanyasaji na ukatili, udanganyifu, au uzinzi. Katika vazi la familia ya Ibrahimu, upande wa Isaka, tatizo la kawaida la udanganyifu linajirudia tena na tena. Ilikuwa ni baba Ibrahimu mwenyewe aliyeiingiza familia nzima kwenye matatizo, mara ya kwanza kule Misri, na mara nyingine Kanaani, kwa sababu aliwaambia watumishi wa serikali kwamba Sara alikuwa dada yake, akiogopa kwamba wangemuua ili kumchukua (Mwanzo 12:11-20; 20:1-13). Kama baba alivyokuwa, naye mwana, yaani Isaka naye aliunda kisa kama hicho kuhusu mke wake, Rebeka, katika maeneo hayo hayo ya wafilisti (Mwanzo 26:7-10). Mwendelezo huu wa udanganyifu ni dhahiri pia katika familia ya Nahori (kaka yake na Ibrahimu), katika upande wa Rebeka. Labani (kaka yake na Rebeka) hatimaye alimlaghai Yakobo siku ya harusi yake, akampatia Lea badala ya Raheli, aliyekuwa bibi harusi mtarajiwa (Mwanzo 29:23-24). Raheli ambaye baadae alikuja kuiba vinyago vya kidini katika nyumba aliyokulia, akavificha chini ya matandiko ya ngamia na kumdanganya baba yake kuvihusu, “Bwana wangu asikasirike kwa sababu siwezi kuinuka mbele yako, maana nimeshikwa na mambo ya kike.” (Mwa. 31:35).

 

Israeli kulikuwa na mithali maarufu iliyosema, “baba wamekula zabibu mbichi, na watoto wametiwa meno ganzi” (Eze. 18:2). Msemo huu ulithibitisha uhalisia wa amri ya pili: urithi wa dhambi katika familia ulipasishwa kwa watoto. Kama vile mithali ilivyomaanisha, ilipelekea kuwalaumu wazazi kwa ajili ya hali aliyokuwa nayo mtu na kukwepa kuwajibika binafsi. Katika Ezekieli 18, kimsingi Mungu anatambulisha picha ya tofauti, akiwaambia Waisraeli kwamba hawakupaswa kunukuu mithali hii tena. Kila mtu anapaswa kuwajibika mbele za Mungu kwa ajili ya matendo yake. Sio sawa kuwalaumu tu wazazi wetu kwa ajili ya mapungufu ya tabia zetu. Kama watu wazima, ni lazima tufanye chaguzi zetu wenyewe na kuwajibika kwa matendo yetu (Eze. 18:20). Fungu hili pia huonyesha ukweli wa tumaini kwamba watu wanaweza kubadilika, pamoja na makosa, na unyasasaji, na maamuzi mabovu ya wazazi wao, na mapungufu ya kitabia yaliyopo katika familia. Kila mzazi ana fursa ya kuwa mtu wa mabadiliko katika ukoo, kuchagua kuondoa sumu za kale ndani yetu wenyewe, ili kwamba maji yaweze kutiririka kwa usafi katika vizazi vinavyofuata.

 

Tunasikia Yakobo na Esau wakiwasihi wazazi kubadili urithi wa kila aina ya maji ya sumu yanayotiririka katika familia. Kama sumu ni ulaghai, basi weka bwawa la kuzuia mtiririko huo katika familia vizazi na vizazi na kushughulikiana kwa uwazi na kwa uaminifu kila mmoja na mwingine kama wazazi na pamoja na watoto wenu.


Timiza Mahitaji ya Wazazi na Mahitaji ya Watoto kwa Ufasaha

Kadiri uhusiano wa vijana hawa ulivyokuwa wa kina zaidi, kila mmoja na mzazi aliyempenda, wanandoa walianza kuserereka taratibu kila mmoja mbali na mwingine. Kila mmoja alianza kupata maana ya binafsi kwa mtoto aliyempendelea. Maisha ya uzembe ya Isaka yaliangazwa na mawindo ya Esau na vyakula vilivyotokana na mawindo yake. Esau akakua bila kunidhamishwa, asiye na heshima, na asiyejali urithi wake. Isaka dhahiri hakuwahi kuonyesha kutokufurahishwa na ndoa ya Esau kwa wanawake Wakanaani (angalia Mwanzo 28:8). Kwa upande wake, Rebeka alihitaji Yakobo amtegemee. Bila kujali ni mkubwa kiasi gani, alidhamiria kumsimamia. Asingeweza kumkatalia mama yake; Rebeka alilenga kumfanya awe kiongozi wa familia.

 

Wazazi wote wawili bila shaka waliamini kwamba walikuwa kama wazazi katika uamuzi wao kwamba kijana wao mahususi ndiye angepata zawadi ya urithi. Isaka alitegemea kumpatia Esau uzaliwa wa kwanza kulingana na tamaduni. Rebeka aliamini kwamba Yakobo ndiye aliyechaguliwa na mbingu kwa sababu ya ufunuo maalum aliokabidhiwa na kwa sababu kijana wake mkubwa asiye na maadili alikuwa amekwisha dharau haki yake kwa kubadilishana na bakuli la supu ya dengu (Mwanzo 25:334). Kwa uhalisia, wazazi walikuwa wakijiangalia wenyewe badala ya kuwaangalia watoto.

 

Wazazi wengi huamini kwa makosa kwamba watoto wao wapo ili kutimiza mahitaji yao. Kinyume chake ndio ukweli. (2) Familia nyingi huchukulia amri isemayo “Waheshimu baba yako na mama yako” kuwa kanuni ya maisha inayowafunga watoto wao katika kuyaweka matakwa ya wazazi wao mbele. Wangeweza kuiweka katika maneno, Esau na Yakobo wangewasihi wazazi wao kutafuta msaada wa kiutu uzima kwa ajili yao wenyewe na kuwapatia msaada wao kulingana na umri wao. Shauri la Paulo linatenda kazi katika malezi pia, “Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.” (Wafilipi 2:4). Wazazi wengi hufanya kazi zaidi kwa watoto wanapokuwa watoto, hasa wakati ambapo vijana watu wazima na vijana wa kati, wanapohitaji uhuru wa kuishi maisha yao wenyewe. Wengine wengi hutafuta kutimiza mahitaji yao ya kiutu uzima kwa ajili ya malezi na upendo kupitia mapatano yasiyofaa na watoto wao.

 

Jali Ndoa Yako

Migogoro ndani ya ndoa ilikuwa wazi kati ya Rebeka na Isaka, huenda ikijitokeza kutoka kwenye tofauti zao. Alikuwa mchangamfu aliyependa kutoka, wakati Isaka alikuwa mpole zaidi, mkimya na mwenye kutafakari. Isaka alikuwa mtoto wa pekee, aliyezaliwa uzeeni, aliyekuwa akisikilizwa na kujaliwa sana. Rebeka alikuwa na ndugu na alizaliwa katika mazingira ya tofauti. Walikuwa na mitazamo iliyotofautiana katika maisha. Ni wazi suala la uzaliwa wa kwanza na kwamba ni nani apewe haki hiyo lilisababisha kufarakan kati yao. Hawakuwahi kulizungumzia. Isaka kwa dhana kwamba alikaribia kufa (pamoja na kwamba aliishi miaka mingine sitini), alipanga njamaa na akatenda kwa utaratibu ili kumpatia mbaraka wa uzaliwa wa kwanza Esau (Mwanzo 27:2). Familia haikualikwa katika tukio hili maalum. Hata Rebeka hakuambiwa. Alitega sikio na “akasikia kwa mbali” mazungumzo kati ya Isaka na Esau (Mwanzo 27:5, 6). Wanandoa hawa hawakuwa na mawasiliano na walikuwa wamefungwa katika vita vya mamlaka.

 

Tendo la kibinafsi la Isaka lilisababisha Rebeka kujibu mapigo. Yakobo kwanza alionyesha kukataa, kisha akamezwa na mbinu ya udanganyifu ya Rebeka. Kipengele hiki cha kusikitisha kilisababisha msongo zaidi na kuleta kuchanganyikiwa kwa wote kihisia pale nyumbani. Mawimbi ya hasira yaliifyeka familia. Kwa sababu ya vurugu hizo, Yakobo alikimbia nchi na alitengwa kutoka kwa familia yake kwa miaka mingi. Hakuwahi kumwona mama yake tena.

 

Hali ya familia hii ni ngumu, lakini katika kiini tunaweza kuona kazi ya msingi ya mahusiano ya ndoa katika familia. Ndoa ya mume na mke imefananishwa na mfumo wa joto nyumbani. (3) Ndoa yenye afya, ambapo kuna kukubaliana kila mmoja kama watoto wa Mungu, ambapo kuna kuheshimiana na mawasiliano fasaha, pale ambapo kuna upendo na ukaribu wa ndoa, pale ambapo tofauti hupimwa na kufurahiwa kwa sababu ya nguvu inayotokana nayo, hutengeneza uzoefu wa joto linalofunika nyumba. Kwa upande mwingine, endapo mgogoro utazidi katika uhusiano wa mume na mke, endapo wanandoa watapambana kwa mbinu za ulaghai, udanganyifu, na mapatano yasoyofaa na wengine ili kupata hisia ya mahali au kuchukua madaraka na mamlaka, ni dhahiri kwamba baridi itaingia nyumbani. Tabia za watoto mara nyingi huwa kama kipimo cha hali ya hewa iliyowekwa na ndoa. (4)

 

Moja kati ya ushauri wa muhimu zaidi kutoka kwenye kisa hiki ni kwamba baba na mama wanapaswa kufanya kila wawezavyo ili kuimarisha uhusiano wao kwa wao na kushughulika moja kwa moja pamoja katika kutatua migogoro na tofauti. Maelekezo ya Mathayo 18:15 kwa ajili ya kutatua migogoro huondoa mkanganyiko: ”Nenda ukamwambie kosa lake kati yenu wewe na yeye peke yenu.” Mungu anafahamu tabia ya kibinadamu ya kuunda pembetatu za kihisia, ambapo wawili ambao wana mgogoro humvuta mtu mwingine wa tatu. Anafahamu maumivu na msongo wa huyo mtu anayeingizwa katika mtego huu wa mgogoro kati ya watu wengine wawili, ambao wote wanaweza kuwa marafiki zake au ndugu zake. Mungu anatutaka tujifunze kuwasiliana na kuwajibika kutatua migogoro yetu moja kwa moja sisi kwa sisi, tuepuke kuwaingiza wengine bila sababu. Hii itafanya uhusiano wa familia zetu kuwa imara.

 

Kuanzisha Upendo Upya

Isaka na Rebeka walipooana, walipendana. Yakobo na Esau ni lazima walifahamu kisa cha upendo wao na ahadi yao ya kumwamini Mungu katika uchaguzi wa mwenzi wa ndoa. Wakiwa kama wanandoa wachanga, walikutana na changamoto ya kukosa uzao. Walifanikiwa kuvuka katika kipindi kigumu pale Isaka aliposaliti ndoa yake kwa kumdanganya Abimeleki. Walivumilia huzuni ya kupoteza na kutengana na wazazi. Pale magumu yanapoinuka katika familia, upendo wa wazazi kila mmoja kwa mwingine na ahadi yao ya kuyashughulikia ni muhimu zaidi. Bila shaka Yakobo na Esau wangeweza kuwatia moyo wanandoa, ambao mahusiano yao ni kama ya wazazi wao, wanapopitia katika magumu mengi. Wangewaambia kukumbuka upendo na ukaribu wao wa awali na kuurudisha na kuumba upya upendo ule. Ellen White anashauri mtu mmoja mmoja katika nyakati za giza,”tazama pale ulipoona mwanga kwa mara ya mwisho.” (5)

 

Hitimisho

Kipengele hiki kimeachwa kama maagizo kwa ajili yetu kutoka kwa Mzazi wa Kimbingu katika Neno Lake. “Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Rumi 15:4). Kwa mtazamo wa historia, tunaona kwamba Mungu hakutelekeza familia hii, pamoja na magumu yote. Alikuwa pamoja nao katika vurugu zote. Ahadi yake ya upendo na uaminifu inaendelea kuwepo na kusudi Lake lilitimia. Kama wazee wa zamani, sisi pia tunaweza tukamuamini Yeye.

 

Mwangaza wa Hubiri

 

Moja (1): “katika nyakati za kale uchumba wa ndoa kiwa kawaida ulifanywa na wazazi, na huu ndio uliokuwa utamaduni kati ya wale waliomuabudu Mungu. Hakuna aliyeruhusiwa kuoa yule ambaye hakumpenda; lakini katika kuonyesha upendo wao vijana waliongozwa na maamuzi ya wazazi wazoefu waliomcha Mungu. Ilichukuliwa ni kuwakosea heshima wazazi, na hata kuwa kosa la jinai, kufuata njia iliyokuwa kinyume na hii. “Isaka, akiwa anaamini hekima ya baba yake na upendo wake, aliridhika kumkabidhi suala hili, akiamini pia kwamba Mungu mwenyewe angeongoza chaguo litakalofanywa” (Patriachs and Prophets, uk. 171).


Mbili (2): “Wazazi wapo ili kuwahudumia watoto wao, na sio watoto kuwahudumia wazazi. Ni kanuni ya msingi ya maisha kwamba kizazi cha wakubwa lazima kiwe tayari kutoa kafara shauku zao kwa ajili ya kizazi cha wadogo” (Mace, 1985, uk. 109).

 

Tatu (3): “upendo kati ya Mume na mke utakuwa kwa familia kama vile mfumo wa joto ulivyo kwa nyumba. Utatunza uhusiano wa wanafamilia wote katika mandhari nzuri yenye uhuru” (Mace, 1985, uk. 109).

 

Nne (4): Wanandoa Fulani walijiuliza kuwa ni kwa nini vijana wao wawili; mmoja wa shule ya msingi mwingine wa shule ya sekondari walipigana pale baba yao aliporudi kutoka kazini, wakati muda mwingine wote walionekana kuwa na nidhamu. Mtiririko wa tabia ya kifamilia ulionekana kuonyeshwa kila wakati walipopigana: (1) baba aliporudi nyumbani, mama na baba walipokuwa wakikabiliana, walianza kwa kugombana; (2) watoto nao wakaanza kupigana; (3) tabia ya wavulana hawa humkasirisha baba ambaye hutoa nidhamu kali; (4) ukimya wa hasira unatawala kwenye nyumba; (5)mama na baba wanaacha kugombana na kila mtu anaendelea na shughuli yake. Wanandoa hawa waliweza kuona kwamba migogoro yao ya kindoa iliamsha mwitikio wa watoto. Mabadiliko ya makusudi katika uhusiano wa wazazi ambayo yaliweza kuonekana kwa wavulana hawa yalitiwa moyo kwa wazo kwamba hali hii ingeweza kuleta mabadiliko ya tabia kwa upande wa watoto. Hitaji la kupitisha picha ambayo kusababisha mama na baba kuacha kugombana kwao lingepungua.

 

Tano (5): “Pale majaribu yanapokufunika, pale ambapo wasiwasi, matatizo, na giza vinapoonekana kuzunguka nafsi yako, tazama mahali ulipoona mwanga kwa mara ya mwisho. Tulia katika upendo wa Kristo na chini ya ulinzi wake. Pale mapambano ya dhambi kwa ajili ya kuuteka moyo wako yanapojidhihirisha, pale hatia inapotesa nafsi na kulemea akili, pale kukosa imani kunapotia wingu akili yako, kumbuka kwamba neema ya Kristo yatosha kushinda dhambi na kuondoa giza. Tunapoingia katika mahusiano ya Mwokozi, tunaingia katika eneo la amani” (Ministry of Healing. Uk. 249).

 

 


Somo la Tisa

 

MWANGA WA MUNGU KATIKA MACHO YA MTOTO

 

Na

 

Audray Johnson

 

Mkurugenzi, Idara ya Huduma za Familia, Konferensi ya Kusinimashariki

 

California Divisheni ya Amerika Kaskazini

 

Na

 

Idara ya Huduma za Familia NTUC & STUM

 

 

Mada Kuu: Maendeleo ya kiroho ya watoto wetu ni sehemu muhimu ya malezi na ni kazi ya kanisa. Watu wazima wana wajibu ulio chanya wa kuwezesha imani ya watoto kwa Mungu na kuepuka mitazamo na tabia zozote zitakazowasababisha watoto kujikwaa.

 

Fungu Kuu: Marko 9:36-42

 

Dondoo za Uwasilishaji: Katika orodha ifuatayo, namba zilizo katika mabano (1), (2),

 

(3)   zitamaanisha vitu kutoka kwenye kipengele kinachoitwa Mwangaza wa Somo ambacho kitatumika kwa ajili ya mifano. Nyongeza ya mifano yako mwenyewe itakuza uwasilishaji.

 

Kama ilivyo kwa Wakristo wengi, Waadventista Wasabato wamekuwa na shauku kuhusu kujengwa kwa tabia ya watoto wao. Kiwango cha fedha tunachotumia kwa ajili ya elimu ya watoto wetu katika shule, taasisi, na vyuo vingi vya dini tulivojenga hudhihirisha jinsi tunavyo wachukulia watoto wetu kwa uzito. Tunataka wakue na kuwa Wakristo. Tunataka wakue katika kanisa tunalopenda na kuamini kama tunavyoamini. Tunataka waokolewe. Tunataka waende mbinguni. Kwa hiyo tunajitoa kafara makusudi kabisa, tunaishi kwa shida, tunaacha kufanya manunuzi makubwa, wakati mwingine hata tunafanya kazi za ziada ili tu tuweze kuwahudumia.

 

Pamoja na shauku zetu na uwekezaji wetu kwao, tunaelewa kwa uchungu kwamba watoto wetu wengi huchagua kufuata njia tofauti na ile tuliyodhani itafaa kwa ajili yao. Wengine wanaonekana kuhitimu kutoka kanisani wanapokuwa wamemaliza vyuo na taasisi mbalimbali. Ni nini kinachotokea? Kwa nini wale waliokuwa na furaha sana hapo mwanzo kulitaja jina la Yesu sasa wanaonekana kuwa mbali sana Naye sasa?

 

Majibu ya maswali ya kwa nini watoto wakubwa na wanaopevuka hufanya chaguzi wanazofanya ni dhana ngumu sana. Jambo moja la muhimu ambalo lazima lifanyike ni kwamba maendeleo ya kiroho sio sawa na kutia kasumba. Uzoefu wa kidini kwa vijana wengi umekuwa wa kutia kasumba badala ya maendeleo ya kiroho. Karibu kila mtu anaweza kujifunza seti ya kanuni au kukariri matamko ya mafundisho fulani, lakini uhusiano ulio hai na Yesu, pamoja na kwamba unahusisha uelewa wa mafundisho, kwa hakika ni zaidi, zaidi sana ya hivyo tu.

 

Yesu Aliwaheshimu Watoto

 

Yesu alijitambulisha kwa karibu sana na watoto. Yesu aliwaheshimu watoto na akatufundisha kuhusu ukuaji wao wa kiroho. Wakati Fulani, Alimwita mtoto, akambeba mikononi mwake na kusema, “Mtu akimpokea mtoto mmoja wa namna hii kwa jina langu, anipokea mimi; na mtu akinipokea mimi…“ (Marko 9:37). Yesu alisema kitu cha kushangaza namna gani! Jambo hilo lilikuwa na uhusiano gani na ufalme mpya? Mtu anaweza akasikia baadhi ya wanafunzi wake wakifiria, “Huyu anajua nini kuhusu watoto wadogo? Anafahamu vurugu wanazoweza kufanya hawa, au ni gharama kiasi gani kuwalea, au jinsi ada ilivyo pale kwenye shule ya sinagogi?”

 

Yesu aliikuza imani ya watoto. Fungu linaloendana na hilo huongezea mawazo ya ziada, “akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 18:3). Inashangaza jinsi gani kwamba Yesu aliinua imani ya mtoto kiasi cha kuwa na kiwango cha kuingia katika ufalme! Watoto wanamwamini Mungu? Yesu alidumu kusema ndio. Tazama maneno yake, “…mmojawapo wa wadogo hawa waaminio…” (Marko 9:42).

 

Mwanasaikolojia wa watoto, Robert Coles (1990) alifanya utafiti wa kuvutia ambapo aliwahoji watoto wenye historia mbalimbali: Wakatoliki, Wabaptisti, Wamethodisti, Wayahudi, Waislamu, Wabudha, Wamarekani wa asili, Wapagani, na hata Waadventista Wasabato. Kile alichojifunza ni kwamba watoto, hasa wale walio katika miaka ya awali ya kupevuka, katika hali halisi, wana maisha hai ya kiroho na wanaelezea dhana kwamba Mungu ni wa muhimu katika maisha yao. Watu wengi ambao wametenga muda kwa ajili ya kuwasikiliza watoto hawatashangazwa na jambo hili. Inawezekana kwamba tumeshindwa kuelewa umuhimu wa kazi ya Roho Mtakatifu katika maisha ya hawa walio wadogo kati yetu, kazi ambayo inafanyika hata kama tutaelezea kisa cha Yesu ama la; ikiwa tutawajaza mafundisho au la? Tumekosa dhana kwamba Mungu anajaribu kuwafundisha hawa walio wadogo, wowote au popote walipo? Kwa nini sisi hatufanyi hivyo? Kwa nini Mungu asifanye hivyo, yeye ambaye anamimina neema yake kwa wanadamu wote, aone kwamba kuna thamani kufanya kazi na fikra za mwanadamu ambaye ni mchanga, mwenye akili mpya, ambazo zinaweza kusikia kwa utayari zaidi sauti yake? (1)

 

Yesu alionya kuhusu kuwafanya watoto watende dhambi. Katika mafungu ya awali ya Marko 9, tunakuta kwamba wanafunzi walikuwa na mgogoro wa nani awe mkuu na walikuwa kwa namna Fulani hawajaridhishwa na fundisho la Yesu, kama ilivyoonekana katika jibu lao. Mtume Yohana alibadili mada, akileta tukio la mtu ambaye wanafunzi walimkemea kwa kutoa mapepo kwa jina la Yesu. Yesu alimheshimu Yohana kwa kutoa jibu fupi, kisha akamrudisha yeye na mitume wengine nyuma kwenye jambo alilosema kuhusu watoto. “Na ye yote atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini.” (Marko 9:42).

 

Yesu anazungumzia nini anapotamka matokeo ya kutisha namna hii juu ya Yule anayemkosesha mtoto? Ina maana gani kumfanya mtoto atende dhambi? Ni wazazi wachache ambao kwa makusudi wanaweza kumfundisha mtoto kuiba, kuua, au kutenda dhambi zingine. Yesu lazima alikuwa akimaanisha kitu tofauti na hicho. Inawezekana kwamba Yesu anachukulia kuwakosesha watoto kuwa kitu chochote ambacho kinaathiri vibaya imani ya mtoto wake? Ni dhahiri Yesu anamaanisha mtazamo na matendo yanayomwongoza mtoto mbali na Mungu, yanayomkatisha tamaa, au yanayoelekeza katika jambo ambalo litafanya iwe vigumu kwa mtoto kumwamini Mungu wa upendo na wa neema. Yesu aliwataka wale walio wakubwa kutia moyo ukuaji wa kiroho wa watoto wetu na watoto wengine wote kanisani kwa kuwafundisha, kwa mifano ya neema, upendo, amani, furaha na shuhuda zote za tunda la Roho wa Mungu aliyeko ndani. Kuna njia kadhaa za kiutendaji tunazoweza kupitia ili kufanya hivi.

 

Kulinda Ukuaji wa Kiroho wa Mtoto

 

Mpatie mtoto wako usalama kihisia. Ikiwa itaonekana ni salama kuzungumzia jambo lolote nyumbani, kwa utulivu unaoeleweka, watoto watajifunza kuwa huru kuzungumza jambo lolote na Mungu. Kama ni salama kuzungumza mambo katika Shule ya Sabato na viongozi wakiwa huru kutenda kazi na akili zinazojifunza na kuuliza maswali, basi itakuwa rahisi kwa mtoto au kijana kuleta shauku zake kwa Mungu. Hata hivyo, endapo hasira na kupiga kelele kumekuwa ndio mfumo wa maisha ya nyumbani, kama wazazi na waalimu wanapata usumbufu au kushtuliwa au kuwa na hasira dhidi ya akili ndogo zenye maswali, itakuwa vigumu zaidi kwa mtoto kuamini kwamba kila kitu kinaweza kuletwa kwa Mungu. Ile sauti ndogo, tulivu ya Mungu inaweza ikamezwa na sauti za hasira, na za maumivu za wazazi na ndugu.


Mtoto anayekuwa katika mazingira yenye matusi huachwa akiwa na njaa ya amani, usalama wa kihisia, na mtu fulani wa kumsikiliza na kumchukulia kwa uzito. Mara kadhaa anaweza kujaribu kushibisha njaa hiyo kwa uzoefu fulani wa ajabu wa kidunia au katika safari ya kiroho ya kutafuta kwa undani.

 

Tia moyo imani ya mtoto wako. Pale ambapo nyumbani panakuwa mahali pa kujali ambapo mahitaji ya kimwili na mahitaji mengine hutimizwa, watoto hujifunza kwa utayari kwamba Mungu anaweza kutegemewa na kuwajali. (2) Lakini je, vipi kuhusu wale ambao wamepuuzwa? Watajifunzaje kwamba Mungu kweli hutupatia mahitaji yetu yote?

 

Ukuze hisia za kujithamini kwa mtoto wako. Kujithamini kulikostawi kunaundwa pale watoto wanapopewa uhakikisho na vijana wanapotiwa moyo (na pale mama, baba, bibi, babu wanapohakikishiana!). pale watoto wanapoeleweshwa jinsi walivyo wa thamani kwa walezi wao, itawasaidia kuelewa kwamba Mungu anawathamini pia. (3) Lakini, maneno ya kukatisha tamaa, na mbaya zaidi, matendo ya kuharibu nafsi yanaweza kutamkwa bila kutafakari na kwa kuropoka. “Huwezi kufanya jambo lolote vyema!” “Unakuwaje mjinga namna hii?” “Ninatamani usingezaliwa.” Na mengine mengi ya jinsi hiyo. Wazazi wengi ambao ni Waadventista wa Sabato huona ni rahisi tu kumpakia mtoto wao kwa mafungu ya Biblia kichwani au kwa nukuu za Mama White. Watoto ambao wanaoshambuliwa kwa namna hii hupata shida kupata hisia za kuthaminiwa na yeyote, na zaidi sana Mungu wa ulimwengu.

 

Tumia nidhamu inayofaa kwa mtoto wako ili kukuza nidhamu binafsi na heshima. Watoto wanapofundishwa kuanzia umri wa awali kabisa kupitia nidhamu ya upendo inayofaa, wanajifunza kupangilia maisha yao kwa nidhamu binafsi. Wanajifunza jinsi ya kuishi chini ya mamlaka ya Mungu na kuheshimu ipasavyo mamlaka za kidunia. Kila mmoja, pamoja na mtoto, hujifunza heshima kwa kuheshimiwa. Kufundisha heshima kwa watoto kunaweza kufanyika kwa ubora zaidi kwa kupata heshima yao.

 

Madhara Yaliyosababishwa na Unyanyasaji na Ukatili ndani ya Familia

 

Kukosa nidhamu-binafsi. Endapo watoto watatawaliwa na adhabu, mapigo na unyanyasaji mwingine wa kimwili, itakuwa ngumu sana kujifunza nidhamu binafsi.

 

Mtazamo uliodhoofishwa juu ya Mungu. Jambo baya zaidi katika uzoefu wao wa kiroho ni kwamba, katika akili zao, Mungu atakuwa ameshikilia kiboko kubwa kuliko zote. Watu wazima wengi wamekuwa wakipambana maisha yao yote kuhusiana na Mungu kama Mungu wa upendo. Wakiwa wamechanganyikiwa, wanaweza kuwa wametulia katika uelewa wa kiakili kwamba pengine Mungu anawapenda. Hata hivyo, hawawezi kukimbia hofu kwamba, kama tu wakitoka nje ya mstari, Mungu yupo tayari kutoa adhabu kali.

 

Watu wengi katika jamii leo wamedhihirisha shauku kubwa juu ya kukua kwa tabia za ukatili, hasa kati ya vijana. Wanaamini kwamba kinachohitajika ni “kurejeshwa” kwa adhabu za viboko. Katika kuvunjika kwao moyo, wananchi hawa wenye nia njema wanasahau kwamba wakosaji wabaya zaidi mara nyingi ni wale watu ambao tayari wamepigwa na kunyanyaswa mara nyingi bila idadi.

 

Maendeleo ya tabia yaliyofungiwa. Tafiri za hivi karibuni zinaonyesha kwamba kadiri adhabu kali zinavyotumika, ndivyo nafasi ya maendeleo ya tabia inavyozidi kupungua. Wakristo hawapaswi kushangazwa na hili kwa sababu ya uvumilivu na ustahimilivu wa Mungu na kunyamaza kwake katika kuwaweka watu wake anaowapenda kwenye kurekebishwa kwa ukali, lakini historia inatupatia maelezo ya kusikitisha juu ya matumizi ya adhabu kali kutoka kwa Wakristo. Waadventista wa Sabato wanapaswa kutokushangazwa kabisa, maana tuna ushauri mahususi kutoka kwa Ellen White kuhusu matokeo mabaya, na adhabu kali za viboko. (4)

 

Ongezeko la mapambano. Ellen White aliwahi kusafiri kuelekea magharibi kwa treni. Katika kituo kimoja, usikivu wake ulivutwa kwa mama aliyekuwa akisafiri na watoto kadhaa, na mmoja wao alikosa heshima. Mwanamke huyu alikuwa akimpigia kelele kijana wake, akimpiga, na kumtishia kwa kila aina ya adhabu watakapofika nyumbani. Taswira yote inatukumbusha vipengele ambavyo tumekuwa tukiviona katika maeneo ya umma leo! Mama White, hata hivyo alikuwa na ujasiri wa kwenda kukaa na huyu mama, kusikiliza matatizo yake na kuzungumza naye. Kati ya vitu ambavyo Mama White alisema ni, “Ukatili utaongeza tu mapambano na kumfanya awe mbaya zaidi.” (5) cha kushangaza, hicho ndicho wanasayansi wa tabia wanachojifunza leo! Wapatie Watoto Aina ya Mguso ulio Sahihi

 

Matokeo ya mguso wa upendo. Pale ambapo mguso wenye afya, unaofaa unapokuwa sehemu ya kawaida katika familia, watoto katika familia hujifunza upendo na kuurudisha tena. Kule kukumbatia kwa upendo na busu, kumkumbatia mtoto kwa karibu, kuwasomea, kuwaambia visa, zile nyakati za upole ambazo watoto hujihisi kupendwa, hizo ndizo nyakati ambazo watoto hujifunza kuhusu upendo. Upendo wa wazazi na wa wanadamu wengine hufundisha kuhusu upendo wa Mungu. Watafurahia visa vya Yesu aliyewabeba watoto mapajani mwake. Watachukua katika utu uzima wao dhana kwamba Mungu anawafurahia, na anawapenda.


Usaliti wa unyanyasaji wa kingono. Pale unyanyasaji wa kingono unapotendeka, hasa unapofanywa na mzazi, mtoto anawezaje kujifunza maana ya mahusiano na upendo mkamilifu wa Mungu? Ni watu wazima wangapi ambao bado wanapambana na jambo hilo leo! Wale tu waliopitia uzoefu wa unyanyasaji wa kingono ndio wanaoweza kuelewa kwamba neema ya Mungu huwasaidia kuvuka, kamwe maumivu ya uzoefu huu hayapotei kabisa. Usaliti wa namna hii huingia katika sehemu ya ndani zaidi ya nafsi na kuweka makovu mabaya kabisa.

 

Hitimisho

Hitimisho ambalo tunafikia ni kwamba Yesu anachukulia kuwakosesha watoto kwa uzito kiasi kwamba ameweka matokeo mabaya zaidi kwa wale wanao wakosesha. Ni Muhimu kuwa na nidhamu na mpangilio nyumbani au katika jamii, lakini mafundisho kama hayo na nidhamu lazima viwe katika muktadha wa neema. Mara nyingi ni ngumu kujifunza kufanya mambo kwa njia tofauti na ile tulivyofanyiwa. Wazazi wengi hufanya mambo kama wazazi wao walivyofanya. Kutoka kizazi hadi kizazi tabia zimekuwa zikirithiwa, na mpangilio wa tamaduni ni mgumu sana kuuvunja. Lakini Yesu anakuja na kututaarifu kwamba hata katika miundo ya tamaduni zetu, sisi ni wa tofauti! Tunaweza kupitia nguvu tuliyopatiwa, kujifunza njia za ufalme wa Mungu.

 

Mungu ametuita kumtumikia kwa moyo wa upendo. Ametuita kuuhamishia ule upendo kwa watoto wetu na watoto wa watoto wetu. Kuanzia na nyakati zile ambazo mtoto wetu anapokuwa kwenye kitanda cha kitoto, tuliwafundisha thiolojia tulipowabeba. Sisi wenyewe tulipolia kwenye kitanda chetu cha kitoto tukainuliwa na kupigwa busu, tulijifunza kwamba tunapendwa. Tunawafundisha watoto wetu kwamba wao ni watakatifu tunapowafanyia hivyo hivyo.

 

Yesu alikuwa na upendo wa kina sana kwa watoto. Walikuwa na nafasi maalum katika moyo wake na aliwachukulia kama mifano katika uwanja wa Mungu, imani takatifu inapaswa kuchukuliwa kwa upendo na huruma. Hali yao ya kutokuwa na hatia, urahisi na imani ya mtoto hufunua ukubwa wa Mungu kwetu pia pamoja na kutupatia mwangaza wa jinsi maisha ya kibinadamu yanavyopaswa kuwa. Furaha inayoambukiza hufariji na kuinua nafsi zetu. Uwezo wao wa kuvuta usikivu wa upendo ni kama ule wa Mungu, ambaye upendo wake hutuvuta kutoa mwitikio wa upendo. Waacheni watoto wadogo waje kwangu, kwa maana ufalme wa mbinguni ni wao.


Mwangaza wa hubiri

 

Moja (1): Timothy aliyekuwa na miaka mitatu alikuwa na siku mbaya. Kwa kweli, majuma mengi yaliyopita yalikuwa magumu kwa sababu ilimbidi baba yake kwenda hospitalini tena na tena kwa ajili ya Tiba ya kansa. Safari hii, hata hivyo, ilionekana hata kwake kwamba baba alikuwa anaumwa kweli. Alianza kupata wasiwasi kwamba baba yake angekufa. Nje kwenye majani ya hospitali alilia na kupaza sauti na akakataa kuingia kwenye gari kuelekea nyumbani. Alitaka kurudi ndani na kuwa na baba yake. “Baba anaumwa sana. Hatapona na sitakuwa na baba,” alilia. Ilinichukua muda mimi, bibi yake kumfanya atambue kwamba baba yake alikuwa ni mvulana wangu mdogo na kwamba hata mimi nilikuwa na huzuni pia. Kugundua kwamba kuna mtu mwingine ambaye alishirikiana naye huzuni yake kulisaidia kidogo. Alikubali kwenda nyumbani nami kwa gari. Kote njiani mimi na mtoto huyu wa miaka mitatu tulizungumza habari za Ayubu, kwa sehemu kuhusu sehemu yetu. Yalikuwa ni mazungumzo ya kiutu uzima kuhusu maumivu na mateso na sisi na Mungu, ila tu kwa misamiati ya kitoto.

 

Sikutambua kile mazungumzo hayo yalimaanisha kwa Timothy hadi baadae nilipokuwa ninaoga na kujaribu kuondoa huzuni yangu pamoja na uchafu na jasho la siku hiyoo. Nikiwa hapo nikasikia sauti ndogo kutoka upande mwingine wa pazia la bafni. Timothy alikuwa hapo bafuni, karibu yangu, akiimba taratibu, “Msifuni, Msifuni, Msifuni, enyi watoto wote.” Aliimba wimbo huu wa watoto muda wote. Lakini hakuwa amemaliza. Alipokuwa akichezea kidude chake cha kuchezea bafuni, kibata kidogo cha mpira, alisema taratibu, “ninakupenda Mungu.” Wakati mtakatifu! (dondoo ya mhariri: Bibi yake Timothy ni Audray Johnson[mtunzi wa somo], na baba yake yupo nyumbani na anaendelea vizuri.)

 

Mbili (2): Rabi Bradley Arnston wa Mission Viejo, California, analinganisha jinsi anavyochukulia gombo la Torati na jinsi anavyomchukulia mtoto. Wakati ambapo rabi na wazee wanapoingia katika sinagogi wakiwa na Torati takatifu, wanaibeba mikononi kama mtoto. Wanaifungua (kama kumvua ngua), wanaibusu, wanaisoma na kisha wanaifunga tena kwa makini na kwa upendo. Kisha wanaibeba kwenda kwenye “kitanda chake.” Rabi Arnston anasema, hivi ndivyo tunavyopaswa kuwachukulia wale wadogo tuliopewa.

 

Tatu (3): Rex Johnson, mchungaji na mtaalam wa matibabu kutoka Long Beach, California, anapendekeza kwamba tunaweza tukapata njia za ubunifu za kutamka kwa dhati kwa watoto wetu. Kwa mfano, “Siku moja nitajivunia kukubebea mkoba wako!” kuwalinganisha watoto wetu na maduka mazuri au vitu vya gharama kunaweza kuleta njia mpya za kudhihirisha thamani yao. “Una akili kama ya Neiman-Marcus!” (Labda uchaguzi wako unaweza kuwa Obama, Samia S. Hassan, Mo Dewji au duka bora zaidi au kitu chenye ubora zaidi ambacho familia yako inakifahamu.)

 

Nne (4): watoto wako ni mali ya Mungu, walionunuliwa kwa gharama. Muwe mahususi kabisa, nyie akina baba na akina mama, katika kuwatendea kwa namna Kristo alivyowatendea. (Child Guidance, uk 27)

 

Utii kamili katika familia yako; lakini unapokuwa ukifanya hili, mtafute Bwana ukiwa pamoja na watoto wako, na mwombe aingie na atawale. Watoto wako wanaweza kuwa wamefanya jambo linalodai adhabu; lakini ukishughulika nao kwa roho ya Kristo, mikono yao itaruka kukukumbatia; watajinyenyekeza mbele za Bwana na watatambua kosa lao. Hiyo inatosha. Hawahitaji kuadhibiwa. Hebu na tumshukuru Bwana kwamba amefungua njia ambayo kwayo tunaweza kuifikia kila nafsi.

 

Kama watoto wako sio watiifu, wanapaswa kurekebishwa … kabla ya kuwarekebisha, nenda mwenyewe, na muombe Bwana kulainisha na kutawala mioyo ya watoto wako na kukupatia hekima ya namna ya kushughulika nao. Sijawahi hata mara moja kuona mbinu hii ikishindwa. Hauwezi kumfanya mtoto aelewe mambo ya kiroho wakati moyo unasongwa na hisia kali. (Child Guidance, uk. 244)

 

Tano (5): aina ya serikali ya huyu mama iliifanya akili yangu kujifunza. Aliwalazimisha kwa njia kadhaa zisizofaa, hii ilionyesha kwamba usimamizi wa huyu mama ulishindwa … yote ambayo huyu mama alionekana kufahamu kuhusu usimamizi ni kulazimisha kwa nguvu tu. Alikuwa akitishia, akiogofya. Mtoto wake mdogo kabisa alionekana kuogopa kuanzisha chochote. Wengine walionekana wagumu na wakaidi. Wengine walionekana kuona aibu na kuchoshwa.

 

Nilitamani kumhubiria Yule mama somo. Nilifiria endapo Yule mama angejua wajibu wake kama mama, asingefuata njia aliyokuwa anafuata katika treni ile … kila neno la ukali, kila pigo, lingemrudia tena. Kama angekuwa mpole na mvumilivu na mkarimu katika nidhamu yake, nguvu ya mfano wake kwa ajili ya wema ingeonekana katika tabia za watoto wake … ni nafsi ngapi ambazo wanawake kama hawa wangezileta kwenye kundi la Kristo, ni swali. Siamini kweli kama wangeleta hata nafsi moja kwa Yesu. Wanafundisha, wanatawala, wanaharibu. (E.G. White, nukuu ya Adventist Heritage, Summer, 1990, uk. 26)

 

 Somo la Kumi

 

MFANO WA BABA MZURI SANA

 

Na

 

Danie swanepoel

 

Mkurugenzi, Idara ya Huduma za Familia, Union Konferensi ya Afrika Kusini

 

Na

 

Idara ya Huduma za Familia, NTUC & STUM

 

Mada Kuu: Baba wa Mbinguni hutazama kila siku “njiani,” tayari kuwakaribisha wana wapotevu.

 

Fungu Kuu: Luka 15:11-24

 

Katika mifano mingine ya upotevu, Yesu alieleza kuhusu kondoo aliyepotea bila kutarajia na sarafu iliyopotea kwa uzembe. Mfano huu wa mwana mpotevu, kwa kulinganisha, ni upotevu wa hiari, upotevu kwa uchaguzi wa makusudi. Kijana huyu anavunja makusudi vifungo vya nyumbani. Anaona amekua na anaweza kuwajibika kwa chaguzi na matendo yake mwenyewe. Anafanyia kazi uhuru wake, jambo ambalo Mungu mwenyewe haingilii. Anachagua kuondoka nyumbani, na yeye mwenyewe ndiye anachagua kurudi nyumbani. Ni pale tu anapomwona mwanaye kwa mbali ndipo Baba anakwenda kukutana naye.

 

Uchaguzi wa Mwana

 

Amefikia umri ambao anadhani kuwa anafahamu kuliko baba yake. Amechoka vifungo vya nyumbani. Amechoka kuchungwa na baba yake. Anataka uhuru. Anataka kufurahi. Amesikia kuhusu raha za nchi za mbali. Nia ya nafsi yake inajielekeza zaidi katika moyo wake. Anafanya vile anavyopenda. Atafuata njia zake mwenyewe. Anadai mgao wa mali. (sheria ya Kiyahudi ilimpatia kijana mkubwa sehemu mbili ya tatu ya urithi wa familia. Ana haki ya kushirikiana sehemu yake, lakini sio wakati baba yake akiwa hai.) moyo wake tayari upo katika nchi ya mbali. Miguu yake kwa hakika ilikuwa tayari kufuata.


Katika Kuwa Mwana Mpotevu

 

Mtu huwa mwana mpotevu katika hatua za taratibu. Mabadiliko haya hutokea kwa hatua. Kwanza mtu huwa mwana mpotevu moyoni, kisha kiuhalisia. Badiliko hili sio lazima lidhihirike mara moja, lakini haliepukiki pamoja na kwamba viashiria huanza kuonekana na hali ya moyo hudhihirishwa katika mitazamo na tabia.

 

Matokeo Magumu

 

Katika nchi ya mbali “anaharibu mali yake kwa maisha ya anasa na starehe.” Ana gari bora na farasi wenye kasi zaidi mjini. Anaishi kwa kufuata mtindo, anatumia kwa uhuru. Anafurahia uhuru wake. Hakuna vikwazo vinavyokaba, hakuna mivuto ya kumpatia hatia, hakuna tahadhari za kuchukua. Marafiki ni wengi hawezi hata kuwahesabu. Anaishi maisha ya starehe na anasa bila kujizuia, akimsikitikia kaka yake aliyebaki nyumbani.

 

Kama inavyokuwa mara nyingi pale tunapofuata mivuto ya shetani, pale tu tunapofikiri kwamba tumepata vyote, majaliwa hufunua uhalisia wa hali yetu (Ufunuo 3:17). Ile mali ikaisha, na njaa ikaingia. Mwana mpotevu akajikuta hana hata senti mtaani. “marafiki” zake wamemwacha kwenye vumbi. Kitu pekee anachoweza kushika katika maisha yake ni kulisha nguruwe wa mtu na kujilisha wa mabaki ya chakula cha nguruwe.

 

Kujiangalia Sana Katika Kioo

 

Kufikia hapa kwenye kisa hiki, mwana mpotevu anakuwa na sura ya ‘nipe’ ili ‘kunifanya’. “Nipe” huwakilisha mfano wa nia ya nafsi. ‘nifanye’ huwakilisha kusalimisha nia yake. Maandiko husema kwamba mwana mpotevu “alijitambua.” Labda alijiangalia sana kwenye kioo. Nguo zake zimekuwa matambara. Macho yake yameingia ndani, mashavu yake yameisha, tumbo lake limesinyaa. Labda aliona hali yake hasa ilivyokuwa, alielewa vema upotevu wake, hali yake ya kukosa msaada, hali yake isiyo na tumaini, jinsi alivyo mbali hasa na nyumbani (Waefeso 2:1-3, 1213; Warumi 5:6-10). Mawazo yake yakageukia nyumbani. Hisia zake zinafufuka anapohisi harufu za kuvutia za jikoni, anabaki katika njozi ya kila sura, anajitelekeza katika kumbukumbu za nyakati nzuri. Hata watumwa wanaishi kwa raha kuliko hali hii. Akaamua atakwenda kwa baba yake. Anafahamu hastahili kitu. Ameharibu urithi wake; hana haki tena katika nyumba ya baba yake. Labda angemchukua kama mtumishi. Hana cha kupoteza.


Baba Mzuri Kupita Kiasi

 

Katika moja ya mifano mizuri kwenye Maandiko kwa ajili ya Baba Yetu wa Mbinguni, baba yake huyu kijana kila siku anajitokeza, akiangalia kwa macho ya kutamani kumuona mwana wake mpotevu njiani. Na anapomuona kwa mbali, moyo wake unaruka na miguu yake inaanza kukimbia. Anamkumbatia, anamuinua na kumzungusha. Kisha anamuweka tena chini, na kumshikilia usawa wa mikono, akimtazama sana usoni mwake, kisha anamvuta kwake tena na kumkumbatia kwa nguvu. Mtoto huyu anasema kitu kuhusu kuwa mmoja wa watumishi wake, lakini baba wala hasikii chochote. Anazungumzia nini! Huyu ni mwana wake aliyekuwa amepotea! Aliyekuwa amekufa lakini sasa amefufuka! Anahitaji chakula. Anahitaji nguo. Anahitaji kumwambia kisa chake, lakini hilo linaweza kusubiri. “Harakisha” anawaita watumishi wake ambao wamefuatilia kuona kelele hizi ni za nini. “Leta nguo nzuri mvishe. Weka pete kwenye kidole chake na viatu miguuni mwake. Leta ndama aliyenona na mchinje. Hebu na tuwe na sherehe na kusherehekea. Maana huyu mwana wangu alikuwa amekufa na amefufuka tena; alikuwa amepotea na sasa amepatikana!”

 

Ndivyo ilivyo kwetu pia. “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine. Lakini Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda; hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema. Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu; ili katika zamani zinazokuja audhihirishe wingi wa neema yake upitao kiasi kwa wema wake kwetu sisi katika Kristo Yesu. Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.” (Waefeso 2:1-9)

 

Imechapwa tena kutoka kwa Karen & Ron Flowers, Understanding Families. Silver Spring, MD: Idara ya Huduma za Familia Konferensi Kuu ya Waadventista Wasabato, 2000.