Seventh-day Adventist® Church

PASTOR LETTA'S OFFICIAL WEBSITE

Menu

KARAMA ZA KIROHO

KARAMA ZA KIROHO

Usimamizi/Utawala

Karama ya usimamizi ni uwezo maalumu ambao Mungu huutoa kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kanisa ili watambue kwa usahihi malengo ya muda mfupi na ya muda mrefu ya kundi husika la mwili wa Kristo na kisha kubuni na kutekeleza mipango mbalimbali ya kuyafikia malengo hayo. (1 Kor. 12:28; Matendo 6:1-7; Matendo 27:11; Luka 14:28-30; Tito 1:5.)

Kupambanua Roho

Karama ya Kupambanua Roho ni uwezo maalumu Mungu anaoutoa kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kujua kwa uhakika iwapo tabia fulani fulani zinazodhaniwa kuwa ni za Mungu kiuhalisia ni za Mungu, za kibinadamu, ama za kishetani. (1 Wakorintho 12:10; Matendo 5:1-7; Matendo 16:16-18; Yohana 4:1-6; Mathayo 16:21-23.)

Uinjilisti

Karama ya Uinjilisti ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kushiriki Injili na wasio waumini katika namna ambayo wanaume na wanawake wanakuwa wafuasi wa Yesu na waumini wanaowajibika wa mwili wa Kristo. (Waefeso 4:11-14; 2 Timotheo 4:5; Matendo 8:5-6; Matendo 8:26-40; Matendo 14:21; Matendo 21:8.)

Kufariji 

Karama ya Kufariji ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kuhudumu kwa maneno ya faraja, ya kutia moyo, na kushauri washiriki wengine wa mwili wa Kristo katika namna watakayojihisi wamesaidiwa na kuponywa. (Warumi 12:8; 1 Timotheo 4:13; Waebrania 10:25; Matendo 14:22.)

Imani

Karama ya Imani ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kutambua kwa kiwango cha kujiamini kusiko kwa kawaida nia na makusudi ya Mungu kwa kazi yake. (1 Wakorintho 12:9; Matendo 11:22-24; Matendo 27:21-25; Waebrania 11; Warumi 4:18-21.)

Kukirimu

Karama ya Kukirimu ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kuchangia mali zao kwa kazi ya Bwana kwa hiari na uchangamfu. (Warumi 12:8; 2Wakorintho 8:1-7; 2Wakorintho 9:2-8; Marko 12:41-44.)

Kuponya

Karama ya Kuponya ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kutumika kama waombezi wa kibinadamu ambao kupitia kwao, na pale inapompendeza Mungu, hutibu maradhi na kurejesha afya bila kutumia zile njia zingine za asili za uponyaji. (1Wakorintho 12:9, 28; Matendo 3:1-10; Matendo 5:12-16; Matendo 9:32-35; Matendo 28:7-10.)

Masaidiano

Karama ya Masaidiano ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo, kuwekeza karama walizonazo kanisani na hivyo kuwawezesha wengine kukuza karama zao za kiroho. (1Wakorintho 12:28; Warumi 16:1-2; Matendo 9:36; Luka 8:2-3; Marko 15:40-41.)

Ukarimu

Karama ya Ukarimu ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kwa njia ya kutoa nafasi nyumbani mwao wakiwakaribisha wenye uhitaji wa chakula na malazi kwa moyo uliochangamka. (1Petro 4:9; Warumi 12:9-13; Warumi 16:23; Matendo 6:14-15; Hesabu 13:1-2.)

Maombezi

Karama ya Maombezi ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kuomba kwa muda wa ziada kwa utaratibu wa kudumu na kushuhudia maombi yao maalumu yakijibiwa mara kwa mara kwa kiwango kilicho kikubwa zaidi ya kile kinachotarajiwa na Wakristo wa kawaida. (Yakobo 5:14-16; 1Timotheo 2:1-2; Wakolosai 1:9-12; Wakolosai 4: 12-13; Matendo 12:12; Luka 22:41-44.)

Maarifa

Karama ya Maarifa ni uwezo maalum ambao Mungu huutoa kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo ili kugundua, kuzitunza, kuziainisha, na kuzichambua taarifa na dhana muhimu zinazoweza kusaidia katika ukuaji, na ustawi wa Kanisa. (1Wakorintho 2:14; 1Wakorintho 12:8; Matendo 5:1-11; Wakolosai 2:2-3; 2Wakorintho 11:6.)

Uongozi

Karama ya Uongozi ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kuweka malengo ya siku za usoni, kulingana na makusudi ya Mungu, na kuyawasilisha malengo haya kwa wengine katika namna itakayowafanya wajitoe kwa hiari na kwa kushirikiana kuyakamilisha makusudi haya kwa utukufu wa Mungu. (1Timotheo 5:17; Matendo 7:10; Matendo 15:7-11; Warumi 12:8; Waebrania 13:17; Luka 9:51.)

Rehema/Huruma

Karama ya Rehema ni uwezo maalum Mungu autoao kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kuhisi huruma ya kweli kwa wakristo na wasio wakristo wanaopitia maumivu na matatizo ya kimwili, kiakili, au kisaikolojia na kuitafsiri huruma hiyo katika matendo ya uchangamfu, yanayoakisi upendo wa Kristo, na yanayolenga kupunguza maumivu. (Warumi 12:8; Marko 9:41; Matendo 16:33-34; Luka 10:33-35; Mathayo 20:29-34; Mathayo 25:34-40; Matendo 11:28-30.)

Umishenari

Karama ya Umishenari ni uwezo maalum ambao Mungu huutoa kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo ili watumikie karama zingine za kiroho walizonazo katika tamaduni nyingine. (1Wakorintho 9:19-23; Matendo 8:4; Matendo 13:2-3; Matendo 22:21; Warumi 10:15.)

Uchungaji

Karama ya Uchungaji ni uwezo maalum ambao Mungu huutoa kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo ili wachukue jukumu la kudumu la uwajibikaji wa binafsi wa hali ya kiroho ya kundi la waaminio. (Waefeso 4:11-14; 1Timotheo 3:1-7; Yohana 10:1-18; 1Petro 5:1-3.)

Kuhudumu

Karama ya Kuhudumu ni uwezo maalum ambao Mungu huutoa kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo ili waainishe mahitaji yasiyotimizwa, huku wakijihusisha na shughuli zinazoshabihiana na kazi ya Mungu, na kutumia rasilimali zinazopatikana kutimiza mahitaji hayo na kusaidia kuyafikia malengo yaliyokusudiwa. (2Timotheo 1:16-18; Warumi 12:7; Matendo 6:1-7; Tito 3:14; Wagalatia 6:2, 10.)

Ualimu

Karama ya Ualimu ni uwezo maalum ambao Mungu huutoa kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo kuwasilisha taarifa zinazohusu afya na utumishi wa  mwili wa Kristo kwa waumini wake katika namna ya kuwafanya wajifunze. 1Wakorintho 12:28; Waefeso 4:11-14; Warumi 12:7; Matendo 18:20:20-21

Hekima

Karama ya Hekima ni uwezo maalum autoao Mungu kwa baadhi ya washiriki wa mwili wa Kristo ili waijue nia ya Roho Mtakatifu kupitia maarifa yaliyotolewa na namna ya kuyatumia maarifa hayo kwenye mahitaji maalum ya kanisa. 1Wakorintho 2:1-13; 1Wakorintho 12:8; Matendo 6:3,10; Yakobo 1:5-6; 2Petro 3:15-16.