|
PITA KOTE KOTE 1. Ipaze sauti yako, kuihubiri injili, Wajulishe ndugu zako, wakaribu na wa mbali, Wasihi jirani zako, Mwokozi wamkubali, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 2. Pita kwenye njia kuu, na pia vichochoroni, Sauti ipae juu, isikike milimani, Iwapatie nafuu, waishio mabondeni, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 3. Pita katika vijiji, watembelee mijini, Hubiri kwenye majiji, wasikie ghorofani, Kwamba Mungu muumbaji, tawapatia amani, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 4. Pita kote kwa bidii, porini na mashambani, Wajulishe watalii, na walio viwandani, Wasifanye usanii, kwenye mambo ya imani, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 5. Pita pita masokoni, ongea na wachuuzi, Nenda hospitalini, wafundishe wauguzi, Kwamba hivi karibuni, watamwona Mkombozi, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 6. Vyuoni pia shuleni, kahubiri mabwenini, Wanafunzi darasani, na walimu ofisini, Walio maabarani, wote wadumu salani, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 7. Wageni mahotelini, kwenye nyumba za wageni, Wanasayansi angani, wanaokwenda mwezini, Warudipo duniani, waonywe kwa umakini, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 8. Danguroni makahaba, wanaoishi gizani Wasifiao mahaba, kwa kuzini hadharani, Waoneshwe msalaba, ili warudi mwangani, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 9. Inua paza sauti, isikike gerezani, Kwa pendo bila shuruti, waelekezwe mbinguni, Wayakimbie mauti, wakajazwe tumaini, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. 10. Haya sasa nenda kote, kwa nguvu zake Mwokozi, Hubiri kwa nguvu zote, ikibidi kwa machozi, Ijaze dunia yote, na neno la ukombozi, Pita pita kote kote, wafundishe watu wote. --------------------------------------------------- Christopher R. Mwashinga (Sauti Toka Ughaibuni) |
PIGA SIMU JU MBINGUNI 1. Wasimama dirishani, nje unaangalia, Moyoni unatamani, kwa makelele kulia, Kwa kuwa wako mwandani, amekwishakuchunia, Piga simu ju mbinguni, daima utajibiwa. 2. Moyoni unahuzuni, jirani kakununia, Watazama mawinguni, mengi unayawazia, Ndugu sijione duni, hayo mambo ya dunia, Piga simu ju mbinguni, daima utajibiwa. 3. Kila upigapo simu, mwandani kikukatia, Kukupa maji ya ndimu, matusi kukurushia, Au kukwita hasimu, uongo kukuzushia, Piga simu ju mbinguni, daima utajibiwa. 4. Watu wakikuhujumu, ubaya kukufanyia, Ukashindwa kujikimu, au kujihudumia, Jua huo ni msimu, utapita vumilia, Piga simu juu mbinguni, daima utajibiwa. 5. Upatwapo na maradhi, kitanda kukilalia, Watu waovu baadhi, wakakunyanyapalia, Wakiitamani ardhi, ije kukukumbatia, Piga simu ju mbinguni, daima utajibiwa. 6. Ubambikiwapo kesi, kortini ukaingia, Ukasikia tetesi, hakimu ameridhia, Uswekwe ndani upesi, upate kuangamia, Piga simu ju mbinguni, daima utajibiwa. 7. Usotapo gerezani, usiku kucha kulia, Kuogelea gizani, nuru kuitamania, Na huku mwovu Shetani, hofu akikupatia, Piga simu ju mbinguni, daima utajibiwa. 8. Mvua igomapo nyesha, mazao yakafifia, Hadi ukapata presha, kwa uchungu ukalia, Mungu atakuwezesha, ukimtumainia, Piga simu ju mbinguni, daima utajibiwa. 9. Kadi tama narudia, piga simu usichoke, Mungu atakusikia, takwondolea upweke, Yeye ukishamwambia, inabaki kazi kwake, Piga simu ju mbinguni, daima utajibiwa. ------------------------------------------------------------- Christopher R. Mwashinga (Sauti Toka Ughaibuni) |
MTI USIO NA TUNDA 1. Pole nimekusikia, machozi nimeyaona, Watu wamekununia, moyoni unasonona, Watamani kukimbia, huzuni imekubana, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. 2. Kama unapigwa mawe, usiku pia mchana, Watu wenye chuki nawe, watamani kukuchana, Jua mambo yako wewe, sasa yamekwisha fana, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. 3. Kama watu wakusema, japo huna konakona, Hiyo ni dalili njema, sali mshukuru Bwana, Matunda yako ni mema, wengi wameshayaona, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. 4. Kama wanaleta visa, matusi kukutukana, Wakija kukutikisa, kwa yasiyo na maana, Jua hayo kwako tisa, cheza piga danadana, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. 5. Kama wakikusudia, kukufanyia hiyana, Kutangazia dunia, kwamba wewe huna mana, Ndugu yangu vumilia, jiepushe kuzozana, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. 6. Kama hilo jua lako, liangazalo mchana, Lamulika njia yako, tangu siku za ujana, Hapo jua fyucha yako, ina upepo mwanana, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. 7. Kama unapigwa mawe, kamshukuru Rabana, Shukuru usichelewe, usianze kutukana, Kwani mti wako wewe, wapendeza kwa shehena, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. 8. Kama watupiwa mawe, na wazee na vijana, Usiingie kiwewe, na kuanza kubishana, Bali kwepa kila jiwe, kwa hekima yake Bwana, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. 9. Beti tisa zinatosha, sihitaji sema sana, Njia nimekuonesha, wewe mtu wa maana, Watu wanapokutisha, wambie leo si jana, Mti usio na tunda, kamwe haupigwi mawe. ---------------------------------------------------- Christopher R. Mwashinga (Sauti Toka Ughaibuni) JUA ZURI LITUALO 1. Mchana ulipoanza, kwa radi nyingi na mvua, Wenyeji walojibanza, walianza kutimua, Wageni wakajifunza, kwa chozi kuomba dua, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 2. Tufani kila upande, imegoma kupungua, Waipende wasipende, watu waweza ugua, Wafanyaje wajilinde, na ugonjwa wa mafua? Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 3. Mchana hadi jioni, hatukuliona jua, Kisha pepo za kusini, zikavuma kwa hatua, Zikaondoa tufani, mambo yakawa murua, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 4. Ni jioni ona jua, magharibi linatua, Rangize kama maua, mwangaza unachanua, Hali ya hewa murua, koti la mvua navua, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 5. Anga la kisamawati, hakuna wingu la mvua, Huu sasa ni wakati, mandhari kufurahia, Na kuweka mikakati, ubunifu kuibua, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 6. Mdomoni ninakiri, moyoni nimetambua, Mambo yaliyo mazuri, yote ukiyachungua, Mungu wetu mashuhuri, ndo aliyoyavumbua, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 7. Mambo mengi yapendeza, kama upinde wa mvua, Hata mwenye makengeza, akiona atajua, Ya kwamba Mungu muweza, apanga na kupangua, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 8. Wavaao nguo chafu, mambo wakishatibua, Kwa matendo ya uchafu, maovu wakitubia, Mungu wetu mtukufu, nguo zao atafua, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 9. Kama ua la waridi, furaha itachanua, Na kama zabarijadi, Mungu atawachukua, Kuwapatia zawadi, wokovu kufurahia, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 10 Hivyo wewe mwenye dhambi, kwa nini wajisumbua? Njoo na yako mavumbi, Mungu hatokuumbua, Atakusafisha dhambi, nawe utashangilia, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. 11. Akishafuta adhabu, juu akikuinua, Utapendeza ajabu, zidi mwangaza wa jua, Kwani yazidi dhahabu, bei alokununua, Jua zuri litualo, kulitazama ni kheri. ---------------------------------------------------------- Christopher R. Mwashinga (Sauti Toka Ughaibuni) |
KUNA SIKU UTAVUNA ( A ) ( B ) |
|
MWANAMKE NDO KIPIMO 1. Kama wataka kujua, jamii yako ilipo, Kama inaendelea, kwa mapato na malipo, Au inasuasua, kwa kudhani nayo ipo, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 2. Ukiona mwanamke, mapato yake madogo, Na pia elimu yake, imezungukwa na zogo, Jua hiyo nchi yake, uchumi wake mdogo, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 3. Ukiona mwanamke, atembea kwa miguu, Kabeba watoto wake, pamoja na wajukuu, Jua usafiri kwake, ndo tatizo lake kuu, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 4. Ukiona mwanamke, anabebwa machelani, Na kujifungua kwake, siku zote ni nyumbani, Jua hiyo afya yake, ndiyo kero ya moyoni, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 5. Ukiona mwanamke, anabeba zake kuni, Pamoja na maji yake, mgongoni na kichwani, Jua familia yake, haina raha nyumbani, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 6. Ukiona mwanamke, pekupeku atembea, Mavumbi kichwani mwake, huku anachechemea, Ujue uchumi wake, umekwishatokomea, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 7. Ukiona mwanamke, mdomowe umezibwa, Makovu mwilini mwake, kila siku anazabwa, Jua maishani mwake, haki zake zimeibwa, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 8. Ukiona mwanamke, machozi tele shavuni, Kapoteza sura yake, kwa kutopata sabuni, Ujue moyoni mwake, mwisho uko karibuni, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 9. Mwanamke ndo kipimo, cha nchi ilositawi, Kama shina kwenye shimo, na matunda kwenye tawi, Mwanamke ni kipimo, cha nchi ilositawi, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 10 Kamwe nchi haikui, kumpita mwanamke, Na hata kama hajui, yeye ndo kipimo chake, Mawingu hayapungui, mpaka apate chake, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. 11. Kaditama namaliza, kompyuta naweka chini, Uanze kujiuliza, yatafakari moyoni, Kisha ukisha maliza, jadili mtandaoni, Mwanamke ndo kipimo, cha ukuu wa taifa. --------------------------------------------------------- Christopher R. Mwashinga (Sauti Toka Ughaibuni) |
TUMEITWA TUWE TOFAUTI |
|
SIRI SI SIRI TENA 1. Siri sii siri tena, itokapo kwa mmoja, Jambo ukishalinena, hata kwa mtu mmoja, Hilo sii siri tena, tayari limeshavuja, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 2. Mwingine ukimwambia, hapo siri imekufa, Hata kama ukilia, umeshaupata ufa, Na usipoangalia, utayapata maafa, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 3. Aweza kuwa rafiki, pale unapomwambia, Akakufaa kwa dhiki, huduma kukupatia, Maneno kama muziki, sikioni kukwambia, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 4. Siku akibadilika, utaisoma nambari, Juani takuanika, bila kujali hatari, Wewe ukihangaika, yeye taona fahari, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 5 Siri ukishaitoa, rafikiyo kumwambia, Aweza kukutoboa, huwezi kumzuia, Nyundo ya kukubomoa, umekwishampatia, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 6. Kumdhibiti huwezi, umeshampa upanga, Umejipa utelezi, umeshafanya ujinga, Akikwita mtembezi, ni vigumu kumpinga, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 7. Aweza kukutangaza, kila kona ya dunia, Chini kukugaragaza, bila kukuhurumia, Hata ukimkataza, hawezi kukusikia, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 8. Hivyo hiyo siri yako, ukipenda iwe siri, Itunze moyoni mwako, kamwe usiihubiri, Leo umakini wako, kesho utakusitiri, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 9 Kushindwa kutunza siri, ni ugonjwa wa mauti, Kama unao tayari, wewe sasa mahututi, Wahitaji daktari, mwenye nguvu madhubuti, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. 10. Mwombe Mungu wa mbinguni, ushindi akupatie, Uiepuke huzuni, mauti uyakimbie, Uwapo ulimwenguni, maisha ufurahie, Siri sii siri tena, itokapo mdomoni. ---------------------------------------------------------- Christopher R. Mwashinga (Sauti Toka Ughaibuni) |
USIACHE MBACHAO |
|
AKILI BILA HEKIMA Mwanakwetu sikiliza, neno langu zingatia, |