Seventh-day Adventist® Church

PASTOR LETTA'S OFFICIAL WEBSITE

Menu

UWANJA WA MASHAIRI


KAMA UNATAKA MALI, MTAIPATA SHAMBANI

Karudi Baba mmoja, toka safari ya mbali,
Kavimba yote mapaja, na kutetemeka mwili,
Watoto wake wakaja, ili kumtaka hali,
Wakataka na kauli, iwafae maishani.

Akatamka mgonjwa, ninaumwa kweli kweli,
Hata kama nikichanjwa, haitoki homa kali,
Roho naona yachinjwa, kifo kinanikabili,
Kama mwataka kauli, semani niseme nini.

Yakawatoka kinywani, maneno yenye adili,
Baba yetu wa thamani, sisi tunataka mali,
Urith tunatamani, mali yetu ya halali,
Sema iko wapi mali, itufae maishani.

Baba aliye kufani, akajibu lile swali,
Nina kufa maskini, baba yenu sina mali,
Neno moja lishikeni, kama mnataka mali,
Kama mnataka mali, mtayapata shambani.

Wakazidi kumchimba, baba mwenye homa kali,
Baba yetu watufumba, hatujui fumbo hili,
Akili yetu nyembamba, haijajua methali,
Kama tunataka mali, tutapataje shambani.

Kwanza shirikianeni, nawapa hiyo kauli,
Fanyeni kazi shambani, mwisho mtapata mali,
Haya sasa buriani, kifo kimeniwasili,
Kama mnataka mali mtayapata shambani.

Alipokwisha kutaja, fumbo hili la akili,
Mauti nayo yakaja, roho ikaacha mwili,
Na watoto kwa umoja, wakakumbuka kauli,
Kama mnataka mali, mtayapata shambani.

Fumbo wakatafakari, watoto wale wawili,
Wakakata na shauri, baada ya siku mbili,
Wote wakawa tayari, pori nene kukabili,
Kama mnataka mali, mtayapata shambani.

Wakazipanda shambani, mbegu nyingi mbalimbali,
Tangu zile za mibuni, hata zitupazo wali,
Mvua ikaja chini, wakaona na dalili,
Kama mnataka mali, mtayapata shambani.

Shamba wakapalilia, bila kupata ajali.
Mavuno yakawajia, wakafaidi ugali,
Wote wakashangilia, usemi wakakubali,
Kama mnataka mali, mtayapata shambani.

Wakawanunua ngómbe, majike kwa mafahali,
Wakapata na vikombe, mavazi na baskeli,
Hawakuitaka pombe, sababu pombe si mali,
Kama mnataka mali, mtayapata shambani.

Wakaongeza mazao, na nyumba za matofali,
Pale penye shamba lao, wakaihubiri mali,
Wakakiweka kibao, wakaandika kauili,
KAMA MNATAKA MALI, MTAYAPATA SHAMBANI.


SIZITAKI MBICHI HIZI

Hadithi inayokuja, ni ya Sungura sikia,
Hadithi uliyongoja, leo ninakuletea,
Alitoka siku moja, njaa aliposikia,
Njaa aliposikia, Sungura nakuambia.

Siku ile akaenda, porini kutembelea,
Akayaona matunda, mtini yameenea,
Sungura akayapenda, mtini akasogea,
Mtini akasogea, Sungura nakuambia.

Sungura karukaruka, lakini hakufikia,
Matunda hakuyashika, mikononi hakutia,
Hakika alisumbuka, nguvuze zikapungua,
Nguvuze zikapungua Sungura nakuambia.

Mtazame hapo juu Sungura amelegea,
Mtazame na miguu, matunda anarukia,
Atafanya sikukuu, matunda akifikia,
Matunda akifikia, Sungura nakuambia.

Karuka tena karuka, matunda akarukia,
Mwisho Wave akachoka, kachoka hata mkia,
Penye mti akatoka, pembeni akasogea,
Pembeni akasogea, Sungura nakuambia.

“Sizitaki mbichi hizi” Sungura akagumia,
“Naona nafanya kazi, bila faida kujua”,
Yakamtoka machozi matunda akalilia,
Matunda akalilia, Sungura nakuambia.

Sio kama hakutaka, sasa nakupasulia,
Matunda aliyataka, ndiyo kisa akalia
Tunajua hakufika, alichoka kurukia,
Alichoka kurukia, Sungura nakuambia.

Hadithi nimemaliza, nimekwisha simulia,
Jambo moja sikiliza, rafiki yangu sikia,
Usikose kujikaza, mazuri kukazania,
Utamshinda Sungura, utapata mbivu pia.